Maandamano yaendelea Venezuela huku hasira ikiongezeka kwa matokeo ya uchaguzi yenye utata
Maandamano yaendelea katika mji mkuu wa Venezuela Caracas baada ya matokeo yenye utata ya uchaguzi wa rais nchini humo.
Maelfu ya watu walikusanyika katikati mwa jiji ili kuonyesha upinzani wao dhidi ya madai ya ushindi wa Rais Nicolas Maduro.
Wengi walisema hawatakoma hadi kuwe na serikali mpya, na wengine walisema hili litaafikiwa tu ikiwa vikosi vya usalama vitaungana na waandamanaji wa upinzani.
Hata hivyo wanajeshi na polisi hadi sasa wamesalia watiifu kwa Bw Maduro na wamewafyatulia mabomu ya kutoa machozi na risasi za mpira baadhi ya waandamanaji.
Maafisa wa eneo hilo wanasema karibu watu 750 wamekamatwa. Mashirika mawili maarufu yasiyo ya kiserikali nchini humo yanasema watu kadhaa wamefariki dunia na makumi ya wengine kujeruhiwa.
Siku ya Jumanne waziri wa ulinzi wa Venezuela alielezea maandamano hayo kama "mapinduzi".
Akiwa amezungukwa na wanajeshi wenye silaha, Jenerali Vladimir Padrino alisoma taarifa akisema kwamba "uaminifu" kwa Rais Nicolás Maduro uko imara "na uungwaji mkono usio na masharti" wa jeshi
Mwanasheria mkuu wa Venezuela, ambaye ni mshirika wa karibu wa Bw Maduro, alisema mwanajeshi mmoja aliuawa katika maandamano ya kuipinga serikali.
Kiongozi wa upinzani Maria Corina Machado alitaka maandamano yawe ya amani.
"Lazima tuendelee kwa njia ya amani. Hatupaswi kutumbukia katika chokochoko ambazo serikali imetulenga. Wanataka kuwafanya Wavenezuela wakabiliane dhidi yao," alisema.
"Mgombea wetu alipata 70% ya kura. Tuliunganisha nchi, Wavenezuela ambao wakati fulani walimwamini Maduro wako nasi leo."
Mwandamanaji mmoja anayeipinga serikali ambaye hakutaka jina lake litajwe, aliambia BBC kwamba wameona ushahidi wa udanganyifu katika uchaguzi.
Soma zaidi: