Wanaharakati wa haki za binadamu wametoa wito kwa mamlaka
nchini Iran kumwachilia mwanamke aliyekuwa kizuizini baada ya kuvua nguo chuo
kikuu, katika kile walichosema ni kupinga sheria za lazima za kuvaa hijab.
Video ilisambaa kwenye mitandao ya kijamii siku ya
Jumamosi ikimuonyesha mwanamke huyo akiwa amevaa nguo ya ndani huku ameketi
kwenye ngazi, kisha akatembea kwa utulivu kwenye barabara ya Tawi la Sayansi na
Utafiti la Chuo Kikuu cha Kiislamu cha Azad mjini Tehran.
Katika video ya pili, mwanamke huyo anaonekana kuvua
chupi yake. Muda mfupi baadaye, maafisa waliovalia kiraia wanaonekana
wakimshikilia kwa nguvu na kumsukuma ndani ya gari.
Chuo Kikuu cha Azad kilisema mwanamke huyo alikuwa na
"matatizo ya akili" na aamepelekwa "hospitali ya matatizo ya
akili".
Raia wengi wa Iran kwenye mitandao ya kijamii walitilia
shaka madai hayo na kueleza vitendo vyake kama sehemu ya vuguvugu linalojulikana
kama “Woman, Life, Freedom” ambalo limeshuhudia wanawake wengi wakipinga
hadharani sheria zinazowataka kufunika nywele zao na kuvaa nguo ndefu
zisizowabana.
Zaidi ya watu 500 waliripotiwa kuuawa wakati wa
maandamano ya nchi nzima yaliyozuka miaka miwili iliyopita baada ya mwanamke wa
Kikurdi, Mahsa Amini, kufariki akiwa mikononi mwa polisi baada ya kuzuiliwa kwa
kutovaa hijabu "vizuri".
Ilisema kichwa cha mwanamke huyo kiligonga mlango au
fremu ya gari la maafisa waliokuwa wamevalia kiraia wakati akizuiliwa na
kusababisha kuvuja damu na kupelekwa kusikojulikana.
Shahidi aliiambia BBC Persian kwamba mwanamke huyo
aliingia darasani mwao katika Chuo Kikuu cha Azad na kuanza kuwarekodi
wanafunzi. Wakati mhadhiri alipopinga hilo, aliondoka huku akipiga kelele.