Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Korea Kaskazini imemuita kiongozi wa Japan 'mpumbavu' na mwanasiasa mwenye fikra za chini
Korea Kaskazini imemuita waziri mkuu wa Japan Shinzo Abe kuwa ''punguani'' na mwanasiasa wa tajiriba ya chini asiye na ushawishi ikiishutumu kutoa taarifa ya kupotosha kuhusu jaribio la sasa la silaha zake.
Waziri Mkuu Abe ameikemea Korea Kaskazini kwa ''vitendo vyake vya kurusha makombora mara kwa mara'' baada ya makombora mawili siku ya Alhamisi.
Lakini Korea Kaskazini imesema ilikuwa inafanya majaribio ya ''roketi yake kubwa''
Korea Kaskazini imepigwa marufuku kufyatua makombora marufuku hiyo imekuja chini ya makubaliano ya baraza la usalama la Umoja wa Mataifa.
Nchi hiyo inakabiliwa na vikwazo kwa sababu ya mpango wake ya nyuklia.
Kuondosha vikwazo imekuwa ni kusudio kubwa kwa Korea kaskazini kuwa katika mazungumzo na Marekani-mshirika wa Japan lakini mazungumzo yamesimama tangu baada ya mkutano kati ya kiongozi wa nchi hiyo Kim Jong-un na rais Donald Trump ulipovunjika mwezi Februari.
Kulitokea nini?
Korea Kaskazini ilifyatua kile kinachoelezwa na waangalizi wa Korea Kusini kuwa ''makombora mawili'' kutoka jimbo lake la kusini la Hamgyong kuelekea bahari ya Japan siku ya Alhamisi.
Akikemea tukio hilo, Bwana Abe amesema: ''Korea ya Kaskazini kitendo cha kufyatua makombora ni uasi si tu kwa nchi yetu lakini pia kwa jumuia ya kimataifa.''
Korea Kaskazini imetoa picha zinazoelezwa kuwa za Kim akikagua tukio hilo.
Chombo cha habari cha serikali ya Korea Kaskazini kimesema: ''Unaweza kusema Abe ni mjinga pekee duniani na mpumbavu kuwahi kutokea kwenye historia kwa kushindwa kutofautisha kati ya Kombora na mfumo wa kurusha roketi alipoitazama picha na ripoti.''
Kiliongeza: "Abe ni punguani na ni mwanasiasa mwenye tajiriba ya chini asiye na ushawishi.''
Unaweza pia kusoma
Mazungumzo yamefikia wapi?
Mazungumzo kati ya Korea Kaskazini na Marekani yemesimama tangu kuvunjika kwa mkutanowa mwezi Februari mjini Hanoi.
Trump na Kim walikutana tena katika eneo linalozigawanya nchi za Korea mwezi Juni na kukubaliana kuanza tena jitihada za kuanzisha tena mazungumzo.
Walianza mwezi Oktoba, lakini walishindwa kupiga hatua yoyote.
Korea imeitaka Marekani kubadili mwelekeo ifikapo mwishoni mwa mwaka.
Mwezi Mei, Abe alisema kuwa yuko tayari kukutana na Kim ''bila masharti'', hatua iliyotoa matumaini ya kuanza upya kwa mazungumzo kuhusu masuala ya Nyukilia pia kuhusu mgogoro wa muda mrefu kuhusu Korea Kaskazini kuwateka raia wa Japan.
Raia wa Japan walichukuliwa Korea Kaskazini miongo kadhaa iliyopita kusaidia kuwafunza majasusi wake. Japan inaamini raia wake 17 walitekwa, watano pekee kati yao wamerejeshwa.