Ifahamu hati ya kufutiwa mashitaka 'Nolle Prosequi' na vigogo walionufaika nayo Tanzania

Iliyochapishwa

Moja ya kesi maarufu katika miaka ya hivi karibuni nchini Tanzania ya mashtaka dhidi ya ugaidi ya Masheikh wa Jumuiya za Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu Zanzibar (JUMIKI), waliokuwa gerezani nchini kwa zaidi ya miaka saba imefikia tamati wiki iliyopita kwa masheikh hao kuachiwa huru, baada ya mashtaka dhidi yao kufutwa.

Kesi yao ilikuwa na mvuto kwa makundi mengi ikiwemo wanasiasa, watetezi wa haki za binadamu pamoja na viongozi wa dini, waliokuwa wanataka waachiwe ama wahukumiwe kama ushahidi upo, lakini waliachiwa huru kupitia hati ya kufuta mashitaka ya Mwendesha mashtaka (DPP), inayofahamika kama 'Nolle Prosequi'.

Hati hii hutolewa na DPP akieleza kutokuwa na nia ya kuendelea na kesi na hivyo kuiomba mahakama kufuta mashtaka dhidi ya mtuhumiwa ama watuhumiwa.

Vigezo gani vinaangaliwa wakati wakutoa 'Nolle'?

Mwendesha Mashataka (DPP), ana mamlaka kisheria chini ya kifungu cha 91 (1) cha sheria ya makosa ya jinai (CPA), kuondoa mashitaka dhidi ya mtuhumiwa yeyote lakini vipo vigezo vya kawaida vya utoaji wa 'Nolle' lakini kigezo kikubwa kinachotumika sana ni kama DPP anaona hakuna ushahidi wa kutosha wa kumtia hatiani mtuhumiwa. Kisheria makosa ya jinai yanapaswa kuwa na ushahidi wa kutosha na usio na shaka hata chembe ili kumtia hatiani mtuhumiwa.

Na iwapo DPP atatumia mamlka yake haya ya kumuondolea mashtaka mtuhumiwa, halazimiki kutoa sababu yoyote ya kwanini ameamua hivyo, mamlaka ambayo baadhi ya wanasheria wanayaona ni makubwa mno na akipatikana mtu asiye muadilifu anaweza kuyatumia vibaya.

Mwanasheria Edwin Mugambila, amemwambia mwandishi wa makala hii kwamba Nolle ni kitu kizuri, ila kinapaswa kuboreshwa.

'Nolle ni vizuri iwepo, ila uwekwe utaratibu maalumu wa uwazi na kuelezwa sababu ya msingi za kwanini DPP atoe Nolle na fidia gani zitatolewa kwa waliokaa ndani muda mrefu mfano miaka zaidi ya mitano, ili kurejesha imani ya watu katika mifumo ya kisheria', alisema Mugambila.

Utaratibu huu umewanufaisha watu wengi hasa katika kipindi cha hivi karibuni. Ukiacha Mashekh wa Uamsho waliokuwa wakikabiliwa na mashitaka ya ugaidi, wafuatao ni watu watano wengine walionufaika na 'Nolle Prosequi'.

1: Yusuf Manji

Huyu ni mfanyabiashara mkubwa nchini Tanzania, ambaye yeye na wenzake watatu walikuwa wanakabiliwa na mashtaka saba ya uhujumu uchumi, kwa kukutwa na mabunda 35 ya vitambaa vinavyotumika kutengeneza sare ya jeshi la wananchi wa Tanzania (JWTZ) zenye thamani ya dola zaidi 80,000.

Septemba mwaka 2017, Mahakama ya Hakimyu Mkazi Kisutu ilimuachiwa huru mfanyabiashara huyu baada ya kukaa ndani kwa zaidi ya siku 70. Kesi yake ilivutia wengi mbali na kuwa mfanyabiashara anayefahamika, alikuwa pia ni Mwenyekiti wa klabu ya soka ya Yanga, mabingwa wa kihistoria nchini humo.

