Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Macharia Gaitho: Mwandishi maarufu Kenya asimulia utekaji nyara wake baada ya kuachiliwa

Polisi nchini Kenya wamemwachilia mwanahabari mkongwe baada ya "kumkamata kimakosa" katika kituo cha polisi na kumsukuma kwa kasi ndani ya gari binafsi.

Muhtasari

  • Aisha Masaka: Mtanzania wa kwanza kusajiliwa na timu ya ligi kuu ya wanawake ya England
  • Aliyekwama kwenye lifti kwa saa 42 nchini India alidhani angekufa
  • Mawakili wa Guinea walalamikia ukandamizaji wa jeshi
  • Macharia Gaitho: Mwandishi maarufu Kenya asimulia utekaji nyara wake baada ya kuachiliwa
  • UN, Mashirika ya kimataifa yasiitupe Sudan:MSF
  • Wafanyakazi watafutwa baada ya lori la mafuta kuzama pwani ya Oman waendelea
  • Fernandez kuadhibiwa kwa madai ya kutumia wimbo wenye kauli za kibaguzi
  • Wanafunzi walazwa hospitalini kwa kula vibanzi vyenye 'pilipili nyingi'
  • Sita waliofariki walikunywa chai yenye sumu ya sianidi
  • Israeli na Hezbollah wanakaribia kujiingiza katika vita
  • Shirika la Ford lakanusha kufadhili maandamano nchini Kenya
  • Guo:Tajiri wa China apatikana na hatia kwa kashfa ya zaidi ya $1bn Marekani
  • Mtu mmoja auawa katika maandamano ya kumtaka rais wa Kenya kuondoka madarakani
  • Usalama wa Trump uliimarishwa wiki kadhaa zilizopita kutokana na njama ya Iran ya kumuua

Moja kwa moja

Asha Juma

  1. Aisha Masaka: Mtanzania wa kwanza kusajiliwa na timu ya ligi kuu ya wanawake ya England

    Mwanasoka Aisha Masaka ameweka rekodi ya kuwa mchezaji wa kwanza mwanamke kutoka Tanzania kusajiliwa na timu ya ligi kuu ya wanawake ya England.

    Aisha amesaini kandarasi na klabu ya Brighton akitokea BK Hacken ya kutoka Sweden aliyojiunga nayo mnamo mwaka 2022 akitokea kwenye klabu ya Yanga Princess inayoshiriki ligi kuu ya wanawake nchini Tanzania

    Mwaka mmoja uliopita Aisha aliweka rekodi ya aina yake kuwa mchezaji wa kwanza mwanamke kutoka Tanzania kucheza michuano ya klabu bigwa ulaya kwa wanawake wakati timu yake ya BK Hacken iliposhiriki michuano hiyo.

    Masaka licha ya kuwa mchezaji wa kwanza mwanamke kusaiji mkataba kwenye klabu hiyo anaungana na nahodha wa timu ya Taifa ya Tanzania Mbwana Samatta ambaye aliwahi kupita kwenye klabu ya Aston Villa mnamo mwaka 2019.

  2. Aliyekwama kwenye lifti kwa saa 42 nchini India alidhani angekufa

    Mwanaume mmoja kutoka jimbo la Kerala kusini mwa India, ambaye alinasa kwenye lifti ya hospitali kwa saa 42 bila chakula wala maji, ameiambia BBC kuwa alihofia angefia humo.

    Ravindran Nair, 59, aliingia kwenye lifti ili kwenda kukutana na daktari Jumamosi mchana, kisha alikwama ndani hadi Jumatatu asubuhi, wakati msimamizi wa lifti alipomkuta.

    Sasa yuko hospitali na anatibiwa upungufu wa maji mwilini na maumivu ya mgongo.

    Watu wa familia yake hapo awali walidhani alikuwa kazini, lakini baadaye waliwasiliana na polisi na kuanza kumtafuta.

    Tukio hilo limegonga vichwa vya habari, na kusababisha serikali ya jimbo hilo kuwasimamisha kazi mafundi watatu na kuanzisha uchunguzi.

