Ukraine ilikomboa kilomita za mraba 6,000 mwezi Septemba- Zelensky

Chanzo cha picha, Reuters
Vikosi vya Ukraine vimeteka maeneo mengi zaidi kutoka kwa Urusi huku wakiendelea na mashambulizi yao, rais wa nchi hiyo amesema.
Volodymyr Zelensky alisema wanajeshi sasa wamechukua zaidi ya kilomita za mraba 6,000 (maili za mraba 2,317) kutoka kwa udhibiti wa Urusi mnamo Septemba, mashariki na kusini.
BBC haiwezi kuthibitisha takwimu hizi.
Urusi imekiri kupoteza miji muhimu katika eneo la kaskazini-mashariki la Kharkiv, katika kile kinachoonekana na baadhi ya wataalam wa kijeshi kama uwezekano wa mafanikio katika vita.
Moscow inaelezea uondoaji wake wa wanajeshi katika eneo hilo katika siku za hivi karibuni kama "kujipanga tena" kwa lengo la kuangazia maeneo ya Luhansk na Donetsk mashariki mwa Ukraine
Madai hayo yamewadhihaki wengi nchini Urusi, huku watumiaji wengi wa mitandao ya kijamii wakielezea kujiondoa kama "aibu".
Akizungumza na BBC Jumatatu jioni, Mason Clark wa taasisi ya wasomi yenye makao yake nchini Marekani ya Taasisi ya Utafiti wa Vita (ISW) alisema hii ilikuwa "shida kamili" ya wanajeshi wa Urusi, ambao walilazimika kuacha vifaa vingi nyuma.
Na mwandishi wa BBC James Waterhouse alisema kuwa ni tukio muhimu zaidi la kurudi kwa jeshi la Urusi tangu kampeni yake iliyofeli karibu na mji mkuu wa Kyiv mwishoni mwa mwezi Machi.
Akizungumza baadaye siku ya Jumatatu, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken alisema vikosi vya Ukraine vimepata "maendeleo makubwa" katika mapambano yao ya kukabiliana na mashambulizi, lakini akaongeza kuwa ni mapema mno kutabiri matokeo.
Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.
Bonyeza hapa kujiunga
Mwisho wa Whatsapp
"Warusi wanadumisha vikosi muhimu sana nchini Ukraine pamoja na vifaa na silaha na zana za kivita. Wanaendelea kuitumia kiholela sio tu dhidi ya wanajeshi wa Ukraine bali raia na miundombinu ya kiraia kama tulivyoona," Bw Blinken alisema.
Rais wa Urusi Vladimir Putin aliamuru uvamizi kamili wa Ukraine mnamo tarehe 24 Februari. Urusi bado inashikilia karibu theluthi moja ya nchi.
Katika hotuba yake ya mwisho ya video siku ya Jumatatu, Rais Zelensky alisema: "Tangu mwanzoni mwa Septemba hadi leo, wapiganaji wetu tayari wamekomboa zaidi ya kilomita za mraba 6,000 za eneo la Ukraine - mashariki na kusini".
"Harakati za wanajeshi wetu zinaendelea," alisema.
Uvamizi wa kukabiliana unaonekana kuwa wa haraka. Alhamisi iliyopita, Rais Zelensky alisema vikosi vya Ukraine vimechukua tena kilomita za mraba 1,000, lakini kufikia Jumapili idadi hiyo iliongezeka mara tatu hadi kilomita za mraba 3,000.
Bw Zelensky alishukuru brigedi kadhaa za Ukraine zilizohusika katika mashambulizi hayo, akiwataja wapiganaji wao kama "mashujaa wa kweli".
Hakufichua ni miji na vijiji gani vya Kiukreni vilikombolewa.
Jeshi la Urusi hapo awali lilikiri kwamba wanajeshi wake walilazimika kuondoka katika miji muhimu ya Balakliya, Izyum na Kupiansk katika mkoa wa Kharkiv. Urusi sasa inadhibiti sehemu ndogo tu ya mashariki ya eneo hilo.
Mafanikio makubwa - ingawa ya polepole - maendeleo ya wanajeshi wa Ukraine pia yameripotiwa katika eneo la kusini la Kherson, ambalo linapakana na Crimea - peninsula ya Ukraine iliyotwaliwa na Urusi mnamo 2014.
Maafisa wa ulinzi wa Uingereza wanasema mafanikio ya hivi majuzi ya jeshi la Ukraine yatakuwa na "madhara makubwa" kwa muundo wa jumla wa uendeshaji wa Urusi.
Hata hivyo, msemaji wa Kremlin Dmitry Peskov amesisitiza kuwa operesheni za kijeshi nchini Ukraine zitaendelea "mpaka kazi zote zilizowekwa awali" zitakapotimizwa.
Urusi inasema vikosi vyake vimekuwa vikiendesha mashambulizi katika maeneo hayo yaliyotwaliwa tena na Ukraine katika siku za hivi karibuni.
Valerii Marchenko, meya wa Izyum, aliiambia BBC kuwa jeshi la Ukraine lilikuwa katika mji wake na bendera ya taifa ilikuwa imepandishwa.
Wanajeshi sasa wanajishughulisha na kuusafisha mji huo uliokumbwa na vita na vikosi vya Ukraine vinawasaka wanajeshi wa Urusi ambao wanaweza kujificha kwenye nyumba za watu.
Bw Marchenko alisema kwamba baada ya "takriban siku 10", wakazi ambao walilazimika kutoroka jiji wataweza kurejea "salama".
Urusi imeshutumiwa kwa kulenga miundombinu ya kiraia ili kulipiza kisasi kwa kushindwa kwenye uwanja wa vita.
Wimbi la mashambulio ya makombora siku ya Jumapili lilisababisha kukatika kwa umeme kaskazini-mashariki mwa Ukraine, na kuwaacha makumi ya maelfu ya watu bila umeme na maji kwa saa kadhaa.


