Wakati wa kusikilizwa kwa kesi yake, kuna wakati Mahakama hiyo ililazimika kuhamia katika Taasisi ya Jakaya Kikwete (JKCI) iliyoko katika Hopsitali ya Taifa ya Muhimbili na kusomewa mashtaka yake saba ya uhujumu uchumi. Wakati huo, Manji alikuwa hospitalini kwa matibabu ya matatizo ya moyo.

Baada kuhitimishwa kwa kesi hiyo, Manji aliondoka nchini kabla ya kurejea tena mapema mwezi huu, baada ya Rais Samia Suluhu kuhimiza wafanyabiashara waliotoroka nchi kurejea na kuendelea na uwekezaji wao.

2: Marijan Abubakar 'Papaa Msofe'

Mfanyabiashara huyu maarufu alikuwa akikabiliwa na mashtaka kadhaa kati ya mwaka 2010 mpaka 2019, lakini mashtaka yaliyotikisa vyombo vya habari yalikuwa ni mashtaka ya mauaji.

Mshataka hayo yalimuweka ndani yeye na mwenzake, Makongoro Jospeh, kwa zaidi ya miaka miwili. Sababu ya kukaa ndani muda huo, mara zote ilielezwa kuwa ni kutokamilika kwa ushahidi. Ameachiwa huru Juni 18, 2021, kupitia 'Nolle' ya DPP.

3: Adam Kighoma Malima

Aliwahi kuwa mbunge wa jimbo la Mkuranga na Naibu waziri wa fedha na Uchumi katika serikali ya awamu ya nne chini ya Rais Mstaafu Jakaya Kikwete. Amewahi kuwa mkuu wa mkoa wa Mara chini ya Rais John Magufuli na sasa ni Mkuu wa Mkoa wa Tanga katika serikali ya Rais Samia Suluhu.

Mwaka 2017 Kigogo huyu alikuwa ana kesi ya kushambulia na kumzuia ofisa Polisi Konstebo Abdu kufanya kazi yake kihalali, tukio lililodaiwa kufanyika Mei 15, 2017. Tukio hilo lilisambaa zaidi na kuzua mjadala kwenye mitandao ya kijami.

Mahakama ilimfutia kesi yake hiyo, siku sita tu baada ya kuteuliwa kuwa mkuu wa mkoa wa Mara na aliyekuwa Rais wa taifa hilo, Magufuli. Ingawa hakuwepo Mahakamani wakati kesi yake inafutwa, lakini alinufaika na 'Nolle' iliyoitishwa na Mkurugenzi wa Mashataka( DPP), aliyeonyesha kutokuwa na nia ya kuendelea kesi.

4: Tiagi Masamaki

Alikuwa miongoni wa vigogo wa juu kabisa wa mwanzo mwanzo kufikishishwa mahakamani kwa makosa ya uhujumu uchumi chini ya utawala wa Rais John Magufuli. Alikuwa ndiye kiongozi wa juu wa kukusanya mapato ya serikali ya nchi hiyo, Kamishna wa Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA). Masamaki alikabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi ya kuisababishia serikali hasara ya dola karibu milioni 5.4. Na yeye ni mnufaika wa 'Nolle' ya Mkurugenzi wa Mashataka( DPP).

5: Laurean Bwanakunu

Alikuwa Mkurugenzi wa Bohari ya Dawa Tanzania (MSD). Alikuwa anakabiliwa na mashitaka matano likiwemo la utakatishaji wa fedha haramu zaidi ya dola nusu milioni, makosa aliyodaiwa kuyafanya yeye na mwenzake, Byekwaso Tabura, aliyekuwa Mkurugenzi wa Logistiki wa bodi hiyo katika kipindi cha kati ya Julai 1 2016 mpaka Juni 30, 2019.

Lakini baadae Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ikamuachia kupitia 'Nolle Prosequi', iliyowasilishwa na mwendesha mashitaka.