    Maafisa kutoka Chuo cha Serikali cha Matibabu, Thiruvananthapuram, na waziri wa afya wa jimbo hilo wamemwomba Bw Nair msamaha.

    Bw Nair aliiambia BBC kwamba aliponasa, alijaribu kupiga nambari ya dharura iliyowekwa kwenye lifti lakini hakujibiwa. Pia alijaribu kumpigia simu mke wake Sreelekha CP, ambaye anafanya kazi hospitalini, na "mtu mwingine yeyote ambaye aliweza kumfikiria", lakini simu hazikuunganishwa.

    "Nilianza kuogopa na kuanza kugonga milango ya lifti ili kuwashtua watu. Hapo ndipo simu yangu ilipoanguka sakafuni na kuacha kufanya kazi," asema.

    "Nilipiga kelele na kupiga mayowe kuomba msaada na nilijaribu kung'oa milango kwa mikono yangu. Sasa kulikuwa na giza ndani ya lifti, lakini cha kushukuru, kulikuwa na hewa ya kutosha ya kupumua."

    Kisha akazunguka kwenye lifti, akibonyeza kengele ya hatari tena na tena, akitumaini kwamba ingelia, lakini bila mafanikio yoyote.

    “Saa zilizidi kwenda sikujua ni mchana au usiku kwani ndani kulikuwa na giza totoro, nilipochoka nililala pembeni, ikabidi nitumie kona nyingine kujisaidia haja ndogo,” anasema.

    Unaweza kusoma;

  3. Mawakili wa Guinea walalamikia ukandamizaji wa jeshi

    Mawakili nchini Guinea wamegoma wakilalamikia ukandamizaji wa upinzani unaofanywa na utawala wa kijeshi.

    Siku ya Jumanne, chama cha wanasheria nchini kilishutumu kile kilichoeleza kama "kukamatwa kiholela" na kuwekwa kizuizini kwa siri kwa raia.

    Mawakili watasusia vikao vya mahakama hadi tarehe 31 Julai, ilisema.

    Shughuli za mahakama zinasemekana "kulemezwa" na mgomo huo, ambao unaweza kuvuruga kesi ya kihistoria kuhusu mauaji ya mwaka 2009 ambayo yanachukuliwa kuwa moja ya nyakati mbaya zaidi katika historia ya taifa hilo la Afrika Magharibi.

    Mahakama inatazamiwa kutoa uamuzi wake kwa mtawala wa zamani wa kijeshi wa nchi hiyo, Moussa Dadis Camara, kuhusu uhalifu dhidi ya binadamu kuhusiana na mauaji ya mwaka 2009 ya zaidi ya watu 150 katika uwanja wa michezo tarehe 31 Julai.

    Mamlaka imesisitiza kusikilizwa kwa kesi hiyo, lakini haijafahamika iwapo hukumu itasomwa tarehe hiyo kwa sababu ya mgomo huo.

    Mgomo huo umekuja baada ya kukamatwa tarehe 9 Julai kwa Oumar Sylla na Mamadou Bah, viongozi wa vuguvugu la wananchi ambalo limekuwa likiikosoa serikali inayoongozwa na jeshi na kutaka kurejeshwa kwa utawala wa kiraia.

    Shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International limeitaka serikali "mara moja" kuwaachilia huru.

    Unaweza kusoma;

  4. Macharia Gaitho: Mwandishi maarufu Kenya asimulia utekaji nyara wake baada ya kuachiliwa

    Polisi nchini Kenya wamemwachilia mwanahabari mkongwe baada ya "kumkamata kimakosa" katika kituo cha polisi na kumsukuma kwa kasi ndani ya gari binafsi.

    Macharia Gaitho alisema alifuatwa karibu na nyumba yake katika mji mkuu, Nairobi, na watu waliokuwa kwenye magari mawili, ambao walikataa kujitambulisha.

    Alikuwa na mwanawe, ambaye alikwenda naye hadi kituo cha polisi kilicho karibu kwa usalama wake, ambapo alisukumwa kwa nguvu ndani ya gari na kukimbizwa.

    Polisi baadaye walisema ni kisa cha "utambulisho wa makosa" na kwamba wamekuwa wakimsaka mtu mwingine ambaye wanamtuhumu kwa kudharau uchunguzi wa polisi kuhusu mshukiwa wa mauaji ya mfululizo.

    "Polisi wangependa kufafanua kwa umma kwamba asubuhi ya leo, tulimkamata mwanahabari Macharia Gaitho katika kesi ya utambulisho kimakosa, iliyokusudiwa kumkamata Francis Gaitho ambaye ni mtu tuliyekuwa tukimchunguza," walisema katika taarifa.

    Wawili hao hawana uhusiano. Video iliyosambazwa sana kwenye mitandao ya kijamii inaonesha mwanahabari huyo akilazimishwa kuingia kwenye gari jeupe na maafisa waliovalia sare na wengine waliovalia kiraia.

    Tukio hilo liliibua hasira kutoka kwa Wakenya mtandaoni, baada ya wimbi la shutuma kwamba maafisa wa usalama walikuwa wamewateka nyara watu walioonekana kuhusishwa na maandamano ya hivi karibuni dhidi ya serikali.

    Bw Gaitho aliwaambia wanahabari kuwa ndani ya gari hilo, "alikuwa katikati ya wanaume wawili waliovalia kiraia". "Nilifungwa pingu na kushambuliwa," alisema.

    Alisema watu hao walitaka kufahamu kwa nini anakataa kukamatwa.

  5. UN, Mashirika ya kimataifa yasiitupe Sudan:MSF

      • Author, Caro Robi
      • Nafasi, BBC Swahili

    Mkuu wa shirika la Kimataifa la madaktari wasio na mipaka MSF amesema mashirika ya Umoja wa Mataifa na mashirika mengine ya kimataifa ya kutoa misaada ya kibinadamu yanapaswa kurudi na kuwasaidia watu wa Sudan.

    Vita vililivyozuka mwezi Aprili mwaka jana nchini Sudan vimsababisha mzozo unaotajwa na Umoja wa Mataifa kuwa mbaya zaidi duniani na taifa hilo limetumbukia katika msukosuko mkubwa.

    Mkuu wa MSF Christos Christou amesema baada ya miezi kumi na tano ya vita vikali Sudan,takriban mtu mmoja kati ya watatu waliojeruhiwa nchini humo ni mwanamke au mtoto wa chini ya umri wa miaka kumi na kuongeza kuwa mashirika mengi yameuamua kuchukua msimamo wa kusubiri na kuona jinsi mzozo huo utakavyokwenda.

    Bwana Christou amesema MSF inazungumza na pande zote mbili zinazozona kujaribu kupata ridhaa ya kupitishwa kwa misaada ya kiutu kwa mamilioni ya wasudan wanaohitaji kwa dharura chakula,maji na makazi.

    MSF inasisitiza mzozo wa kibinadamu unaoikumba Sudan kuwa mkubwa zaidi duniani na kusema kuwa licha ya hali kuwa ngumu na inayohusisha changamoto lukuki,hatua zaidi zinahitaji kuchukuliwa kulisaidia taifa hilo na watu wake.

    Wito huo unakuja huku wajumbe wa pande zinazozozana Sudan wakifanya mazungumzo na mjumbe wa Umoja wa Mataifa mjini Geneva tangu wiki iliyopita.

    Sudan kwa sasa inakabiliwa na ukame mkali,wengi nchini humo ambao wameachwa bila ya makazi wakiripoti kuwa hawana uwezo wa kujikimu kimaisha kwani wameishiwa fedha,chakula na njia karibu zote za kujipatia riziki.

    Mashirika mengi ya kutoa misaada yamesitisha shughuli zao kwa kuhofia usalama wa wafanyakazi wake,kushambuliwa kwa vituo vyao,kuporwa kwa misaada,kunyimwa ruhusa ya kufikia maeneo yanayohitaji misaada na kutopata ufadhili wa kutosha kutoka kwa jumuiya ya kimataifa.

