Waziri Mkuu wa zamani wa Lebanon asema nchi yake imetelekezwa na jumuiya ya kimataifa
Aliyekuwa waziri mkuu wa Lebanon wakati wa vita vyake vya mwisho na Israel mwaka 2006 ameambia BBC kuwa nchi yake imetelekezwa na jumuiya ya kimataifa.
Fouad Siniora alisema ni jambo lisilokubalika kuiacha Lebanon isambaratike, na kulikuwa na ukosefu wa kujitolea linapokuja suala la kujaribu kurejesha amani.
“Sasa tuko katika hali ngumu sana inayohitaji juhudi za kweli ndani ya nchi, pia kwa upande wa Waarabu na kimataifa.
"Unaweza kushinikiza mambo - wakati mwingine hadi kufikia hatua ya kukaribia kusambaratika - katika janga kubwa bila kutambua baadaye itakuwa inamaanisha nini.
"Inatokea wakati utawala wa Marekani una shughuli nyingi na uchaguzi.
"Na hatuna uwezo wa kumchagua rais, kwa sababu baadhi ya makundi hasa Hezbollah, yamekuwa yakisisitiza kwamba wanataka rais ambaye hatakuja kusaliti kundi hilo baadaye," Siniora alisema.
Vita vya mwisho kati ya Lebanon na Israel, karibu miaka 20 iliyopita, vilianza pale wapiganaji wa Hezbollah walipovuka mpaka na kuwashambulia wanajeshi wa Israel.
Wawili walitekwa nyara na watatu waliuawa, na kusababisha vita vya mwezi mzima.
Katika siku zilizofuata, Siniora alitoa taarifa kwa umma kuitenganisha serikali ya Lebanon na kile kilichotokea.
Anafikiria, viongozi wa sasa wa nchi wameshindwa kufanya kile ambacho raia waliwaamini nacho, kufanya kama ilivyotokea wakati ule.
"Serikali hii haikufanya kile ambacho serikali yangu ilifanya siku hiyo. Serikali yangu ilikuwa wazi na ilidhamiria kusema kwamba hatukujua, na hatukuwa tumearifiwa juu ya mpango wa Hezbollah wa kuvuka mpaka na kuteka nyara na kuua wanajeshi wa Israel.
"Wakati huu hakujakuwa na hatua yoyote iliyofanywa na serikali ya Lebanon. Faida ya tulichofanya ni kwamba tuliweka mpaka kati ya serikali ya Lebanon na Lebanon upande mmoja, na Hezbollah kwa upande mwingine," alielezea.
Siniora hajaegemea upande wowote katika tathmini yake ya uhuru uliopotea wa Lebanon.
"Kiuhalisia, Lebanon kama taifa imetekwa nyara na Hezbollah. Na nyuma ya Hezbollah ni Iran.
"Bunduki hii iliyokuwa inashikiliwa na Hezbollah, badala ya kunyooshewa Israel, ilianza kunyooshewa ndani ya nchi na ikaanza kutumika kama njia ya Iran kuingilia Syria, Iraq na Yemen. Lebanon haiwezi kujihusisha na vita vya namna hiyo.
" Siniora pia alikuwa mmoja wa wasanifu wa azimio la UN 1701, makubaliano ambayo yalimaliza vita vya 2006.
Soma zaidi: