Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Maandamano ya kupinga utawala wa rais Ruto yafanyika Kenya

Polisi waliokuwa wakipiga doria katikati ya jiji la Nairobi nchini Kenya wametumia vitoa machozi kuwatawanya vijana waliokuwa wamekusanyika kwa maandamano dhidi ya serikali.

Muhtasari

  • Maandamano ya kupinga utawala wa rais Ruto yaendelea Kenya
  • Kylian Mbappe atambulishwa rasmi Real Madrid
  • Mauaji ya Kware Kenya: Mshukiwa adai aliteswa ili kukiri mauaji
  • Polisi wengine 200 wa Kenya waelekea Haiti
  • Nani kumrithi Southgate? - Makocha wanaozungumziwa sana
  • Wapakistani wanne wauawa kwa kupigwa risasi karibu na msikiti huko Oman, Pakistan yasema
  • Southgate ajiuzulu baada ya England kushindwa katika michuano ya Euro 2024
  • 'Nyangumi adimu zaidi duniani' apatikana katika ufuo wa New Zealand
  • Rais Kagame ashinda kwa kishindo-Matokeo ya awali ya uchaguzi Rwanda
  • Wanajeshi wanne wa India wauawa huku ghasia za Kashmir zikiongezeka
  • Mauzo ya fulana zaTrump baada ya kupigwa risasi yasitishwa China
  • Kaspersky:Kampuni ya Urusi yajiondoa Marekani
  • Trump amchagua JD Vance kuwa mgombea mwenza wake
  • Pango lililogunduliwa mwezini linaweza kuwa makao ya wanadamu
  • Biden atetea kumwita Trump tishio kwa demokrasia
  • Shambulizi la Israel katika shule katikati mwa Gaza lasababisha vifo vya watu 22
  • Mtu tajiri zaidi barani Afrika asema hana nyumba nje ya Nigeria
  • Bunge nchini Gambia lapinga mswada wa kuruhusu ukeketaji
  • Trump aliyefungwa bandeji akaribishwa kwa nderemo katika kongamano la chama cha Republican

Moja kwa moja

Asha Juma na Lizzy Masinga

  1. Maandamano ya kupinga utawala wa rais Ruto yaendelea Kenya

    Polisi katika waliokuwa wakipiga doria katikati ya jiji la Nairobi nchini Kenya wametumia vitoa machozi kuwatawanya vijana waliokuwa wamekusanyika kwa maandamano dhidi ya serikali.

    Kulikuwa na maafisa wengi wa polisi katikati ya jiji la Nairobi, ambalo limekuwa kitovu cha hatua ya awali ya maandamano ya vijana.

    Jumanne ilikuwa siku nyingine ya maandamano makali huku shughuli za biashara zikisimama katikati ya mji huo pamoja na miji mingine kote nchini.

    Wakati huohuo mtu mmoja amedaiwa kuuawa kwa kupigwa risasi eneo la Kitengela, Kaunti ya Kajiado wakati wa maandamano dhidi ya serikali huku wito wa kumtaka Rais William Ruto ajiuzulu ukiongezeka.

    Kilichoanza kama maandamano ya amani katika mji wa Kitengela yaligeuka kuwa ghasia baada ya maafisa wa polisi kuwarushia vitoa machozi waandamanaji hao.

    Hii ilisababisha makabiliano makali kati ya waandamanaji na maafisa wa kupambana na ghasia ambao walijibu kwa kuwarushia waandamanaji maji ili kutawanya umati.

  2. Kylian Mbappe atambulishwa rasmi Real Madrid

    Nyota wa Ufaransa Kylian Mbappe ametambulishwa rasmi kama mchezaji wa Real Madrid Jumanne, na kuwaambia mashabiki 80,000 "ndoto yangu imetimia".

    Mshambulizi huyo, ambaye alikuwa amekamilisha vipimo vyake vya afya mapema Jumanne asubuhi, alisaini mkataba wa miaka mitano na kukabidhiwa jezi nambari 9 na rais wa klabu Florentino Perez.

    "Wow," Mbappe alisema kwa Kihispania katika Uwanja wa Santiago Bernabeu uliojaa.

    "Kwa miaka mingi nimekuwa na ndoto ya kuichezea Real Madrid na leo ndoto yangu imetimia," alisema mchezaji huyo wa zamani wa Paris Saint-Germain mwenye umri wa miaka 25.

    "Mimi ni mvulana mwenye furaha. Nitatoa maisha yangu kwa ajili ya klabu hii," alisema Mbappe.

    Akiwa ameambatana na wazazi wake waliokuwa wakitazama kutoka kwa umati wa watu na gwiji wa zamani wa Ufaransa wa klabu hiyo, Zinedine Zidane, aliyehudhuria, Mbappe alijawa na hisia huku umati wa watu wakiimba jina lake, na wakati fulani akabusu jezi ya mabingwa hao watetezi wa Uhispania na Ulaya.

    Mbappe ni "mchezaji wa kipekee ambaye anakuja kutusaidia kuendelea kushinda, mchezaji ambaye leo anatimiza ndoto ya maisha yake," alisema Perez. "Karibu nyumbani kwako."

