Majengo 10 marefu zaidi Afrika Mashariki 2026

.

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Makao Makuu ya CBE, Addis Ababa.
    • Author, Abdalla Dzungu
    • Nafasi, BBC Swahili
    • Akiripoti kutoka, Nairobi Kenya
  • Iliyochapishwa
  • Muda wa kusoma: Dakika 5

Mandhari ya anga ya Afrika Mashariki inabadilika kwa kasi huku majengo marefu ya Nairobi, Dar es Salaam, na Kigali yakichukua nafasi ya juu, jambo linaloakisi ukuaji wa uchumi na azma ya maendeleo ya mijini katika eneo hili.

Kulingana na Construction Kenya {CK} Mbali na urefu wao, majengo haya ni alama za maendeleo; yanaunda mandhari ya miji na kuashiria nafasi inayozidi kukua ya Afrika Mashariki katika maendeleo ya mijini na uchumi barani Afrika.

Haya hapa ni majengo 10 marefu zaidi Afrika Mashariki kulingana na CK:

1. Makao Makuu ya CBE, Addis Ababa.

Makao Makuu ya Commercial Bank of Ethiopia ni jengo refu lenye ghorofa 53 lenye urefu wa mita 209, lililopo Addis Ababa, mji mkuu wa Ethiopia.

Jengo hilo, ambalo ujenzi wake ulikamilika mwezi Februari 2022, ndilo jengo refu zaidi katika Afrika Mashariki.

Jumba hilo la kisasa ni ofisi inayotumika kama makao makuu ya Commercial Bank of Ethiopia na kusimama kama ishara ya ukuaji wa uchumi na maendeleo ya mijini nchini humo.

2. Britam Tower, Nairobi

.

Chanzo cha picha, (Photo: Courtesy CK

Maelezo ya picha, Britam Towers Nairobi

Britam Tower, jengo la ofisi lenye urefu wa mita 200 lililoko Upper Hill, Nairobi, lilizinduliwa rasmi kwa matumizi ya umma mnamo Julai 2018, na kulipiku jengo la UAP Old Mutual Tower kama jengo refu zaidi nchini Kenya.

Jengo hilo lenye ghorofa 32, ambalo ujenzi wake ulianza mwanzoni mwa mwaka 2013 na kukamilika mnamo Septemba 2017, linajivunia muundo wa kipekee wa umbo la 'prism'.

Katika sehemu yake pana zaidi, jengo hilo linaonekana kama piramidi nyeusi ambayo imekosa ncha ya juu, na likitazamwa kutoka pembe nyingine, linaonekana kama umbo jembamba zaidi la 'prism' nyeusi.

Mnamo mwaka wa 2018, Britam Tower ilikuwa jengo la kwanza barani Afrika kuingizwa katika orodha ya tuzo ya Emporis Skyscrapers Award katika historia yake ya miaka 19, likishika nafasi ya 10 kati ya majengo marefu bora duniani.

3. Jengo la Ofisi la GTC, Nairobi

GTC Office Tower ni jengo la ofisi lenye urefu wa mita 184 na ghorofa 42 lililoko Westlands, Nairobi. Likiwa sehemu ya Global Trade Centre, ujenzi wake ulikamilika mwaka wa 2022 na kulifanya kuwa mojawapo ya majengo marefu zaidi ya ofisi Afrika Mashariki.

likiwa imeundwa kwa muundo wa kisasa wa kuta za vioo na vifaa vya kiwango cha juu jengo hilo lina ofisi za hadhi ya juu na linachukua nafasi muhimu katika mandhari ya anga ya Nairobi inayobadilika kwa kasi.

4. UAP Old Mutual Tower, Nairobi

.

Chanzo cha picha, Getty Images

UAP Old Mutual Tower ni jengo refu la ofisi lenye urefu wa mita 163 na ghorofa 33, lililoko katika eneo la Upper Hill jijini Nairobi, mji mkuu na jiji kubwa zaidi nchini Kenya.

Jengo hilo, ambalo ujenzi wake ulikamilika mwaka wa 2016, kwa muda mfupi lilishikilia rekodi ya kuwa jengo refu zaidi nchini Kenya lilipofunguliwa, kabla ya kupitwa na majengo ya Britam Tower na GTC Office Tower.

Iikiwa limeundwa kuwa na nafasi za kisasa za ofisi na biashara, jengo hili linasalia kuwa kivutio kikubwa katika mandhari ya anga na ya kibiashara ya Nairobi .

5. Makao Makuu ya PPF, Dar es Salaam

Makao Makuu ya PPF ni jengo refu la ofisi lenye urefu wa mita 160 na ghorofa 37, lililopo Barabara ya Sam Nujoma jijini Dar es Salaam, Tanzania.

Jengo hilo, ambalo ujenzi wake ulikamilika mwaka 2019, ndilo jengo refu zaidi nchini Tanzania.

Jengo hilo la kisasa la ghorofa nyingi hutumika kama makao makuu ya Mfuko wa Pensheni wa Mashirika ya Umma (PPF) .

6. Mamlaka ya Bandari Tanzania, Dar es Salaam

Mnara wa Mamlaka ya Bandari Tanzania ni jengo refu la ofisi lenye urefu wa mita 157 na ghorofa 40, lililopo katika Barabara ya Sokoine jijini Dar es Salaam, kitovu cha biashara.

Jengo hilo, ambalo lilikamilika mwaka 2016, linatumika kama makao makuu ya Mamlaka ya Bandari Tanzania na lilikuwa miongoni mwa majengo marefu zaidi nchini wakati wa kukamilika kwake.

Muundo wa kisasa wa jengo hilo na eneo lake la kipekee linalotazamana na eneo la bandari hulifanya kuwa alama muhimu katika mandhari ya majengo ya jijini Dar es Salaam.

7. NSSF Pension Towers, Kampala

NSSF Pension Towers ni jengo la ghorofa 32 lenye urefu wa mita 155 lililojengwa katika Barabara ya Lumumba jijini Kampala, mji mkuu na jiji kubwa zaidi nchini Uganda.

Ujenzi huo, unaoongozwa na Mfuko wa Kitaifa wa Hifadhi ya Jamii (Uganda), lina mijengo mitatu iliyounganishwa na, ikikamilika, inatarajiwa kuwa majengo marefu zaidi nchini Uganda, na kuongeza nafasi kubwa ya kisasa ya ofisi na rejareja katika anga ya jiji.

Kukamilika kunatarajiwa mwaka wa 2026.

8. PSPF Commercial Towers A & B, Dar es Salaam

.

PSPF Commercial Towers A na B ni majengo pacha ya ofisi yenye urefu wa mita 152.7 na ghorofa 35 jijini Dar es Salaam.

Majengo hayo pacha, yaliyokamilika mwaka 2014, yalikuwa miongoni mwa majengo marefu zaidi nchini wakati wa kufunguliwa kwake na yanaendelea kuwa alama muhimu katika mandhari ya anga ya jiji hilo.

Majengo hayo yanajumuisha nafasi za ofisi na maeneo ya biashara, na yanaashiria nafasi inayozidi kukua ya Dar es Salaam kama kitovu cha biashara cha kikanda.

9. Mwalimu Nyerere Foundation Square, Dar es Salaam

Mwalimu Nyerere Foundation Square ni jengo refu la ghorofa 31 na urefu wa mita 145, linalotumika kwa shughuli mbalimbali na liko katika Mtaa wa Zanaki jijini Dar es Salaam.

Jengo hilo, ambalo ujenzi wake ulikamilika mwaka 2019, linajumuisha nafasi za ofisi, maeneo ya biashara na hoteli ya nyota tano, na pia linajulikana kama Johari Rotana Dar es Salaam.

Jina lake linaenzi urithi wa kiongozi mwanzilishi wa Tanzania, Julius Nyerere.

10. Nairobi GTC Hotel Tower, Nairobi

Nairobi GTC Hotel Tower ni jengo refu lenye urefu wa mita 143 na ghorofa 35, lililopo Westlands, Nairobi. Ni sehemu ya eneo la majengo ya GTC na ndani yake kuna Hoteli ya JW Marriott.

Jengo hilo, ambalo ujenzi wake ulikamilika mwaka wa 2022, linajulikana sana kutokana na muundo na urefu wake.

Linaongeza mvuto katika mandhari ya majengo marefu ya Nairobi na kuimarisha hadhi yake inayokua kama kitovu cha kikanda cha biashara na utalii.