Moja kwa moja, Marekani yaendelea na mashambulizi dhidi ya Iran huku miundombinu ya Bandar Abbas ikilengwa

Marekani yaanzisha wimbi la sita la mashambulizi dhidi ya Iran, yalenga madaraja na uwanja wa ndege

Ruka Video uendelee
  • xx
  • xx
  • xx
  • Lungu
  • xx
  • xx
  • d
  • s
  • a
  • Sonko
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • xx
  • Dangote
  • xx
  • Lydia Wanjiku

Moja kwa moja

Na Mariam Mjahid & Ambia Hirsi

  1. Wamarekani saba wawekwa karantini katika kituo cha Ebola nchini Kenya

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Wafanyakazi saba wa misaada kutoka Marekani, ambao walikuwa nchini Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo kusaidia juhudi za kukabiliana na mlipuko wa Ebola, wamewekwa karantini nchini Kenya baada ya serikali ya Marekani kuweka masharti mapya ya usafiri kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters na mkuu wa shirika la misaada la Marekani lililowaajiri.

    Wafanyakazi hao wa misaada ni wa kwanza kuwekwa karantini katika kituo hicho, ambacho ujenzi wake ulipingwa vikali nchini Kenya na kesi dhidi yake inaendelea mahakamani, baada ya jaji kuamuru shughuli katika za kuistishwa hadi uamuzi utakapotolewa.

    Licha ya agizo hilo la mahakama kituo hicho kimeendelea na shughuli zake, kulingana na maafisa wa Marekani na picha za satelaiti zilizochunguzwa na Reuters.

    Sera mpya ya Washington inaeleza kuwa raia wa Marekani wanaorejea kutoka DR Congo, ambako kuna mlipuko wa Ebola, lazima wakae kwa wiki tatu katika nchi ya tatu kabla ya kuingia Marekani.

    Mwezi uliopita, Waziri wa Afya wa Kenya Adan Duale alitangaza kusimamishwa mara moja kwa ujenzi wa kituo hicho baada ya serikali kupatikana na hatia ya kupuuza mahakama kwa kushindwa kutii amri za kusimamisha ujenzi wa kituo hicho cha karantini.

    Unaweza kusoma:

  2. Iran yazionya nchi za Ghuba dhidi ya kuruhusu Marekani kutumia ardhi yake kushambulia Iran

    d

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Iran imezionya nchi za Ghuba dhidi ya kuruhusu Marekani kutumia ardhi, anga au maji yake kuanzisha mashambulizi dhidi ya Iran, ikisema hatua hiyo itakuwa na matokeo makubwa kwa mataifa husika.

    Mwenyekiti wa Kamati ya Masuala ya Ndani ya Bunge la Iran, Mohammad Saleh Jokar, amesema iwapo Marekani itatumia eneo la nchi hizo kushambulia Iran, zitakabiliwa na “gharama kubwa sana” kutokana na uamuzi huo.

    Wakati huo huo, Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran imesema kurejeshwa kwa vizuizi vya shughuli za majini ni sehemu nyingine ya kile ilichokitaja kuwa ukiukaji wa makubaliano kati ya Tehran na Washington.

    Katika taarifa yake, wizara hiyo pia iliishutumu Marekani kwa kile ilichodai ni uhalifu wa kivita, ikitaja mashambulizi dhidi ya miundombinu na huduma za kiraia.

    Iran iliorodhesha miongoni mwa maeneo yaliyolengwa kuwa ni kituo cha matibabu cha Kikosi cha 388 cha Jeshi la Iran mjini Bampour, eneo la kuhifadhi nafaka la Hoveizeh na mnara wa ulinzi wa wanamaji wa Chabahar.

    Aidha, Tehran imedai kuwa hii ni mara ya tatu ndani ya mwaka mmoja kwa Marekani kuishambulia Iran wakati mazungumzo kati ya pande hizo yakiendelea.