    Umoja wa Mataifa umezishutumu pande zote mbili zinazopigana,jeshi la Sudan na kikosi maalumu cha wanamgambo RSF kwa kuzuia kimakusudi misaada kufikishwa kwa waathiriwa,miongoni mwa visa vingine chungunzima vya ukiukaji wa haki za binadamu.

    Kwa mfano katika mji wa El Fasher,vituo vya MSF vimeshambuliwa mara tisa tangu tarehe kumi mwezi Mei na karibu kila kona ya Sudan,wahudumu wa afya wanatishwa,wagonjwa wanauawa na vituo vya afya vinalipuliwa kwa mabomu. Inaripotiwa zaidi ya asilimia sabini ya vituo vya afya nchini humo havifanyi kazi.

    Mzozo wa Sudan umesababisha mauaji ya maelfu ya watu na kuwaacha takribani watu milioni kumi na moja bila ya makazi.

    Zaidi ya nusu ya idadi, jumla ya wasudani milioni 48 hawana chakula cha kutosha na hali inabashiriwa kuwa itazidi kuzorota.

    Unaweza pia kusoma;

  6. Wafanyakazi watafutwa baada ya lori la mafuta kuzama pwani ya Oman waendelea

    Operesheni ya kuwatafuta wafanyakazi 16 waliotoweka, 13 kati yao wakiwa Wahindi, baada ya meli ya mafuta kupinduka katika pwani ya Oman inaendelea.

    Afisa mmoja wa India aliiambia BBC kwamba wizara ya mambo ya nje ilikuwa ikiratibu operesheni hiyo na mamlaka ya masuala ya bahari ya Oman.

    Maafisa wa Oman walisema Jumatatu kwamba meli ya mafuta, Prestige Falcon, ilikuwa imepinduka maili 25 kusini mashariki mwa rasi yake ya Madrakah.

    Wafanyakazi watatu kati ya 16 waliotoweka ni raia wa Sri Lanka.

    Meli hiyo iliyokuwa na bendera ya Comoro ilikuwa ikielekea katika bandari ya Aden nchini Yemen ilipopinduka.

    Maafisa kutoka Kituo cha Usalama cha Baharini cha Oman waliliambia shirika la habari la Reuters Jumanne kwamba meli hiyo ilisalia "imezama, ikiwa imepinduka"

    Wizara ya ulinzi ya Oman, ambayo inasimamia kituo hicho, haikujibu maswali ya BBC kuhusu iwapo yaliyomo ndani ya meli hiyo ya mafuta yalikuwa yamemwagika baharini.

    Meli hiyo yenye urefu wa 117.4m iliundwa mwaka wa 2007, kulingana na marinetraffic.com.

    Idadi kubwa ya wafanyakazi wa Kihindi wa baharini ulimwenguni mara nyingi huwa waathiriwa wa ajali au uharamia.

    Wafanyakazi 17 wa India wa MSC Aries, meli ya kibiashara yenye uhusiano na Israel, walikwama wakati wanajeshi wa Iran walipoikamata meli hiyo mnamo Aprili.

    Waliachiliwa baada ya mazungumzo kati ya India na Iran. Mnamo mwaka wa 2022, wafanyakazi 16 wa meli ya India walizuiliwa chini ya ulinzi wa jeshi la wanamaji la Guinea ya Ikweta kwa miezi tisa.

  7. Fernandez kuadhibiwa kwa madai ya kutumia wimbo wenye kauli za kibaguzi

    Chelsea wameanza kuchukua hatua za kinidhamu dhidi ya kiungo Enzo Fernandez baada ya kuweka video kwenye mtandao wa kijamii ambayo Shirikisho la Soka la Ufaransa lilisema ilijumuisha wimbo unaodaiwa kuwa wa "kibaguzi".

