Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Vita vya Ukraine: Kijiji cha mpakani kinachokaribiana na Urusi na Belarus
Kijiji cha Senkivka huko Ukraini kiko kwenye kiunganisho cha mpaka kati ya Ukraine, Urusi na Belarus.
Eneo ambalo kwa wakati fulani lilisherehekea urafiki kati ya nchi hizo tatu, sasa ni mstari wa mbele katika vita, na wakazi wake wanasimulia kuhusu familia zimetenganishwa kwa mipaka ambako zinaishi kwa hofu.
Kwa ufikiaji adimu wa kijiji hicho, Yogita Limaye amejionea mwenyewe athari za jamii iliyosambaratishwa na vita.
Vikosi vya Urusi viliondoka kaskazini mwa Ukraine mwanzoni mwa Aprili, lakini mashambulizi ya makombora na maguruneti yanaendelea huko Senkivka.
Kabla ya uvamizi huo, palikuwa na watu zaidi ya 200.
Sasa kuna wachache tu ambao wamebaki nyuma.
Nyumba ya Nina Malenok iko kando tu ya barabara ambayo wanajeshi wa Urusi walitumia walipokuwa wakianza uvamizi wa Ukraine, walipokuwa wakielekea katika mji wa kaskazini mwa Chernihiv, na mji mkuu wa Kyiv.
Ndani ya yadi ya nyumba ya Nina kuna mkia wa roketi iliyorushwa mapema Februari 24 - siku ambayo vita vilianza.
''Niliisikia roketi ikianguka kwenye yadi yangu. Kulikuwa na moto na moshi kila mahali, taa zangu zilizimika. Niliruka kitandani na kukimbia nje ya nyumba yangu,'' alisema Nina.
Siku zilizofuata, akiwa amejificha kwenye hifadhi, alisikia ndege zikipaa kwa juu, magari makubwa yakiingia na filimbi zikipulizwa mara kwa mara.
Mnamo Machi 8, waandishi wa habari wa TV wa Urusi walikuja nyumbani kwake wakiandamana na askari wa Urusi.
''Walikuwa wakirekodi kila kitu hapa, makombora yote na kila kitu. Waliniambia Ukraine inajishambulia yenyewe. Kisha wakatuma nambari [zilizochapishwa] kwenye roketi kwa mtu huko Urusi, na wakapokea jibu mara moja kwamba ilikuwa moja ya makombora yao.''
Makombora mengi kama haya yametawanyika kote kijijini.
Wataalamu ambao wameona picha za roketi hizo wameiambia BBC kwamba zingeweza kuwa zimebeba mabomu ya vishada, yaliyopigwa marufuku katika sehemu nyingine za dunia kwa uharibifu unaosababisha.
Urusi na Ukraine zote mbili zimeshutumiwa kutumia roketi hizo.
Hata baada ya kujiondoa, Nina hajisikii akiwa salama.
''Inatisha kuishi hivi, lakini nimezoea nyumba yangu, nitaenda wapi? Ninasikia makombora. Ninaweza kukuonyesha kutoka kwa uwanja wangu kizuizi cha ukaguzi cha Urusi,'' alisema.
Nyumba yake, na wengine katika kijiji hicho wanaonekana kutoka Urusi.
Wanajeshi wake wanaweza kuona kile ambacho wamekuwa wakikirushia risasi.
Kwa Lidiya Bilousova, ni mara ya pili maishani mwake kuona mizinga kwenye mlango wake.
Soma zaidi:
Alizaliwa mwaka wa 1930, anakumbuka vyema Vita vya Pili vya Dunia na wanajeshi wa Ujerumani wakija katika kijiji chao.
''Tulipewa onyo na wanajeshi wetu waliokuwa wakijisalimisha kwamba watakuja.
Kwa hiyo tulijificha kwenye mahandaki tukiwa na mikate mikavu iliyohifadhiwa kwenye mifuko ya nguo.
Kulipopambazuka, walikuwa katika barabara zetu, wakiwa na farasi zao na zana zao, wakivuka bustani zetu na bunduki za rashasha.
Lakini hakukuwa na urushaji wa makombora mengi kama ilivyo sasa,'' alisema.
''Hapo zamani, ningeweza nimekimbia.''
''Lakini sasa mimi ni mzee. Siwezi tena. Haya ndiyo nitakuambia, hakuna kitu kizuri kuhusu vita,'' Lidiya alisema.
''Baada ya vita vya mwisho [Vita vya Pili vya Dunia] tulibaki na nini?''
Kurushwa kwa makombora kunamtisha, lakini hataki kuondoka katika nyumba ambayo amekuwa akiishi kwa muda mrefu wa maisha yake.
Kabla ya uvamizi wa Urusi huko Crimea mnamo mwaka 2014, njia tatu za kuvuka mpaka zingefunguliwa na tamasha la umoja lingeadhimishwa mahali ambapo nchi hizo zinakutana, ambapo mnara wa kumbukumbu wa urafiki kati yao unaoitwa ''Dada Watatu'' bado upo.
Ilikuwa tamasha nzuri.
Sisi, Warusi, Wabelarusi tungesherehekea pamoja.
Watu kutoka pande zote, waheshimiwa wangekuja wote,'' alisema.
Mume wa marehemu Lidiya alikuwa Belarusi.
''Nchi hizo tatu zilikuwa marafiki kwa miaka mingi, tulitembeleana, tukaoana.
Sasa yamepitwa na wakati. ''Familia na urafiki ulioenea mipakani umegawanyika kwa mawazo na kwa umbali.
Baada ya 2014, kuvuka mpaka ikawa vigumu kwa watu wa pande zote. Sasa, haiwezekani.
Ndugu wawili wa Mykhaylo Dudko, dada, wapwa wa kike na kiume wanaishi Urusi.
Hajakutana na familia yake kwa miaka mingi.
Sasa, hawezi kuwaelewa
''Dada yangu aliniambia ni sisi tulioanzisha vita. Lakini hatukuwa na nia hiyo. Ni Urusi iliyotuvamia. Nataka familia yangu itumie vichwa vyao, kuangalia hali hiyo kwa uhuru,'' alisema.
Nina Malenok alisema ameacha kuwasiliana na kaka yake anayeishi Belarusi.
''Anasema ni Marekani iliyokushambulia, na unailaumu Urusi. Yuko maili tano tu kuvuka mpaka, na haamini kinachotokea,'' alisema.
''Nataka kumuondoa katika maisha yangu kwa sababu hiyo.''
Unaweza pia kusoma
- YA MSINGI:Mzozo wa Ukraine: Kwanini Urusi inaivamia Ukraine na Putin anataka nini?
- UFAFANUZI:Mzozo wa Ukraine: Swift ni nini na kwa nini kuipiga marufuku Urusi ni muhimu sana?
- UCHAMBUZI:Mzozo wa Ukraine: Putin humsikiliza nani?
- KWENYE RAMANI:Uvamizi wa Ukraine: Shambulio la Urusi kwenye ramani
- ZELENSKY:Volodymyr Zelensky: Mfahamu rais wa Ukraine aliyeacha umaarufu wake wa TV na kuingia kwenye siasa
- PUTIN:Vladimir Putin: Rais wa Urusi aliyeagiza shambulio Ukraine
- SILAHA:Mzozo wa Ukraine:Makombora ya stinger na silaha nyingine kali zinazotumiwa Ukraine