    Iran imezitaka nchi za eneo hilo kutoruhusu ardhi, anga au maji yake kutumiwa katika mashambulizi dhidi yake, ikisema inalenga kuimarisha uelewano na ushirikiano wa kikanda bila uwepo au kuingiliwa na Marekani.

    Jokar pia amezitaka nchi za Ghuba kujifunza kutokana na kile alichokiita “uzoefu wa Vita vya Ramadhani” na kutozikabidhi ardhi na fukwe zao kwa majeshi ya Marekani.

    Pia Soma:

  3. Kombe la Dunia kusafirishwa kwa sanduku maalum la Louis Vuitton

    d

    Chanzo cha picha, Reuters

    Kombe la Dunia litawasili katika uwanja wa New York New Jersey likiwa ndani ya sanduku maalum lililobuniwa na kampuni ya kifahari ya Louis Vuitton, ambayo imeendelea kuaminiwa na FIFA kubuni kifaa cha kubebea moja ya tuzo zenye hadhi kubwa zaidi katika mchezo wa soka.

    Sanduku hilo limepambwa kwa herufi ya dhahabu V, inayowakilisha neno Victory yaani ushindi, pamoja na jina la kampuni hiyo. Pia lina nembo maarufu ya Louis Vuitton na kingo za shaba zilizopakwa dhahabu.

    Kwa ndani, sanduku hilo limefunikwa kwa ngozi ya rangi ya beige na lina alama maalum ya kuadhimisha ushirikiano kati ya FIFA na Louis Vuitton.

    Hii ni mara ya tano mfululizo kwa kampuni hiyo ya Ufaransa kubuni sanduku la kubebea Kombe la Dunia, baada ya kufanya hivyo katika fainali za mwaka 2010, 2014, 2018 na 2022.

    "Mashirikiano ya Louis Vuitton na FIFA kwa zaidi ya muongo mmoja yamejengwa juu ya dhamira ya pamoja ya ubora na imani kwamba michezo ina uwezo wa kuhamasisha na kuwaunganisha watu duniani," alisema Mwenyekiti na Mtendaji Mkuu wa Louis Vuitton, Pietro Beccari.

    Kwa muda mrefu, kampuni za bidhaa za kifahari zimekuwa zikijenga ushirikiano na michezo ya kiwango cha juu. Louis Vuitton pia hutengeneza masanduku maalum ya kubebea makombe ya Formula One, huku Tiffany and Co. ikiwa imetengeneza Kombe la Vince Lombardi linalotolewa kwa mabingwa wa Super Bowl tangu mwaka 1967.

    Kombe la Dunia, ambalo kwa kawaida huhifadhiwa katika Makumbusho ya FIFA mjini Zurich, ni kombe moja pekee linalotolewa kwa mabingwa wa dunia kila baada ya miaka minne. Hivyo, jukumu la kubuni sanduku lake maalum la usafirishaji linaendelea kuwa moja ya heshima kubwa katika ushirikiano kati ya FIFA na Louis Vuitton.

    Soma Zaidi:

  4. JD Vance aishutumu Israel kwa kujaribu kushawishi Wamarekani kuendeleza vita dhidi ya Iran

    f

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Makamu wa Rais wa Marekani JD Vance amesema baadhi ya maafisa wa serikali ya Israel wanajaribu kuishawishi Marekani kuendeleza vita dhidi ya Iran.

    Katika mahojiano yaliyochapishwa Jumatano kwenye podikasti ya The Joe Rogan Experience, Vance amesema ana imani na baadhi ya viongozi wa Israel lakini akadai wengine “wanacheza michezo ya kisiasa na kujaribu kuwavuta Wamarekani katika vita visivyo na mwisho.”

    Vance alisema anaamini wasikilizaji wameelewa kile alichokiita "mpango wa siri na wa gharama kubwa" unaolenga kuvuruga mazungumzo na kuzuia kufikiwa kwa makubaliano kati ya Marekani na Iran.