    Siku ya Jumanne FFF ilisema itawasilisha malalamiko kwa shirikisho la soka duniani Fifa, juu ya video hiyo iliyo na wimbo ulioimbwa na baadhi ya kikosi cha Argentina kuhusu wachezaji wa Ufaransa.

    Mchezaji mwenzake wa Chelsea Fernandez Wesley Fofana, alichapisha picha ya video hiyo kwenye mtandao wa Instagram, akiielezea kama "ubaguzi wa rangi usiovumilika".

    Fernandez alisema "anasikitika sana" kwa video aliyochapishwa mtandaoni wakati Argentina ikisherehekea kushinda Copa America.

    "Wimbo huo una maneno ya kukera sana na hakuna sababu kabisa ya maneno haya," alisema.

    "Ninapinga ubaguzi wa aina zote na ninaomba radhi kwa kutekwa na shangwe za sherehe zetu za Copa America.

    "Video hiyo, nyakati hizo, maneno hayo, hayaakisi imani yangu au tabia yangu."

    Taarifa ya Chelsea ilisema: "Tunatambua na kuthamini msamaha wa mchezaji wetu na tutatumia hii kama fursa ya kuelimisha.

    "Klabu imeanzisha utaratibu wa ndani wa kumpa nidhamu."

    FFF itawasiliana na Chama cha Soka cha Argentina (AFA) kuhusu video ya moja kwa moja iliyotumwa kwenye mitandao ya kijamii na Fernandez baada ya Argentina kuifunga Colombia 1-0 kwenye fainali ya Copa America Jumapili.

    Pia unaweza kusoma:

  8. Wanafunzi walazwa hospitalini kwa kula vibanzi vyenye 'pilipili nyingi'

    Wanafunzi kumi na wanne wa shule ya upili huko Tokyo walikimbizwa hospitalini baada ya kula vibanzi "vyenye pilipili nyingi", polisi walisema.

    Takriban wanafunzi 30 walikula vibanzi hivyo baada ya mmoja wao kuja nazo shuleni, vyombo vya habari vya nchini humo viliripoti.

    Muda si muda, baadhi yao walianza kulalamika kuwa na kichefuchefu na maumivu makali mdomoni, na kusababisha idara ya zimamoto na polisi kupigiwa simu.

    Wasicha 13 na mvulana mmoja ambao walipelekwa hospitali walikuwa wamepoteza fahamu.

    Kampuni inayotengeneza kitafunio hicho, Isoyama Corp, alitoa taarifa akiomba radhi kwa "tatizo lolote" kwa wateja, na kuwatakia wanafunzi afueni ya haraka.

    Shule na kampuni bado hazijasema lolote tangu BBC ilipowasiliana nazo.

    Tovuti ya kampuni hiyo inaonya yeyote ambaye angependa kula vibanzi hivyo.

    Pia, " inakataza wale walio na umri chini ya miaka 18 kutokula vibanzi hivyo ambavyo vina pilipili sana – na wale ambao wanapenda kula vyakula vya pilipili "kula kwa tahadhari". Vibanzi hivyo vina pilipili kiasi kwamba vinaweza kusababisha maumivu", ilisema.

    Pia, kampuni hiyo inashauri watu kutokula vibanzi hivyo "wakiwa peke yao" na kuongeza kuwa zinaweza kusababisha kuhara zikiliwa "kwa wingi".

  9. Sita waliofariki walikunywa chai yenye sumu ya sianidi

    Watu sita waliofariki dunia katika hoteli ya kifahari nchini Thailand walitiliwa sumu ya sianidi kwenye chai, polisi wamesema.

    Polisi wanashuku mmoja kati ya waliofariki ndiye aliyetekeleza kitendo hicho kutokana na deni kubwa alilokuwa anadaiwa.

    Watu hao walipatikana wamefariki dunia na wafanyakazi wa hoteli ya kifahari ya Hyatt Erawan katika mji mkuu wa Bangkok, Jumanne.

    Wachunguzi wanaamini hadi wakati wanapatikana, walikuwa wameshafariki saa 24 zilizopita.

    Wawili kati ya sita walikuwa wamekopeshwa "mamilioni" ya pesa ikiwa ni takriban $280,000 (£215,000) na mmoja wa waliofariki kwa ajili ya uwekezaji, mamlaka ilisema.

    Awali kulikuwa na hali ya mkanganyiko na sintofahamu baada ya ugunduzi wa kutisha wa miili hiyo, huku ripoti za ndani zikiashiria kwamba kulikuwa na ufyatuaji risasi. Polisi baadaye walitupilia mbali taarifa hizi.

    Katika mkutano na waandishi wa habari siku ya Jumatano, Naibu mkuu wa polisi wa Bangkok Jenerali Noppassin Poonsawat alisema kundi hilo lilikuwa limeingia katika hoteli hiyo kila mmoja kivyake na walipewa vyumba vitano - vinne kwenye ghorofa ya saba, na kimoja kwenye ghorofa ya tano.

    Siku ya Jumatatu, walikwenda kwenye chumba cha ghorofa ya tano.

    Wawili kati ya waathiriwa, Sherine Chong, 56, na Dang Hung Van, 55, ni raia wa Marekani.

    Wengine wanne walikuwa raia wa Vietnam Thi Nguyen Phuong, 46, mumewe Hong Pham Thanh, 49, Thi Nguyen Phuong Lan, 47, na Dinh Tran Phu, 37.

    Pia unaweza kusoma:

  10. Israeli na Hezbollah wanakaribia kujiingiza katika vita

    Wakati vita huko Gaza vikiendelea, kuna hofu inayoongezeka huenda vikazuka vita vingine vya Mashariki ya Kati - na matokeo mabaya kwa eneo hilo, na kwingineko.

    Israel na kundi la Lebanon Hezbollah (linaloungwa mkono na Iran) wamekuwa wakifyatuliana risasi na makombora katika mpaka wao wa pamoja kwa muda wa miezi tisa iliyopita.

    Iwapo mzozo huu utazidi kuwa vita vya pande zote, unaweza kupunguza uharibifu ambao umeonekana Gaza, kuwaingiza vitani wanamgambo wanaoungwa mkono na Iran nchini Iraq, na Yemen, kueneza mzozo Mashariki ya Kati na kuihusisha Marekani. Iran yenyewe inaweza kuingilia moja kwa moja.

    Umoja wa Mataifa umeonya kuhusu "janga lisiloweza kufirika".

  11. Shirika la Ford lakanusha kufadhili maandamano nchini Kenya

    Shirika la Ford Foundation lenye makao yake nchini Marekani limekanusha madai ya Rais William Ruto kwamba linafadhili maandamano ya kupinga serikali.

    Katika taarifa walioitoa kwenye mtandao wao, Ford Foundation imesema, "Ingawa tunatambua haki ya Wakenya kutetea kwa amani nchi yenye haki na usawa, tunakanusha vitendo au matamshi yoyote ambayo yana chuki au kuunga mkono unyanyasaji dhidi ya taasisi yoyote, mtu binafsi au jamii yoyote. Hatukufadhili maandamano ya hivi majuzi dhidi ya mswada wa fedha na tuna sera isiyopendelea upande wowote kwa utoaji wetu wote wa ruzuku."

    Haya yanajiri baada ya Rais William Ruto hususan kulitaja shirika hilo na kulitaka kuambia Wakenya ukweli juu ya nani anayefadhili maandamano ya Kenya ya kupinga serikali.

    Bw. Ruto aliongeza kuwa wote wanaohusika watakabiliwa na mkono wa sheria.

    Shirika la Ford ni la kibinafsi lililoanzishwa mwaka 1963 na Edsel Ford, mtoto wa mwanzilishi wa Kampuni ya Ford Motor Henry Ford.

    Shirika hilo linalenga kuendeleza haki na maadili ya demokrasia na linaendesha shughuli zake duniani kote.

