Nicki Minaj kumlipa Tracy Chapman dola 450,000 katika kesi ya hakimiliki

Nicki Minaj and Tracy Chapman

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Minaj awali hakujua kuwa wimbo wake umeiga utunzi wa Chapman
Iliyochapishwa

Msanii wa muziki wa kufokafoka au rapper ukipenda Nicki Minaj atamlipa msanii Tracy Chapman dola 450,000 ili wamalize uhasama wao wa hakimiliki baada ya kuiga utunzi wa moja ya nyimbo zake.

Chapman alimshtaki Minaj mwaka 2018 akisema ametumia sehemu ya wimbo wake wa 'Baby Can I Hold You Tonight' katika wimbo wake wa 'Sorry'.

Ingawa wimbo huo haukuwahi kutolewa, tayari ulikuwa umevuja na kumfikia DJ Funkmaster Flex na hapo ndio ukaanza kusambaa kwenye mitandao ya kijamii.

Chapman alimshutumu Minaj kwa kutoa wimbo huo kwa Flex ingawa wote wawili wamekanusha madai hayo. Minaj aliandika wimbo Sorry rapper mwenzake Nas wakati anarekodi albamu yake ya nne Queen mwaka 2018.

Wimbo huo ulikuwa umeiga mtindo wa dancehall unaojulikana kama Sorry ulioimbwa na msanii wa Jamaica Shelly Thunder.

Minaj, asijue kuwa wimbo wa Baby, Can I Hold You Tonight, ni wa Chapman ambaye pia ni mshindi wa Tuzo ya Grammy.

Baada ya kugundua hivyo, Minaj na kampuni yake ya kurekodi muziki walijaribu kupata ruhusu ya kutumia utunzi wa Chapman lakini mwimbaji huyo alikataa.

Miongoni mwa hatua zilizochukuliwa na jaji ni kuangalia namna wimbo Sorry ulivyovuja na kuanza kusambazwa mitandaoni na ikiwa hilo ni ukiukaji wa hakimiliki.

Kesi hiyo imefika mwisho baada ya Chapman kukubali kulipwa na Minaj pesa ambazo zinajumuisha gharama za Chapman na zile za kulipia kesi hadi kufikia sasa kulingana na nyaraka zilizowekwa wazi na mahakama moja huko California.