Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Vita vya Ukraine : Urusi yaharibu hospitali katika shambulio la hivi punde la kombora

Takriban watu wawili wameuawa na zaidi ya 30 kujeruhiwa katika shambulizi la kombora la Urusi hospitali iliyopo katika mji wa Dnipro mashariki mwa Ukraine, maafisa wa Ukraine wamesema.

Moja kwa moja

  1. Vita vya Ukraine: Urusi yaharibu hospitali katika shambulio la hivi punde la kombora

    Takriban watu wawili wameuawa na zaidi ya 30 kujeruhiwa katika shambulizi la kombora la Urusi kwenye hospitali katika mji wa Dnipro mashariki mwa Ukraine, maafisa wa Ukraine wamesema.

    Watoto wawili wavulana wenye umri wa miaka mitatu na sita pia walikuwa miongoni mwa waliojeruhiwa, mkuu wa mkoa Serhiy Lysak alisema.

    Rais Volodymyr Zelensky alielezea shambulio hilo kama "ukatili mtupu".

    Mashambulizi ya Urusi dhidi ya Ukraine yameongezeka katika wiki za hivi karibuni kabla ya shambulio linalotarajiwa la Ukraine.

    .Bw Zelensky alichapisha video ya kliniki iliyoharibika ambayo ilionyesha wazima moto kwenye eneo la tukio na moshi ukifuka kutoka kwa jengo hilo.

    "Magaidi wa Urusi kwa mara nyingine tena wanathibitisha hali yao ya wapiganaji dhidi ya kila kitu cha utu na uaminifu," alisema.

    Hapo awali, Bw Lysak alisema eneo hilo lilikumbwa na "mashambulizi makubwa...kwa makombora na ndege zisizo na rubani" Alhamisi usiku.

    "Ulikuwa usiku mgumu sana. Ilikuwa ni sauti kubwa," alisema. "Dnipro ameteseka."

    Katika eneo la tukio, wazima moto walikuwa wakikata miti ili kupata bomba lililowekwa karibu na moto ambao ulikuwa umeshika jengo kubwa la ghorofa tatu.

    Wakati huo huo, katikati ya vifusi, timu za uokoaji zilikuwa zikiwasaka watu wawili waliopotea.

    Mamlaka ya Ukraine ilisema ilirusha makombora 17 na ndege zisizo na rubani 31 zilizorushwa kutoka Urusi usiku kucha.

    Ndege zisizo na rubani na makombora kadhaa zililenga shabaha huko Dnipro na mji wa mashariki wa Kharkiv, pamoja na ghala la mafuta.

    Mji mkuu wa Ukraine, Kyiv, pia ulilengwa na maafisa walisema vipande vya ndege zisizo na rubani zilizonaswa zilianguka juu ya paa la kituo cha biashara, huku nyumba na magari kadhaa yakiharibiwa.

    Nchini Urusi, mlipuko uliharibu jengo la makazi na ofisi katika mji wa kusini wa Krasnodar siku ya Ijumaa asubuhi.

    Mashambulio ya Ukraine: Mengi zaidi

    • YA MSINGI:Mzozo wa Ukraine: Kwanini Urusi inaivamia Ukraine na Putin anataka nini?
    • UFAFANUZI:Mzozo wa Ukraine: Swift ni nini na kwa nini kuipiga marufuku Urusi ni muhimu sana?
    • UCHAMBUZI:Mzozo wa Ukraine: Putin humsikiliza nani?
    • KWENYE RAMANI:Uvamizi wa Ukraine: Shambulio la Urusi kwenye ramani
    • ZELENSKY:Volodymyr Zelensky: Mfahamu rais wa Ukraine aliyeacha umaarufu wake wa TV na kuingia kwenye siasa
    • PUTIN:Vladimir Putin: Rais wa Urusi aliyeagiza shambulio Ukraine
  2. Erling Haaland: Mshambulizi wa Man City ashinda tuzo za mchezaji na mchezaji bora chipukizi wa Primia Ligi

    Mchezaji wa Manchester City Erling Haaland amekuwa mchezaji wa kwanza kushinda tuzo za mchezaji bora wa mwaka wa Primia Ligi katika msimu mmoja.