    Soma zaidi:

  12. Guo:Tajiri wa China apatikana na hatia kwa kashfa ya zaidi ya $1bn Marekani

    Mfanyabiashara wa China aliyekimbia nchi yake na kwenda uhamishoni Guo Wengui amepatikana na hatia na mahakama ya Marekani kwa kosa la kuwalaghai wafuasi wake mtandaoni katika kashfa ya mabilioni ya dola.

    Alipatikana na hatia katika makosa tisa kati ya 12 aliyokabiliwa nayo, ikiwa ni pamoja na ulaghai na utakatishaji fedha.

    Hukumu ya Guo itatolewa tarehe 19 Novemba, ambapo anaweza kufungwa kwa miongo kadhaa. Amekuwa gerezani tangu kukamatwa kwake Machi 2023.

    Yeye ni mkosoaji wa chama cha Kikomunisti cha China na alikuwa mshirika wa Stephen Bannon, mwanamkakati mkuu wa zamani wa Ikulu ya White House chini ya rais wa zamani Donald Trump.

    Guo ana majina mengi ikiwa ni pamoja na Miles Guo, Miles Kwok na " Brother Seven". Alitajwa kama Ho Wan Kwok alipofunguliwa mashtaka mwaka 2023.

    Waendesha mashtaka walisema Guo alichangisha zaidi ya $1bn (£770bn) kutoka kwa wafuasi wake mtandaoni, ambao walijiunga naye katika miradi ya uwekezaji nasarafu za kidijitali (cryptocurrency) kati ya 2018 na 2023.

    Pesa alizochangisha zilitumika kufadhili maisha yake ya ambayo yalijumuisha jumba la futi za mraba 50,000, Lamborghini ya $1m na boti ya $37m, walisema.

    "Maelfu ya wafuasi wa Guo mtandaoni walidhulumiwa ili Guo aweze kuishi maisha ya kifahari," Mwanasheria wa Marekani huko Manhattan, Damian Williams, alisema baada ya hukumu hiyo.

    Soma zaidi:

  13. Mtu mmoja auawa katika maandamano ya kumtaka rais wa Kenya kuondoka madarakani

    Waandamanaji wanaoipinga serikali nchini Kenya walirejea barabarani wakiongeza madai ya kumtaka Rais William Ruto ajiuzulu licha ya mabadiliko yake ya hivi majuzi.

    Mwanamume mmoja ameuawa kwa kupigwa risasi wakati wa makabiliano kati ya waandamanaji na vikosi vya usalama viungani mwa mji mkuu, mwandishi wa BBC katika eneo hilo anasema.

    Katikati ya jiji la Nairobi, maduka yalisalia kufungwa huku polisi wakifyatua gesi ya kutoa machozi kuwatawanya mamia ya waandamanaji.

    Maandamano hayo yalianza mwezi uliopita kupinga mswada wa ushuru ambao haukupendwa na watu wengi, na kutoka wakati huo umeondolewa na rais.

    Lakini yamekuwa yakiendelea kutokana na hasira zaidi juu ya utawala mbaya, rushwa na uwajibikaji wa polisi kutokana na vifo vya makumi ya waandamanaji katika maandamano ya hivi karibuni.

    Wiki iliyopita, Rais Ruto alitoa wito wa "mazungumzo" huku akifuta baraza lake lote la mawaziri na mkuu wa jeshi la polisi kujiuzulu.

    Harakati za maandamano hayo kwa kiasi kikubwa zinaratibiwa mtandaoni na vijana wa Kenya, ambao wengi wao wamekataa mazungumzo na wanamtaka Bw Ruto "aondoke" madarakani.

    Umati wa watu ulibeba mwili wa muandamanaji aliyeuawa Jumanne huko Kitengela, kusini mwa Nairobi, hadi kituo cha polisi kilicho karibu. Jeshi la polisi halijazungumzia kifo cha mtu huyo.

    Waandamanaji hao waliimba "Ruto lazima aende", waliwasha moto barabarani na kurusha mawe walipokuwa wakipambana na polisi, mwandishi wa BBC katika eneo la tukio anasema.