    "Nina hakika mmeona mpango huu wa siri na wa gharama kubwa unaolenga kuvuruga mazungumzo na kuzuia kufikiwa kwa makubaliano," alisema.

    Mwezi uliopita, Marekani na Iran zilitangaza kuwa zimefikia makubaliano ya awali ya kuendelea na mazungumzo. Kwa mujibu wa taarifa hizo, pande hizo pia zilikubaliana kufanyia kazi mpango wa usitishaji mapigano wa siku 60 na hatua za kufungua tena Mlango wa Hormuz, ingawa mazungumzo hayo yamekuwa yakikumbwa na changamoto.

    Serikali ya Israel haikutoa tamko la haraka kujibu kauli hizo.

    Vance amesema ni jambo la kawaida katika mahusiano ya kimataifa kwa maafisa wa nchi washirika kujaribu kushawishi sera za Marekani, lakini akasisitiza kuwa wasiwasi wake ni iwapo maafisa wa Marekani watakubali shinikizo hilo.

    Kauli hizo zinakuja wakati utawala wa Donald Trump ukiendelea kutafuta njia ya kumaliza mzozo na Iran kupitia mazungumzo au hatua za kijeshi.

    Wakati huo huo, Baraza la Wawakilishi la Marekani limekataa pendekezo la kupunguza mabilioni ya dola ya msaada wa Marekani kwa Israel.

    Pia Soma:

  5. Takriban wanafunzi 20 wafariki dunia katika ajali ya basi la shule mashariki mwa Uganda

    H

    Chanzo cha picha, MITANDAONI/X

    Maelezo ya picha, Basi la shule ya King David nchini Uganda lililopata ajali

    Takriban wanafunzi 20 wamefariki dunia baada ya basi la King David Junior School, Ndejje kupata ajali usiku wa kuamkia leo katika wilaya ya Kapchorwa, mashariki mwa Uganda, mamlaka zimesema.

    Basi hilo lilikuwa likiwarejesha wanafunzi kutoka ziara ya masomo Alhamisi usiku lilipodaiwa kupata hitilafu ya kiufundi majira ya saa mbili usiku.

    Kwa mujibu wa taarifa za awali za polisi, dereva alipoteza udhibiti wa basi kabla ya kugonga, na kusababisha ajali hiyo mbaya.

    "Uchunguzi wa awali unaashiria kuwa basi lilipoteza mwelekeo kutokana na hitilafu ya kiufundi. Pia tumebaini kupitia ushahidi wa mashuhuda kuwa gari hilo lilisimama mara kadhaa kabla ya ajali kutokea," polisi walisema katika taarifa iliyotumwa kwa mitandao ya kijamii.

    Shughuli za uokoaji zinaendelea huku majeruhi wakipelekwa katika vituo vya afya vilivyo karibu.

    Uchunguzi unaendelea ili kubaini chanzo halisi cha ajali hiyo.

    Ajali hiyo imezua simanzi nchini Uganda, wakati familia za wanafunzi na viongozi wa shule wakisubiri taarifa rasmi kuhusu hatima ya waliokuwa ndani ya basi hilo.

    H

    Chanzo cha picha, Social Media

    Maelezo ya picha, Majeruhi akipokea matibabu ya dharura katika hospitali nchini Uganda
  6. Wahouthi watishia kushambulia miundombinu ya mafuta ya Saudi Arabia

    Waasi wa Houthi kutoka Yemen ni miongoni mwa washirika wakuu wa Iran katika ukanda wa Mashariki ya Kati, na kwa muda mrefu wamekuwa wakijihusisha na mashambulizi ya hapa na pale dhidi ya Israel tangu vita vya Gaza vilipoanza Oktoba 2023.

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Waasi wa Houthi kutoka Yemen ni miongoni mwa washirika wakuu wa Iran katika ukanda wa Mashariki ya Kati, na kwa muda mrefu wamekuwa wakijihusisha na mashambulizi ya hapa na pale dhidi ya Israel tangu vita vya Gaza vilipoanza Oktoba 2023.

