Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Watu 10 wahofiwa kufa katika ajali ya boti ziwa Tanganyika
Watu wapatao 10 wamefariki na wengine 87 wameokolewa katika ajali ya boti iliyotokea ziwa Tanganyika nchini Tanzania.
Mamlaka imethibitisha tukio hilo kutokea baada ya boti kupinduka majira ya mchana, Alhamisi kutokana na dhoruba kali.
Polisi wamesema bado uchunguzi unaendelea ili kubaini kama waathirika wengine wanaweza kupatikana na taarifa juu ya ajali hii zitaendelea kutolewa.
Aidha vyombo vya habari nchini humo vinasema,mashuhuda na wakazi wa eneo hilo lililotokea Kijiji cha Sibwesa kuelekea Ikora mkoani Katavi wanasema chanzo cha ajali hiyo ni boti kuwa imejaza kupita uwezo wake na hivyo kusababisha kuzama majini.
Idadi ya abiria pia haijaweza kufahamika.
Julai 16, mamlaka ya hali ya hewa ilitoa angalizo kuwa kutakuwa na mawimbi na upepo mkali katika ziwa Tanganyika.
Mamlaka hiyo ilieleza kuwa hali ya hewa itavuruga shughuli za uvuvi na usafiri wa majini.
Mwezi mmoja iliopita ajali kama hii ilitokea katika eneo la kijiji cha Simbwesa ambapo watu tisa walifariki kati ya abiria 60 waliokuwemo katika boti.