    Ghasia pia zilishuhudiwa katika maeneo mengine ya nchi, yakiwemo Mombasa, Kisumu, Nakuru na Nyeri.

    Makumi ya watu wameuawa hadi sasa tangu kuanza kwa maandamano hayo, huku shirika linalofadhiliwa na serikali likisema idadi ya vifo vilivyotokea kutokana na maandamano hayo si chini ya watu 50 huku wengine 413 wakijeruhiwa.

    Mapema Jumanne, kaimu mkuu wa polisi alisema kulikuwa na "intelijensia ya kuaminika" kwamba "makundi fulani ya wahalifu waliopangwa" yalikuwa yamepanga "kupenya, kuvuruga na kuhatarisha" maandamano hayo.

    Soma zaidi:

  14. Usalama wa Trump uliimarishwa wiki kadhaa zilizopita kutokana na njama ya Iran ya kumuua

    Ulinzi kwa Donald Trump uliimarishwa wiki kadhaa zilizopita baada ya mamlaka ya Marekani kujua kuhusu njama ya Iran ya kumuua, kulingana na maafisa wa usalama wa taifa.

    Maafisa wanasema hakuna uhusiano unaojulikana kati ya madai ya njama ya Iran na jaribio la kumuua rais huyo wa zamani siku ya Jumamosi huko Pennsylvania.

    Hata hivyo, ufichuzi kwamba usalama umeimarishwa unazua maswali zaidi kuhusu jinsi Thomas Matthew Crooks, 20, alivyoweza kupanda jengo na kukaribia vya kutosha kumfyatulia risasi Trump.

    Idara ya Huduma ya Siri ya Marekani na kampeni ya Trump ziliarifiwa kuhusu tishio la Iran, na usalama ukaimarishwa kutokana na hilo, kulingana na afisa wa usalama wa taifa wa Marekani.

    Vyanzo vya kijasusi viliiambia CBS, mshirika wa habari wa BBC wa Marekani, kwamba Huduma ya Siri iliimarisha usalama mwezi Juni ili kukabiliana na tishio la Iran. Hii ilijumuisha afisa wa ziada wa kukabiliana na mashambulizi na mpiga risasi kwa kuvamia, ndege zisizo na rubani na mbwa wa roboti.

    CBS iliripoti kwamba maelezo ya uwezekano wa operesheni ya Iran yalipatikana kupitia "intelijensia ya chanzo cha binadamu", na yalipatikana huku kukiwa na ongezeko kubwa la mazungumzo ya Iran kuhusu mashambulizi dhidi ya Trump.

    Trump na maafisa akiwemo waziri wake wa zamani wa mambo ya nje, Mike Pompeo, wamekabiliwa na vitisho kutoka Tehran tangu kuamuru kuuawa kupitia ndege isiyo na rubani kwa Qassim Soleimani, kamanda wa kikosi cha Quds cha Iran, nchini Iraq mwaka 2020.

    Ujumbe wa Iran katika Umoja wa Mataifa uliita ripoti hiyo "isiyo na uthibitisho na yenye nia mbaya", na kuongeza kuwa Trump ni "mhalifu ambaye lazima ashtakiwe na kuadhibiwa katika mahakama ya sheria".

    Anthony Guglielmi, msemaji wa Huduma ya Siri ya Marekani, alisema shirika hilo na mengine "yamekuwa yakipokea taarifa mpya za vitisho na kuchukua hatua kama inavyohitajika".

    "Hatuwezi kutoa maoni juu ya vitisho vyovyote, zaidi ya kusema kwamba Huduma ya Siri inachukukulia vitisho kwa uzito na kujibu ipasavyo."

    Kampeni ya Trump ilisema haitoi maoni yoyote juu ya maswala ya usalama na ilielekeza maswali ya BBC kwa Huduma ya Siri.

    Soma zaidi:

  15. Hujambo na karibu katika matangazo yetu mubashara ikiwa ni tarehe 17/7/2024