    Waasi wa Kihouthi nchini Yemen wameionya Saudi Arabia kuwa watalenga miundombinu ya mafuta na maeneo mengine muhimu iwapo mapigano kati ya pande hizo yataongezeka.

    Kiongozi wa Wahouthi, Abdulmalik Al Houthi, amesema iwapo Saudi Arabia itaanzisha mashambulizi makubwa dhidi ya Yemen na kuzidisha mzozo huo, vituo vyake vya mafuta na maeneo mengine muhimu vitakuwa shabaha ya makombora na ndege zisizo na rubani za Wahouthi.

    “Endapo Saudi Arabia itaanzisha mashambulizi makubwa dhidi ya nchi yetu na kuchochea mivutano, vituo vyake vyote vya mafuta na maeneo muhimu vitakuwa malengo ya makombora na ndege zetu zisizo na rubani,” alisema.

    Wahouthi wameishutumu Saudi Arabia kwa kushambulia Uwanja wa Ndege wa Sanaa Jumatatu, wakisema hatua hiyo ilikuwa jibu la shambulio lililolenga uwanja wa ndege nchini Saudi Arabia.

    Mashambulizi ya pande hizo yameelezwa kuwa makubwa zaidi tangu makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyofikiwa mwaka 2022.

    Kwa mujibu wa shirika la habari la AFP, Abdulmalik Al Houthi pia ametishia kuushambulia Uwanja wa Ndege wa Riyadh iwapo mashambulizi zaidi yatafanywa dhidi ya Uwanja wa Ndege wa Sanaa.

    “Kanuni ni hii: shamba likilengwa, nasi tutalenga shamba; bandari ikilengwa, nasi tutalenga bandari. Na tutaijibu hali ya mzingiro kwa mzingiro,” alisema.

    Serikali ya Yemen yenye makao yake mjini Aden, inayoungwa mkono na Saudi Arabia, imesema shambulio la Jumatatu dhidi ya Uwanja wa Ndege wa Sanaa lililenga kuzuia ndege kutoka Iran kutua katika uwanja huo.

    Kwa zaidi ya muongo mmoja, ndege zote zinazoingia katika anga ya Yemen zimekuwa zikihitaji kibali kutoka muungano wa kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia.

    Serikali ya Yemen na washirika wake wanadai Wahouthi na Iran wamekuwa wakikiuka utaratibu huo kwa kuanzisha safari za moja kwa moja za ndege kutoka Iran kuelekea Sanaa.

    Unaweza Kusoma Pia:

  7. Pakistan yasema upatanishi wa Marekani na Iran umekwama

    G

    Chanzo cha picha, Reuters

    Pakistan imesema juhudi zake za kupatanisha Marekani na Iran zinakabiliwa na changamoto kutokana na kuongezeka kwa mivutano kati ya mataifa hayo mawili, lakini mchakato huo haujasitishwa.

    Akizungumza katika mkutano wa kila wiki na wanahabari mjini Islamabad, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Pakistan, Tahir Andrabi, alikanusha madai kwamba Islamabad imeachana na jukumu lake la upatanishi baada ya mivutano kuzidi.

    “Tunatumaini mantiki ya amani na mazungumzo ndiyo itakayoshinda mwishowe,” alisema Andrabi.

    Aliongeza kuwa mchakato wa amani haukomi kabisa, bali unaweza kusimama kwa muda kabla ya kuendelea tena.

    Kwa mujibu wa Andrabi, misingi iliyowekwa katika Hati ya Makubaliano ya Islamabad kati ya Marekani na Iran bado ipo, na inaweza kutumika kurejesha mazungumzo pindi pande husika zitakapoona kuwa kuendelea kwa mivutano hakutaleta suluhisho.

    Pakistan imezitaka tena pande zote kujizuia na kuepuka hatua zozote zinazoweza kuzidisha mivutano na kuhatarisha amani na utulivu wa eneo hilo.