  3. Habari za hivi punde, Mauaji ya Kware Kenya: Mshukiwa adai aliteswa ili kukiri mauaji

    Collins Jumaisi Khalusha, anayetuhumiwa kuwaua takriban wanawake 42 na kuikatakata miili yao kabla ya kuwatupa kwenye machimbo ya mawe eneo la Kware, mjini Nairobi, amedai ukatili wa polisi kufuatia kukamatwa kwake siku ya Jumatatu.

    Khalusha, kupitia kwa wakili wake John Maina Ndegwa, amedai kuteswa hadi kukiri kuwa aliwaua wanawake hao, huku akiiomba mahakama kumpatia huduma ya matibabu.

    "Mteja wangu, akiwa amekaa pale, anahitaji matibabu ya haraka ... kwa sababu katika kipindi alichowekwa kizuizini, alinyanyaswa, kuteswa na kulazimishwa kukiri kwamba aliwaua watu 42 jambo ambalo ni la kuchekesha. ” alidai Ndegwa mbele ya Mahakama ya Sheria ya Makadara.

    "Mteja wangu amefanyiwa ukatili wa kutisha ili aweze kukiri masuala ambayo si ya kawaida kwake. Ninaomba kwamba mahakama ielekeze uangalizi wa haraka wa matibabu hata wanapofanya uchunguzi wao''.

    Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) hata hivyo ilipuuzilia mbali madai hayo ya unyanyasaji, ikibaini kuwa ni afisa mmoja tu wa polisi aliyepewa mshukiwa kurekodi taarifa yake.

    DCI ilitaka Khalusha azuiliwe kwa siku 30 hadi kukamilika kwa uchunguzi wa mauaji hayo, akisema iwapo ataachiliwa kuna uwezekano wa kuendelea na shughuli za uhalifu.

    Shirika la upelelezi pia liliiambia mahakama kwamba wanahitaji muda zaidi wa kuwatafuta mashahidi na familia za wahasiriwa ambao wametawanyika kote nchini, na kwamba watahitaji pia kuchukua sampuli za DNA, utambulisho, na pia kumfanyia mshukiwa uchunguzi wa kiakili.

    Upande wa mashtaka hata hivyo ulipinga hilo, badala yake uliitaka mahakama kuwapa polisi siku 14 pekee kumzuilia mshukiwa huku uchunguzi ukiendelea.

    Hakimu Mkuu Irene Gichobi hata hivyo aliruhusu DCI kumzuilia mshukiwa katika kituo chochote cha polisi kwa siku 30 ilizoomba ili kukamilisha uchunguzi.

  4. Polisi wengine 200 wa Kenya waelekea Haiti

    Maafisa wengine 200 wa polisi wa Kenya wameondoka kuelekea Haiti chini ya ujumbe unaoungwa mkono na Umoja wa Mataifa kujaribu kumaliza ghasia za magenge katika taifa hilo lenye mgogoro la Caribbean, maafisa wakuu wa polisi walisema Jumanne.

    Kutumwa huko kumekuja baada ya taifa hilo la Afrika Mashariki kutuma maafisa 400 katika mji mkuu wa Haiti ulioharibiwa na ghasia Port-au-Prince mwezi Juni, ikiwa ni sehemu ya ombi lenye utata la kutuma baadhi ya polisi 1,000 kusaidia kuleta utulivu nchini humo.

    Ahadi hiyo, iliyotolewa na Rais William Ruto, ambaye anajaribu kutuliza maandamano ya kuipinga serikali nyumbani, imekumbwa na changamoto za kisheria nchini Kenya.

    "Tuna maafisa wa polisi 200 ambao waliondoka jana usiku, wanapaswa kutua Haiti leo asubuhi," afisa mmoja mkuu wa polisi aliambia AFP siku ya Jumanne.

    "Wanaungana na wenzao ambao tayari wako huko." Chanzo kingine cha juu cha polisi kiliithibitishia AFP kwamba maafisa hao waliondoka Jumatatu usiku, wakisafiri kwa ndege ya kukodi, na kuongeza: "Wengine zaidi wataondoka hivi karibuni hadi tupate 1,000 wote.''

    Taifa hilo la Afrika Mashariki linaongoza kikosi kinachotarajiwa kuwa na jumla ya wanajeshi 2,500.

    Nchi nyingine, hasa za Afrika na Karibiani, pia zinachangia misheni hiyo, ambayo imebarikiwa lakini haidhibitiwi na Umoja wa Mataifa.

    Mnamo Julai 1, Huduma ya Kitaifa ya Polisi ya Kenya ilitoa taarifa kukanusha uvumi kwamba maafisa saba waliuawa nchini Haiti.

    Vikosi vilivyotumwa vilikuwa "vimepokelewa kwa uchangamfu", na "vyote vilikuwa salama na tayari kutekeleza majukumu yao wazi na mahususi," ilisema.

    Walikuwa "wakifanya kazi kwa karibu na mwenyeji wao, Polisi wa Kitaifa wa Haiti, na hadi sasa wamechukua ramani ya kimkakati ya maeneo ambayo yana uwezekano wa kufanyia kazi na kufanya doria kadhaa za pamoja ndani ya Port-au-Prince".

    Unaweza kusoma;

  5. Nani kumrithi Southgate? - Makocha wanaozungumziwa sana

    Thomas Tuchel: Kocha ambaye anatafuta kazi msimu huu wa joto. Gwiji wa Chelsea kwa kuisaidia klabu hiyo kushinda Champions League mwaka wa 2021, aliacha kazi yake huko Bayern Munich mwishoni mwa msimu uliopita, licha ya mazungumzo ya kumshawishi abaki.

    Tuchel, ambaye pia amewahi kunoa klabu za Paris St-Germain na Borussia Dortmund, angefurahi kurejea katika soka ya Uingereza na anaaminika kuwa tayari kwa mazungumzo na FA kuhusu kuwa mrithi wa Southgate.

    Inasemekana alikaribia kuchukua nafasi ya Erik ten Hag huko Manchester United.

    Mauricio Pochettino: Meneja mwingine wa hadhi ya juu, maarufu, wa kigeni hana kazi msimu huu wa kiangazi.

    Kocha huyo wa zamani wa Tottenham, PSG na Chelsea alihusishwa sana na Manchester United, kabla ya Erik ten Hag kuongezwa mkataba na angefurahi kurejea kazini Uingereza.

    Ana nia ya kuwa mrithi wa Southgate na mapenzi yake kwa soka England yanamfanya kuwa mshindani mkubwa.

    Jurgen Klopp:Meneja mwingine mwenye jina kubwa ambaye hana kazi.

    Iwapo FA ingekuwa na nia ya kuteka jina kutoka nje ya nchi, bila shaka Klopp angekuwa kwenye orodha yake ya wagombea.

    Meneja huyo wa zamani wa Liverpool huenda akapatikana kwa sasa, baada ya kujiuzulu Anfield na kutaka mapumziko.

    Lakini FA itakuwa tayari kusubiri. Klopp anaweza kuingia kwenye hesabu.

    Akiwa na miaka 57 tayari anapigiwa upatu kuwania nafasi hiyo iliyo wazi nchini Marekani na kama anayeweza kuwa mrithi wa Julian Nagelsmann, iwapo ataondoka Ujerumani.

    Pep Guardiola: Kocha huyo wa Manchester City kwa muda mrefu amekuwa akitajwa kuwa meneja wa kimataifa wa siku zijazo na jukumu lake na Uingereza bila shaka litawasisimua mashabiki wengi wa England.

    Baada ya kushinda kila kitu na katika ngazi ya klabu na Barcelona, ​​Bayern Munich na Manchester City, changamoto mpya msimu ujao inaweza kuonekana ya kuvutia sana.

    Guardiola yuko chini ya mkataba na City hadi msimu wa joto wa 2025.

  6. Wapakistani wanne wauawa kwa kupigwa risasi karibu na msikiti huko Oman, Pakistan yasema

    Pakistan imesema raia wake wanne wameuawa katika shambulio la risasi katika msikiti wa Shia katika mji mkuu wa Oman, Muscat.

    Taarifa ya wizara ya mambo ya nje ilisema raia wengine 30 wa Pakistani pia ni miongoni mwa waliojeruhiwa katika kile ilicholaani kama "shambulio baya la kigaidi" kwenye Msikiti wa Imam Ali, na kuongeza kuwa "washambuliaji" "wamedhibitiwa".

    Video ilionesha umati wa watu wakikimbilia kujificha ndani ya ua wa msikiti huku milio ya risasi ikisikika.

    Walikuwa wamekusanyika pale katika mkesha wa siku tukufu ya Shia ya Ashura.

    Polisi wa Kifalme wa Oman walitoa taarifa fupi usiku kucha wakisema kwamba maafisa walijibu tukio la ufyatuaji risasi karibu na msikiti katika eneo la al-Wadi al-Kabir ambapo watu wanne waliuawa.

    Haikutoa taarifa yoyote kuhusu kutambuliwa kwa washambuliaji na waathiriwa, pamoja na nia ya kutekelezwa kwa tukio hilo.

    "Hatua zote muhimu za usalama na taratibu zimewekwa ili kukabiliana na hali hiyo. Uchunguzi na ukusanyaji wa ushahidi unaendelea," iliongeza.

    Balozi wa Pakistan nchini Oman, Imran Ali, alisema kwenye video kwamba amewatembelea baadhi ya waliojeruhiwa katika hospitali tatu za mitaa na kuelezea hali zao kuwa "salama kiasi".

    Pia aliwashauri wakazi wa Pakistani wa Oman kuepuka al-Wadi al-Kabir na kushirikiana na mamlaka za mitaa. Gazeti la The National, lenye makao yake makuu mjini Abu Dhabi, lilimnukuu Ali akisema kuwa takribani wafanyakazi 50 kutoka nje ya Pakistani walijeruhiwa katika shambulio hilo, huku 20 wakitibiwa majeraha ya risasi.

    Waumini kadhaa katika msikiti huo, wakiwemo wanawake na watoto pia walichukuliwa mateka na watu wenye silaha na baadaye kuachiliwa kwa msaada wa polisi waliokuwa na silaha.

  7. Southgate ajiuzulu baada ya England kushindwa katika michuano ya Euro 2024

    Kocha wa timu ya taifa ya England Gareth Southgate amejiuzulu siku mbili baada ya kushindwa na Hispania kwenye fainali ya Euro 2024.

    England ilifungwa 2-1 mjini Berlin Jumapili, kikiwa ni kipigo chao cha pili mfululizo katika fainali ya Euro, baada ya kuchapwa kwa penalti na Italia kwenye Uwanja wa Wembley miaka mitatu iliyopita.

    Kocha huyo mwenye miaka 53 aliiongoza nchi yake kwenye michezo 102 ndani ya miaka minane ya uongozi.

    Mkataba wake ulikuwa unamalizika baadaye mwaka huu. "Kama Muingereza wa kujivunia, imekuwa heshima katika maisha yangu kuichezea Uingereza na kuinoa England," alisema Southgate.

    "Imekuwa na maana kwa kila kitu kwangu, na nimetoa yangu yote. "Lakini ni wakati wa mabadiliko, na sura mpya."

    Mtendaji mkuu wa Chama cha Soka Mark Bullingham amesema mchakato wa kumteua mrithi wa Southgate umeanza na "tunalenga kuwa meneja wetu mpya athibitishwe haraka iwezekanavyo".

    Aliongeza FA "kuwa na suluhu la muda iwapo litahitajika" na hatatoa maoni zaidi kuhusu mchakato huo hadi bosi mpya atakapoteuliwa.

    Mechi inayofuata ya England ni dhidi ya Jamhuri ya Ireland katika Ligi ya Mataifa ya Ulaya mnamo Septemba 7.

  8. 'Nyangumi adimu zaidi duniani' apatikana katika ufuo wa New Zealand

    Nyangumi ambaye alipatikana akiwa amekufa kwenye ufuo wa New Zealand mapema mwezi huu ametambuliwa na wanasayansi kuwa nyangumi mwenye meno mithili ya jembe, spishi ambayo haijawahi kuonekana ikiwa hai.

    Utambulisho wa kiumbe huyo mwenye mdomo yenye urefu wa mita tano ulibainishwa kutokana na mifumo yake ya rangi na umbo la fuvu la kichwa, mdomo na meno yake.

    Mabaki yake yamewekwa kwenye hifadhi huku uchunguzi wa vinasaba ukifanyika, huku wataalamu wakisema huenda wakatumia wiki kadhaa kabla ya utambulisho wa mwisho kuthibitishwa.

    Kwa sababu vielelezo vichache sana vimepatikana na hakujawa na masuala yanayojulikana kuhusu nyangumi mwenye meno ya jembe.

    Watafiti wanasema ugunduzi wa mzoga huo unaweza kuwasaidia kupata taarifa mpya muhimu kuhusu spishi hiyo.

    Maafisa wa eneo hilo waliarifiwa kwamba nyangumi huyo alisombwa na maji tarehe 4 Julai kwenye mlango wa mto Taiari, katika mkoa wa Otago kwenye Kisiwa cha Kusini cha New Zealand.

    Afisa wa Idara ya Uhifadhi (DOC) Gabe Davies alisema katika taarifa yake kwamba nyangumi wenye meno ya jembe ni mojawapo ya viumbe wakubwa wa mamalia wanaojulikana sana, na ni sampuli sita pekee zilizowahi kurekodiwa duniani kote.

    Idara hiyo ilisema kwamba kwa sababu sampuli hiyo ilikuwa imekufa hivi karibuni tu inaweza kuwa nyangumi wa kwanza wa spishi hiyo.

  9. Rais Kagame ashinda kwa kishindo-Matokeo ya awali ya uchaguzi Rwanda

    Rais wa Rwanda Paul Kagame yuko mbioni kuongeza utawala wake wa miaka 24 kwa miaka mingine mitano katika ushindi wa kishindo, huku kura nyingi zikihesabiwa kutoka katika uchaguzi wa Jumatatu.

    Ana 99.15% ya kura kufikia sasa, na takribani 79% ya kura zimehesabiwa, matokeo ya awali yaliyotangazwa na tume ya uchaguzi yanaonesha.

    Mzee huyo mwenye umri wa miaka 66 tena hakukabiliwa na upinzani wowote mkubwa, huku viongozi hao wakipigwa marufuku.

    Wapinzani wake wawili waligawana chini ya 1% ya kura.

    Bw Kagame aliwashukuru Wanyarwanda kwa imani yao katika hotuba katika makao makuu ya chama chake cha Rwandan Patriotic Front (RPF).

    "Hizi si takwimu tu, hata ikiwa ni 100%, hizi sio nambari tu. Wao wanaonesha kuamini, na hilo ndilo lililo muhimu zaidi,” Bw Kagame alisema.

    Wapinzani wake, mwanamazingira Frank Habineza na mwandishi wa habari na mwandishi Philippe Mpayimana, wana 0.53% na 0.32% mtawalia.

    Matokeo kamili yanatarajiwa kufikia tarehe 20 Julai na ya mwisho ifikapo tarehe 27 Julai.

    Unaweza kusoma;

  10. Wanajeshi wanne wa India wauawa huku ghasia za Kashmir zikiongezeka

    Takriban wanajeshi wanne wameuawa katika mapigano ya risasi na watu wanaoshukiwa kuwa wanamgambo huko Kashmir inayotawaliwa na India - ikiwa ni tukio la hivi punde zaidi katika mashambulizi ya hivi karibuni ya waasi wenye silaha katika eneo hilo linalozozaniwa.

    Vikosi vya usalama vilishutumiwa usiku wa kuamkia Jumatatu walipokuwa wakifanya msako katika misitu ya wilaya ya Doda huko Jammu.

    Wiki iliyopita wanajeshi watano waliuawa wakati gari lao lilipovamiwa katika sehemu nyingine ya eneo hilo ambayo inazozaniwa na India na Pakistan.

    Uasi wa kutumia silaha dhidi ya utawala wa India umegharimu maisha ya maelfu ya watu huko Kashmir tangu 1989, lakini ghasia zimepungua katika miaka ya hivi karibuni.

    Hata hivyo, eneo lenye amani la Jammu limeshuhudia kuongezeka kwa umwagaji damu katika miezi ya hivi karibuni. Takriban mashambulizi manane yameripotiwa katika eneo hilo tangu mwezi Juni.

    Mwezi uliopita, watu tisa walifariki na 33 kujeruhiwa baada ya watu wanaoshukiwa kuwa wanamgambo kurusha risasi kwenye basi lililokuwa limebeba mahujaji wa Kihindu katika eneo hilo.

    Mnamo tarehe 8 Julai, wanajeshi watano waliuawa katika shambulio la kuvizia katika wilaya ya Kathua.

    Wanajeshi watano walijeruhiwa vibaya katika tukio la kurushiana risasi na wanamgambo, jeshi lilisema kwenye mtandao X. Wanne kati yao walifariki dunia kwa majeraha baadaye.

    Soma zaidi:

  11. Mauzo ya fulana za Trump baada ya kupigwa risasi yasitishwa China

    Majukwaa ya kibiashara ya mtandaoni ya China yameondoa fulana zenye picha ya Donald Trump akionyesha ngumi hewani muda mfupi baada ya kupigwa risasi.

    Fulana hizo ambazo zilianza kuuzwa ndani ya saa chache baada ya Trump kupigwa risasi, zilipatikana kwenye tovuti maarufu za biashara ya mtandaoni kama vile Taobao na JD.com.

    Haijulikani kwa nini zimeondolewa, lakini mtandao wa Wachina unadhibitiwa sana, huku maudhui yanayochukuliwa kuwa "nyeti" yakiondolewa mara kwa mara.

    Jaribio la mauaji katika mkutano wa hadhara wa Pennsylvania Jumamosi iliyopita lilizua mjadala mkubwa mtandaoni, hashtagi zinazohusiana na tukio hilo zikisambaa kwenye jukwaa la X-like Weibo.

    Wauzaji wa reja reja wa Kichina waliingia kwenye mazuo, huku kundi la kwanza la fulana hiyo likichapishwa na kuuzwa mtandaoni chini ya saa tatu baada ya kupigwa risasi.

    Picha iliyopo Taobao, mojawapo ya tovuti kubwa zaidi za biashara ya mtandaoni nchini China, inaonyesha fulana hiyo inayouzwa kwa yuan 39 ($9; £7).

    Nchini China, Trump amekuwa angalizo mtandaoni kwa miaka - kwa sababu nzuri na mbaya.

    Pia unaweza kutazama:

  12. Kaspersky:Kampuni ya Urusi yajiondoa Marekani

    Kampuni kubwa ya Urusi yenye kutengeneza programu ya kukabiliana na virusi vya kompyuta Kaspersky Labs imeambia BBC kwamba inaondoka Marekani baada ya utawala wa Biden kupiga marufuku uuzaji na usambazaji wa programu za kampuni hiyo.

    Kaspersky ilisema imefanya "uamuzi wa kusikitisha na mgumu" kuondoka "kwani fursa za kibiashara nchini humo hazipo tena".

    Hii inakuja baada ya Waziri wa Biashara Gina Raimondo kusema mwezi uliopita kwamba ushawishi wa Urusi juu ya kampuni hiyo uliweka hatari kubwa kwa miundombinu na huduma za Marekani.

    Kampuni ya Kaspersky, ambayo ilikuwa ikifanya kazi nchini Marekani kwa miongo miwili, imekanusha madai hayo.

    "Kuanzia Julai 20, 2024, Kaspersky itatamatisha shughuli zake taratibu nchini Marekani na kuondoa nyadhifa za msingi za Marekani," kampuni hiyo ilisema katika taarifa.

    Tovuti ya kampuni hiyo ya Marekani tayari imeacha kuuza programu hiyo na nyinginezo, na inaonyesha ujumbe unaosomeka "hakuna manunuzi kwa wateja wa Marekani".

    Tangazo hilo linawadia baada ya mauzo na usambazaji wa bidhaa za Kaspersky kupigwa marufuku nchini Marekani.

    Bi Raimondo alisema Marekani ililazimika kuchukua hatua kutokana na "uwezo na... nia ya Urusi kukusanya na kumiliki taarifa za kibinafsi za Wamarekani".

    "Kaspersky kwa ujumla haitaweza tena, miongoni mwa shughuli zingine, kuuza programu zake nchini Marekani au kutoa masasisho kwa programu ambayo tayari inatumika," Wizara ya Biashara ilisema.

    Pia unaweza kusoma:

  13. Trump amchagua JD Vance kama mgombea mwenza wake

    Donald Trump amemteua Seneta wa Ohio JD Vance kuwa makamu wake wa rais.