    Mabao 36 ya mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 22 yamemfanya avunje rekodi ya Ligi Kuu ya England ya kufunga mabao mengi zaidi kwa msimu mmoja.

    Kwa jumla, amefunga mabao 52 wakati wa shindano.

    "Nina heshima kuwa mchezaji wa kwanza kushinda tuzo zote mbili katika msimu mmoja - asante kwa kila mtu aliyenipigia kura," alisema Haaland.

    Haaland, ambaye alipata kura nyingi zaidi kutoka kwa umma na jopo la Primia Ligi, alijiunga na City kutoka Borussia Dortmund msimu uliopita na ameisaidia klabu hiyo kushinda taji la tatu mfululizo la ligi ya juu.

    Tayari ameteuliwa kuwa Mwanasoka Bora wa Mwaka wa Chama cha Waandishi wa Soka (FWA).

    "Umekuwa msimu wa kwanza wa ajabu katika Ligi Kuu na kunyanyua kombe wikendi iliyopita mbele ya mashabiki wetu pale Etihad ulikuwa wakati wa kipekee sana kwangu," aliongeza mchezaji huyo wa kimataifa wa Norway.

    City pia wako mbioni kuwania Treble kwani watamenyana na Manchester United katika fainali ya Kombe la FA mnamo 3 Juni kabla ya kucheza na Inter Milan katika fainali ya Ligi ya Mabingwa mnamo Juni 10.

  3. Vita vya Ukraine: Mamia ya Wajerumani waliofukuzwa kuanza kuondoka Urusi

    Mamia ya Wajerumani wanaofanya kazi katika sekta ya elimu na utamaduni watafukuzwa Urusi mwezi ujao, wizara ya mambo ya nje ya Ujerumani inasema.

    Ilithibitisha ripoti za vyombo vya habari kwamba Urusi imeamua kupunguza idadi ya wafanyikazi wa Ujerumani kuanzia mwanzoni mwa Juni.

    Watakaofurushwa ni pamoja na waalimu katika shule ya Ujerumani iliyopo mjini Moscow na wafanyakazi katika taasisi ya kitamaduni ya Goethe Institute.

    Hatua hiyo inafuatia kufukuzwa kwa wanadiplomasia na kuendelea kuzorota kwa uhusiano kati ya Urusi na Ujerumani.

    Mwezi uliopita, Urusi na Ujerumani kila moja ilitangaza wafanyakazi 40 wa balozi za zao hawatakikani nchini humo - au kutokubalika - na kuwafukuza.

    Gazeti la kila siku la Ujerumani la Süddeutsche Zeitung liliripoti kwamba hatua ya hivi karibuni itawaathiri idadi ya wafanyakazi wa kibalozi , ikiwa ni pamoja na wanadiplomasia.

    "Kwa kuzingatia uamuzi huu wa upande mmoja, usio na msingi na usioeleweka, Serikali ya Ujerumani sasa inahusika na kuhakikisha uwepo wa angalau wapatanishi nchini Urusi huku pia ikidumisha uwepo wa kidiplomasia," gazeti hilo lilinukuu wizara ya mambo ya nje ya Ujerumani.

    Nchi kadhaa za Umoja wa Ulaya zimewatimua wanadiplomasia wa Urusi tangu kuanza kwa vita nchini Ukraine.

    Zaidi ya wanadiplomasia 40 wanaoshukiwa kufanya ujasusi walipewa amri ya kuondoka kutoka nchi nne za Muungano wa Ulaya mnamo Machi 2022.

    Urusi na Ujerumani zilikuwa na uhusiano mkubwa wa kiuchumi na kiutamaduni, ambao umeingia umetatizika pakubwa kutokana na uvamizi wa Urusi nchini Ukraine.