    Andrabi alisema Hati ya Makubaliano ya Islamabad, iliyowezeshwa na Pakistan, ni mfumo wa kudumu wa kukuza amani, kuheshimiana na ustawi wa pamoja, huku Islamabad ikiendelea kuhimiza kurejelewa kwa mazungumzo katika ngazi ya wataalamu.

    Pia alieleza matumaini kuwa pande zote zitaendelea kujikita katika njia ya mazungumzo na diplomasia ili kutatua masuala yaliyosalia.

    Akizungumzia kufungwa kwa Mlango Bahari wa Hormuz kufuatia mashambulizi ya Marekani na Iran dhidi ya kila upande, Andrabi alisema Pakistan inatumaini hali itarejea kuwa ya kawaida haraka na kusisitiza umuhimu wa kuhakikisha usalama wa njia hiyo muhimu ya kimataifa ya usafirishaji baharini.

    Pia Soma:

  8. Trump: Matokeo ya vita dhidi ya Iran yatajulikana hivi karibuni

    g

    Chanzo cha picha, Alex Brandon-Pool/Getty Images

    Rais wa Marekani Donald Trump amesema matokeo ya vita vinavyoendelea dhidi ya Iran yatajulikana hivi karibuni, akidai kuwa Marekani na Israel zinaendelea kupata mafanikio katika operesheni zao za kijeshi.

    Akizungumza katika hotuba yake, Trump alisema Marekani ina mkono wa juu katika mapambano hayo.

    “Mtaona matunda ya juhudi hizi hivi karibuni sana,” alisema. Trump pia alidai kuwa, “Tunashinda ushindi mkubwa dhidi ya Iran.”

    Hata hivyo, hakufafanua alichomaanisha kwa kauli hiyo wala kutoa ushahidi unaounga mkono madai yake.

    Kauli zake zimejiri wakati mapigano kati ya Iran, Marekani na Israel yakiendelea kushuhudia mashambulizi ya pande zote, huku Iran ikiwa haijatoa jibu la haraka kuhusu matamshi ya Trump.

    Maelezo zaidi:

  9. Marekani yaendelea na mashambulizi dhidi ya Iran huku miundombinu ya Bandar Abbas ikilengwa

    G

    Chanzo cha picha, SOCIAL MEDIA

    Marekani imeanzisha wimbi la sita la mashambulizi ya anga dhidi ya Iran, yakilenga uwanja wa ndege, kituo cha reli na madaraja kadhaa kusini mwa nchi karibu na Mlango Bahari wa Hormuz, kwa mujibu wa vyombo vya habari vya serikali ya Iran.

    Shirika la habari la Tasnim limeripoti kuwa ndege za kivita za Marekani zilirusha makombora yaliyolenga Uwanja wa Ndege wa Iranshahr, bila kutoa taarifa kuhusu kiwango cha uharibifu au iwapo kulikuwa na majeruhi.

    Shirika rasmi la habari la Iran na televisheni ya taifa vilisema milipuko mitatu ilisikika karibu na uwanja huo wa ndege, vikiongeza kuwa angalau kombora moja la Marekani lilipiga uwanja huo.

    Wakati huo huo, shirika la habari la Fars liliripoti kuwa daraja katika mji wa Bandar Khamir lililengwa katika shambulio la Marekani.

    Tasnim pia lilisema mashambulizi ya Marekani yalilenga madaraja matatu katika eneo la Khamir, mkoani Hormozgan.

    Mojawapo ya madaraja hayo linaunganisha Bandar Abbas na mji wa Lar katika mkoa wa Fars.

    Kwa mujibu wa Tasnim, mashambulizi hayo yalisababisha kukatika kwa umeme katika baadhi ya maeneo na kuvuruga huduma za mawasiliano ya simu. Marekani haijatoa tamko rasmi kuhusu mashambulizi hayo wala madai yaliyotolewa na vyombo vya habari vya Iran.

    Maelezo zaidi:

  10. Hujambo na karibu kwa matangazo ya moja kwa moja