    Wajumbe wa Kongamano la Kitaifa la chama cha Republican walimchagua rasmi Bw Vance, 39, Jumatatu baada ya Trump kutangaza kwenye mtandao wake wa kijamii kuwa amemchagua baada ya "kutafakari na kufikiria kwa muda mrefu".

    Bw Vance ni mjasiriamali aliyeelimishwa na mwandishi wa riwaya ya kumbukumbu ya maisha yake ya Hillbilly Elegy iliyokuwa na mauzo mazuri ambayo iligeuzwa kuwa filamu.

    Hapo awali alimkosoa mgombea mwenza wake mpya, akipendekeza kwa faragha kwamba Trump anaweza kuwa "Hitler wa Marekani", lakini amekuwa mfuasi mkubwa.

    Mnamo mwaka wa 2016, wakati Donald Trump alipomchagua Gavana wa Indiana Mike Pence kama mgombea mwenza wake, ilitazamwa na wengi kama juhudi ya kupata kura za Wakristo Wainjilisti ambao wanaweza kuwa na wasiwasi wa kumuunga mkono Trump.

    Wakati huu, amemchagua JD Vance. Na kama chaguo lake la awali, uteuzi wa seneta huyo unatoa mwanga kuhusu mkakati wa kampeni ya rais huyo wa zamani - na, pengine, jinsi angetawala ikiwa atarejea Ikulu ya Marekani.

    Chaguo linapendekeza Trump anajua uchaguzi huu atashinda na kushindwa katika majimbo machache yanayokuwa na ushindani mkubwa ya Midwest.

    Kwa historia yake, Vance anaweza kuwa katika nafasi nzuri ya kuungana na kuwatia nguvu wapiga kura wazungu, wanaofanyakazi ambao walimpa ushindi Trump mnamo 2016.

    Rais huyo wa zamani alisema hayo, katika ujumbe wake mtandaoni akitangaza uamuzi wake, na kusema kuwa mgombea mwenza wake "atazingatia sana watu aliowapigania mno, wafanyikazi wa Marekani na wakulima huko Pennsylvania, Michigan, Wisconsin, Ohio, Minnesota na zaidi".

    Trump aliendelea kusifu huduma ya kijeshi ya mteule wake.

    Na ikiwa rais huyo wa zamani atarejea ikulu mwaka ujao, Vance atajiunga mara moja kwenye mazungumzo ya uteuzi wa urais wa chama 2028.

  14. Pango lililogunduliwa mwezini linaweza kuwa makao ya wanadamu

    Wanasayansi kwa mara ya kwanza wamegundua pango kwenye Mwezi.

    Pango hilo lenye kina cha mita 100, linaweza kuwa mahali pazuri kwa wanadamu kujenga makao ya kudumu, wanasema.

    Ni moja tu kati ya mamia ya mapango yaliyofichwa katika "ulimwengu wa chini ya ardhi, ambao haujagunduliwa", kulingana na watafiti.

    Nchi zinakimbia ili kupata makao kudumu wa binadamu mwezini, lakini zitahitaji kuwalinda wanaanga dhidi ya mionzi, halijoto kali na hali ya hewa ya anga.

    Helen Sharman, mwanaanga wa kwanza wa Uingereza kusafiri angani, aliiambia BBC News kwamba pango hilo jipya lililogunduliwa lilionekana kama mahali pazuri kwa makao na alipendekeza kuwa wanadamu wanaweza kuwa wanaishi kwenye mashimo ya mwezi katika miaka 20-30.

    Lakini, alisema, pango hili ni la kina sana hivi kwamba wanaanga wanaweza kuhitaji kujificha ndani na kutumia " lifti" ili kutoka.

    Lorenzo Bruzzone na Leonardo Carrer katika Chuo Kikuu cha Trento nchini Italia walipata pango hilo kwa kutumia rada kupenya shimo kwenye uwanda wa mawe unaoitwa Mare Tranquillitatis.

    Inaonekana kwa macho kutoka Duniani, na pia ndipo Apollo 11 ilitua mnamo 1969.

    Soma pia:

  15. Biden atetea kumwita Trump tishio kwa demokrasia

    Rais wa Marekani Joe Biden ametetea matamshi yake dhidi ya Donald Trump na kusema kwa nini ilikuwa muhimu, katika mahojiano yake ya kwanza tangu jaribio la mauaji ya mpinzani wake wa kisiasa.

    Rais alisema kampeni yake ilikuwa na jukumu la kuwasilisha kwa uwazi tishio la muhula wa pili wa Trump, na kuongeza kuwa maneno yake sio yale yanayohitaji kupunguzwa makali.

    Hata hivyo, alimwambia Lester Holt wa NBC kwamba lilikuwa "kosa" kusema ulikuwa "wakati wa kumwangazia Trump" wakati wa kukutana na wafadhili siku chache kabla ya jaribio la kumuua Trump lililotokea katika mkutano wa Jumamosi huko Pennsylvania.

    Bw Biden alisema anamaanisha kuwa Wanademokrat wanapaswa kuzingatia zaidi Trump, sera zake na taarifa za uongo alizotoa wakati wa mjadala wa urais mwishoni mwa mwezi uliopita.

    Wakati wote wa mahojiano, Bw Biden aliweka wazi kuwa hatajiondoa katika kinyang'anyiro cha urais - licha ya wito kutoka kwa wanachama wa chama chake baada ya utendakazi wake duni kwenye mjadala.