  4. Ngome ya wanajeshi wa Uganda nchini Somalia imeshambuliwa na Alshaabab - UPDF yathibitisha

    Ngome ya kijeshi ya wanajeshi wa Uganda UPDF, ambao ni sehemu ya kikosi cha walinda amani wa Umoja wa Afrika (ATMIS) kilichopo Somalia imeshambuliwa na wanamgambo wa Al-shaabab, kulingana na taarifa ya Wizara ya ulinzi na masuala ya wanajeshi wastaafu.

    Katika taarifa yake iliyotumwa kwenye mtandao wa kijami wa Twitter UPDF, imelaani vikali shambulio la Alshaabab dhidi ya wanajeshi wake lililotokea katika eneo la Buulu Mareer jimbo la Lower Shabelle kilomita 120 kusini -magharibimwa mji mkuu Mogadishu.

    Imesema shambulio hilo ‘‘halitazuia jukumu letu kwa ATMIS la kuhakikisha Afrika inakua huru na yenye utulivu’’, imesema taarifa ya wizara ya ulinzi ya Uganda.

    Kulingana na taarifa hiyo, Maafisa wa UPDF chini ya uongozi wa Kamanda wa vikosi vya ardhiniLuteni Jenerali Kayanja Muhanga wamekwenda Somalia kutathmani shambulio hilo hilo limetokea katika mazingira yapi.

  5. ‘Wachawi’ wa Connecticut waliofutiwa mashtaka na wabunge wa Seneti

    Wabunge wa jimbo la Connecticut wamepiga kura kuwaondolea hatia watu 12 zaidi ya miaka 370 baada ya kukutwa na hatia ya uchawi katika eneo la kikoloni la Marekani.

    Kumi na mmoja kati ya watuhumiwa 12 walinyongwa baada ya kesi ambazo Seneti ya jimbo sasa inakubali kuwaulikua ni "ukosefu wa haki".

    Hatua hii ya bunge la seneti inafuatia kampeni ya muda mrefu ya vizazi iliyolenga kusafisha majina ya wale wanaotuhumiwa kimakosa kuwa wachawi.

    Makumi ya watu waliuawa kwa uchawi huko Merika katika Karne ya 17.

    Siku ya Alhamisi, Seneti ya Connecticut ilipiga kura 33-1 kuwaondolea hatia wale waliopatikana na hatia katika kesi zilizofanyika katika jimbo hilo katikati ya miaka ya 1600.

    Seneta ambaye alipiga kura dhidi ya hatua hiyo, Rob Sampson, alisema kuwa anaamini kuwa ni makosa "kuamuru ni nini kilikuwa sahihi au kibaya kuhusu vipindi vya zamani ambavyo hatuna ujuzi navyo".

    "Sitaki kuona miswada ambayo kwa haki au kimakosa inajaribu kuipaka Marekani kama mahali pabaya na historia mbaya," alinukuliwa akisema na shirika la habari la Associated Press.

    "Nataka tuzingatie tunakoenda, ambao ni mustakabali mzuri na bora zaidi."alisema.

    Azimio hilo lilikuwa tayari limepitishwa katika Baraza la Wawakilishi la Connecticut, kwa kura 121 za ndio na 30 za kupinga.

  6. Mfugaji afariki baada ya kuteleza na kuanguka ndani ya eneo la Mamba

    Mfugajiwa mamba kaskazini mwa Cambodia ameraruliwa vipande-vipande na takriban mamba 40 baada ya kuteleza na kuanguka ndani ya eneo wanamoishi wanyama hao, polisi wa eneo hilo wamesema.

    Luan Nam, mwenye umri wa miaka 72, alijaribu kuopoa yai punde baada ya kutagwa na mnyama mmoja akitumia fimbo lakini mnyama huyo akaing'ata na ghafla ajajipindua kwa kasi, hatua iliyosababisha babu huyo kuteleza na kuanguka ndani ya ua linalowazuia wanyama hao hatari kwa mujibu wa ripoti ya polisi.

    "Mamba wengine walimrukia, na kumshambulia hadi akafa," mkuu wa polisi Mey Savry aliambia shirika la habari la AFP.

