Tetesi za Soka Ulaya Alhamisi 04.04.2024

Chanzo cha picha, Getty Images
Newcastle United wanahofia huenda wakahitaji kumuuza kiungo wa Brazil Bruno Guimaraes, 26, ili kukidhi sheria za kifedha za Ligi ya England. Miamba wa Ufaransa Paris St-Germain wanaongoza katika mbio hizo, huku Manchester United na Arsenal pia wakiwa na hamu. (Sun)
Tottenham pia wameungana na Arsenal katika kinyang'anyiro cha kumsajili mshambuliaji wa Uswidi Alexander Isak, 24, iwapo Newcastle italazimika kuuza wachezaji wake muhimu msimu huu wa joto. (Football Insider)
Lakini Isak amesisitiza kujitolea kwake kwa Newcastle huku kukiwa na nia ya wapinzani wa klabu yake ya Ligi ya Premia. (inews)

Chanzo cha picha, Reuters
Newcastle itapatia kipaumbele usajili wa mabeki wawili wakati dirisha la uhamisho litakapofunguliwa baada ya Mholanzi Sven Botman, 24, na Muingereza Jamaal Lascelles, 30, kukabiliwa na majeraha ya muda mrefu. (Football Insider)
Mshambuliaji wa Uswidi Viktor Gyokeres, 25, yuko juu kwenye orodha ya washambuliaji wa Arsenal, lakini Sporting Lisbon wanatarajia kipengele cha kuachiliwa kwa mchezaji huyo cha euro 100m (£85.6m) kuchochewa ili aondoke. (Caught Offside)
Kiungo wa kati wa Uingereza Kalvin Phillips, 28, atalazimika kukatwa mshahara mkubwa ikiwa anataka kondoka Manchester City na kurejea Leeds United msimu huu wa joto. (Mirror)

Chanzo cha picha, Getty Images
West Ham haina mpango wa kubadilisha mkataba wa mkopo wa Phillips kuwa wa kudumu katika klabu hiyo. (Football Insider)
Manchester United wameanza majadiliano kuhusu kumsajili beki wa Nice mwenye umri wa miaka 23 Melvin Bard, huku wakilenga kusajili beki mpya. (Evening Standard)
Beki wa Wolves Muingereza Max Kilman, 26, pia yuko kwenye orodha ya wachezaji wanaowania uhamisho wa majira ya kiangazi ya Manchester United. (Times - usajili unahitajika)

Chanzo cha picha, Getty Images
Leicester City wameingia kwenye kinyang'anyiro cha kumsajili mshambuliaji wa Arsenal Muingereza Eddie Nketiah mwenye umri wa miaka 24 lakini wanakabiliwa na ushindani kutoka kwa Crystal Palace na Brentford. (Football Transfers)
Arsenal, Liverpool na Manchester United ni miongoni mwa klabu za Ligi Kuu ya England zinazomuwania beki wa Bayer Leverkusen Jeremie Frimpong. Mholanzi huyo, 23, atapatikana kwa £35m msimu wa joto. (Football Insider)
Newcastle wanavutiwa na kiungo wa kati wa Real Madrid Muhispania Dani Ceballos, 27. (Mundo Deportivo - kwa Kihispania)
Imetafsiriwa na Ambia Hirsi