    "Mimi ni mzee," alisema, huku pia akibainisha kuwa yeye na Trump wamepishana kwa miaka mitatu pekee. Alisema uwezo wake wa kiakili ulikuwa mzuri na aliorodhesha mafanikio yake kama rais - lakini alikubali kwamba alikuwa akifanya kazi ili kuwahakikishia Wamarekani yuko sawa kushika nafasi hiyo.

    "Ninaelewa kwa nini watu husema, 'Mungu wangu, ana umri wa miaka 81. Lo. Atakuwa vipi atakapokuwa na umri wa miaka 83, miaka 84?' Ni swali zuri kujiuliza," alisema.

    Aliongeza kuwa imani yake iko kwa wapiga kura ambao kwa kiasi kikubwa walimuunga mkono katika mchujo wa chama cha Democratic. "Nawasikiliza."

    Soma zaidi:

  16. Shambulizi la Israel katika shule katikati mwa Gaza lasababisha vifo vya watu 22

    Takriban Wapalestina 22 waliuawa na wengine 100 kujeruhiwa katika shambulizi la siku ya Jumapili kwenye shule inayosimamiwa na Umoja wa Mataifa katikati mwa Gaza inayotumiwa kama makazi ya watu waliokimbia makazi yao, wizara ya afya inayosimamiwa na Hamas inasema.

    Jeshi la Israel limesema lililenga "magaidi" kadhaa wa Hamas wanaoendesha shughuli zao kutoka shule ya Abu Oraiban katika kambi ya wakimbizi ya Nuseirat iliyoko mjini.

    Walioshuhudia waliambia idhaa ya BBC Arabic hakukuwa na wapiganaji waliojihami na kwamba watoto walikuwepo ni miongoni mwa waliouawa.

    Lilikuwa ni shambulio la tano katika au karibu na shule katika muda wa siku nane.

    Wakaazi walisema kulikuwa na mashambulizi ya anga na mizinga katikati mwa Gaza siku ya Jumatatu, huku watu watano wakiripotiwa kuuawa wakati nyumba moja katika kambi ya wakimbizi ya Maghazi iliposhambuliwa.

    Jeshi la Israel lilisema ndege yake ilishambulia makumi ya maeneo ya "ugaidi yaliyolengwa" katika eneo lote katika siku iliyopita.

    Wakati huo huo, Hamas ilisema mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja juu ya makubaliano ya kusitisha mapigano na kuachiliwa kwa mateka na Israel "yanaendelea" wakati kunatokea shambulio la anga katika eneo la kusini mwa al-Mawasi Jumamosi ambalo wizara ya afya ilisema liliua zaidi ya watu 90.

    Jeshi la Israel lilisema lililenga eneo ambalo mkuu wa tawi la wapiganaji la Hamas, Mohammed Deif, alikuwa amejificha pamoja na kamanda wa Brigedi ya Khan Younis, Rafa Salama.

    Jeshi limetangaza kwamba Salama aliuawa, lakini walisema ni mapema mno kuhitimisha kama Deif pia alifariki. Upande mwingine, Hamas wamesema Deif yu bukheri wa afya.

    Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani alisema Antony Blinken alionyesha wasiwasi mkubwa kuhusu raia waliojeruhiwa hivi majuzi wakati wa mkutano na maafisa wawili wakuu wa Israel siku ya Jumatatu.

    Israel ilianzisha kampeni ya kijeshi huko Gaza ili kuiangamiza Hamas kujibu shambulio ambalo halijawahi kushuhudiwa kusini mwa Israel tarehe 7 Oktoba, ambapo takriban watu 1,200 waliuawa na wengine 251 walichukuliwa mateka.

    Zaidi ya watu 38,660 wameuawa huko Gaza tangu wakati huo, kulingana na wizara ya afya ya eneo hilo, ambayo takwimu hazitofautishi kati ya raia na wapiganaji.

    Soma zaidi:

  17. Mtu tajiri zaidi barani Afrika asema hana nyumba nje ya Nigeria

    Tajiri mkubwa barani Afrika Aliko Dangote amewashangaza watu wengi wa Nigeria baada ya kusema hana nyumba nje ya nchi hiyo.

    Bw Dangote alisema alikuwa na nyumba mbili - katika mji aliozaliwa wa Kano, na Lagos - na aliishi katika nyumba ya kukodi kila anapotembelea mji mkuu, Abuja.

    Aliorodheshwa na jarida la Forbes mwezi Januari kama mtu tajiri zaidi barani Afrika kwa mwaka wa 13 mfululizo licha ya matatizo ya kiuchumi nchini humo.

    Utajiri wake ulipanda kwa $400m zaidi mwaka jana, na kumpa thamani ya jumla ya $13.9bn (£10.7bn), Forbes walisema wakati huo.

    Mfanyabiashara huyo mwenye umri wa miaka 66 alijitajirisha kwa saruji na sukari - na mwaka jana alifungua kiwanda cha kusafisha mafuta katika kitovu cha uchumi cha Nigeria, Lagos.

    Mfanyabiashara huyo alibainisha hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika kiwanda cha kusafisha mafuta cha Dangote Jumapili.