    Tukio hilo lilitokea karibu na mji wa Siem Reap siku ya Ijumaa.

    Mwili wa Bw Nam ulijaa alama za kuumwa na mkono wake mmoja haukuwepo, Bw Savry alisema.

    Muathiriwa alikuwa rais wa chama cha wakulima wafugaji wa mamba wa eneo hilo.

    Mnamo mwaka wa 2019, msichana wa miaka miwili aliuawa na kuliwa na mamba katika shamba kama hilo katika eneo hilo, ambalo liko karibu na hekalu maarufu duniani la Angkor Wat.

    Wanyama hufugwa kwa ajili ya mayai, ngozi na nyama katika taifa hilo la kusini-mashariki mwa Asia.

  7. Tazama:Video kutoka ndege ambayo mlango wake ulifunguliwa ikiwa angani

    Mwanaume mmoja amekamatwa baada ya mlango wa dharura wa ndege ya shirika la ndege la Asiana Airlines kufunguliwa ilipokuwaikikaribia kutua Korea Kusini.

    Ndege hiyo ilitua salama, lakini baadhi ya abiria walizirai na wengine walilazwa hospitalini wakiwa na matatizo ya kupumua, vyombo vya habari vya ndani viliripoti.

  8. Lionel Messi: Destiny - Filamu mpya yasimulia undani wa ushindi wa Argentina wa Kombe la dunia

    Filamu mpya ya BBC inaelezea hadithi ya ndani ya jinsi Lionel Messi hatimaye alivyoshinda Kombe la Dunia.

    Baada ya majaribio manne kufeli, hatimaye Messi alitwaa taji ambalo lilimponyoka kwa kuiongoza Argentina kushinda Qatar 2022.

    Katika filamu iliyochukua saa moja, BBC inachunguza mafanikio hayo kwa maoni kutoka kwa baadhi ya waliohusika - ikiwa ni pamoja na wachezaji Emiliano Martinez, Alexis Mac Allister na Julian Alvarez, na meneja Lionel Scaloni.

    Usiku usio na usingizi ulifuata kushindwa na Saudi Arabia

    Argentina waliingia katika mchuano huo kama moja ya vipendwa, na nyuma ya msururu wa michezo 36 bila kushindwa.

    Lakini kujiamini kwao kulitikiswa walipopoteza mchezo wao wa ufunguzi wa Kundi C kwa mabao 2-1 dhidi ya Saudi Arabia katika mojawapo ya majanga makubwa zaidi ya Kombe la Dunia.

    "Ulikuwa usiku mgumu zaidi maishani mwangu - sikuweza kulala," anakumbuka kipa Martinez."Niliogopa kutupwa nje ya Kombe langu la kwanza la Dunia."

    Mchezaji huyo wa Aston Villa, 30, analinganisha mchezo huo na mchezo wa ndondi ambapo mtu mmoja anapigwa nje."Hatukuweza kupigana," anasema.

    Kiungo wa kati wa Brighton Mac Allister alikuwa mmoja wa mastaa walioshangaza nchini Qatar - na ndiye aliyeongoza mchezaji bora wa BBC Sport wakati Argentina ilipoilaza Ufaransa kwa mikwaju ya penalti katika fainali.

    Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 24 alinawiri pamoja na Messi, Enzo Fernandez na Angel di Maria.

    "Ni kiungo kamili," anasema beki wa kulia wa zamani wa Argentina Pablo Zabaleta.

    Scaloni pia amejaza sifa nyingi kwa Mac Allister, akisema: "Alituonyesha kitu ambacho hatukujua juu yake - hahisi shinikizo.

    "Ni kama anacheza kwenye bustani yake."

    Wachezaji wa Argentina walijihisi wako nyumbani Qatar

    Scaloni alifanya kazi nzuri ya kutengeneza mazingira mazuri kwa wachezaji wake nchini Qatar - ikiwa ni pamoja na kuagiza starehe za nyumbani.