    Maoni yake yaliwashangaza wengi katika nchi ambayo watu matajiri wana sifa ya maisha ya kifahari.

    Wanigeria wengi matajiri wanamiliki nyumba London, Dubai na Atlanta.

    Matamshi yake yamezua hisia nyingi kwenye mitandao ya kijamii, huku wengine wakisema ni uamuzi wa busara wa kibiashara kwani ni nafuu kulipa kodi kuliko kununua nyumba.

    Bw Dangote alisema sababu ya uamuzi wake ni kwamba anataka kuona Nigeria inakua.

    "Sababu ya kutokuwa na nyumba London au Marekani ni kuwa nilitaka kuangazia ukuaji wa viwanda nchini Nigeria," alisema.

    "Nina shauku kubwa juu ya ndoto ya Nigeria na kando na nyumba yangu ya Lagos, nina nyumba nyingine katika jimbo langu la Kano, na nyingine ya kukodi huko Abuja.

    "Ikiwa nitakuwa na nyumba kote Marekani na kwingineko, singeweza kutuliza akili na kufanya kitu kwa ajili ya watu wangu."

    Bw Dangote anajulikana kumiliki makazi ya kifahari katika Kisiwa cha Banana maarufu cha Lagos, ambako Wanigeria wengi wenye hadhi ya juu pia wana majumba ya kifahari.

    Mchanganuzi wa masuala ya umma Sani Bala alisema Bw Dangote alikuwa akionyesha mfano mzuri sana.

    "Wanaijeria wanahitaji kuelekezwa upya kuelewa kumiliki majumba kadhaa sio mafanikio wakati pesa zingehitajika mahali pengine.

    "Dangote alisema aliuza nyumba yake huko London mnamo mwaka 1996 na nina uhakika pesa zilizopatikana kutokana na mauzo zilirejeshwa katika biashara yake – huo ndio mfano wa kuiga."

    Soma zaidi:

  18. Bunge nchini Gambia lapinga mswada wa kuruhusu ukeketaji

    Wabunge nchini Gambia wamekataa mswada unaotaka kubatilisha marufuku ya mwaka 2015 ya ukeketaji.

    Spika wa Bunge, Fabakary Tombong Jatta alisema wabunge wengi wamepiga kura dhidi ya mswada huo hata kabla ya kusomwa kwa mara ya tatu na mwisho, unaotarajiwa baadaye mwezi huu.

    Mashirika ya kutetea haki za binadamu na Umoja wa Mataifa yalikuwa yamewataka wabunge kuzuia mswada huo uliowasilishwa mwezi Machi baada ya shinikizo kutoka kwa baadhi ya viongozi wa dini ya Kiislamu.

    Gambia ni miongoni mwa nchi 10 zenye viwango vya juu vya ukeketaji, huku asilimia 73 ya wanawake na wasichana wenye umri wa miaka 15 hadi 49 wakiwa wamefanyiwa utaratibu huo.

    Mswada, uliowasilishwa na Almameh Gibba, ilikataliwa baada ya wabunge kupiga kura dhidi ya vifungu vyake vyote vilivyopendekezwa.

    Bi Jatta alisema mswada huo "umekataliwa na mchakato wa kutunga sheria umekamilika", na kwa hivyo haungeweza kwenda hatua iliyofuata yaani kusomwa kwa mara ya tatu.

    Ulipowasilishwa mwezi Machi, mswada huo uliidhinishwa na wabunge wengi, na hivyo kuongeza matarajio ya Gambia kuwa nchi ya kwanza kubatilisha marufuku ya tabia hiyo.

    Katika utaratibu wa ukeketaji, unaofanywa Gambia mwanamke hukatwa ‘’kisimi’’,na kushonwa sehemu za siri ili asiweze kufanya au kufurahia tendo la ndoa.

    Soma zaidi:

  19. Trump aliyefungwa bandeji akaribishwa kwa nderemo katika kongamano la chama cha Republican

    Rais Donald Trump amehudhuria mkutano wa chama cha Republican akikaribishwa kwa shangwe na nderemo.

    Hii ni mara ya kwanza kwake kuonekana kwenye hafla kubwa ya umma tangu jaribio la mauaji dhidi yake kwenye mkutano wa kisiasa siku ya Jumamosi.

    Bandeji iliyokuwa kwenye sikio la Trump ilionekana wazi huku akichukua nafasi yake karibu na mgombea mwenza wake, JD Vance.

    Wafuasi wa Republican walikuwa na furaha isiyokifani.

    Walianza kuimba "U-S-A, U-S-A" na kuendelea kusema "Pambana! Pambana! Pambana!" huku wakirusha ngumi hewani, ishara kwamba wengi hapa wamemkubali baada ya Trump kuonyesha kuwa imara alipokuwa anashuka jukwaani baada ya kupigwa risasi huko Pennsylvania.

    Wengine waliokuwepo ni pamoja na wanafamilia, kama vile wanawe Eric na Donald Jr.

    Rais huyo wa zamani alionekana kutabasamu na kupiga makofi wakati wote wa hotuba.

    Mara kwa mara aliwageukiwa Vance na Donald kutoa maoni juu ya kile kilichosikika.

    Soma zaidi:

  20. Hujambo na karibu katika matangazo yetu mubashara ikiwa ni tarehe 16/7/2024