    Wakati huo,iliripotiwa kikosi kilikuwa na pauni 2,000 (kilo 900) za nyama iliyosafirishwa kutoka Amerika Kusini.

    "Kila kitu kilikuwa sawa," anasema Mac Allister."Ilikuwa kama nyumbani. Tulicheza karata na kunywa chai [ya kafeini ]... na hata kula nyama ya Argentina!"

    Zabaleta anasema mambo hayo matatu ni "kama dini" kwa Waajentina.

    Messi alikuwa 'mvulana mbaya ' dhidi ya Uholanzi

    Argentina walitinga robo fainali ambayo ilikuwa na kadi 18 za njano - mbili kati ya hizo zilisababisha kutolewa nje kwa mlinzi wa Uholanzi Denzel Dumfries.

    Baada ya kipenga cha mwisho, wachezaji wa Argentina waliwakejeli wapinzani wao, huku Martinez - ambaye aliokoa penalti mbili kwenye mikwaju iliyofuata sare ya 2-2 - akimzomea bosi wa Uholanzi Louis van Gaal.

    "Nilimsikia Van Gaal akisema kuwa katika mikwaju ya penalti walikuwa na faida," alisema baada ya mchezo huo."Nadhani anahitaji kufunga mdomo wake."

    Hata Messi ambaye kwa kawaida alikuwa mpole alipinga maoni kutoka kwa Van Gaal, ambaye alisema nahodha huyo wa Argentina "hakushiriki sana" wakati timu yake ilipopoteza mpira.

    Messi alipofunga wakati wa kawaida, alikimbia moja kwa moja hadi kwenye benchi ya Uholanzi na kuziba masikio yake.

    Sherehe hiyo, kama filamu inavyoeleza, ilitiwa msukumo na mchezaji mwenza wa zamani Juan Roman Riquelme, ambaye alihisi kutendewa vibaya na Van Gaal akiwa Barcelona.

    Lakini wengi walishangazwa na upande huu mpya kwa Messi.

    "Sisi ni wakali kuliko timu ya taifa aliyokuwa nayo hapo awali," anasema Martinez."Labda alikuwa anakuwa kama sisi - yule mvulana mbaya."

    Martinez ni kama 'mtoto uwanjani'

    Martinez alikuwa shujaa wa mikwaju ya penati wa Argentina kwa mara nyingine kwenye fainali huku La Albiceleste wakiwashinda mabingwa hao watetezi.

    Uchezaji wake ulivutia maoni mengi, alipotupa mpira mbali, akicheza, na kusherehekea mbele ya wachezaji wa Ufaransa.

    Akizungumzia densi alilofanya baada ya Aurelien Tchouameni kukosa penalti ya tatu ya Ufaransa, anasema: "Sijawahi kucheza jinsi nilivyocheza baada ya penalti ya pili ambayo walikosa. Kamwe maishani mwangu.

    "Huyo ni mimi. Mimi ni mtoto uwanjani. Sioni kitakachofuata."

    Unaweza pia kusoma

  9. Afisa wa India akausha bwawa lote ili kupata simu

    Afisa mmoja wa serikali nchini India amesimamishwa kazi baada ya kuamuru bwawa likaushwe maji ili apate simu yake iliyodondoka ndani ya bwawa hilo.

    Ilichukua siku tatu kusukuma mamilioni ya lita za maji kutoka kwenye bwawa hilo, baada ya Rajesh Vishwas kudondosha kifaa hicho alipokuwa akipiga picha ya selfi.

    Hadi ilipopatikana, simu hiyo ilikuwa imeingia maji sana kiasi kwamba haingeweza kufanya kazi tena.

    Bw Vishwas alidai ilikuwa na data nyeti za serikali na simu ilitakiwa kupatikana kurejeshwa, lakini ameshutumiwa kwa kutumia nafasi yake vibaya.

    Afisa huyo wa ukaguzi wavyakula alidondosha simu yake ya Samsung, yenye thamani ya takriban $1,200 (rupia 100,000), kwenye Bwawa la Kherkatta, katika jimbo la kati la India la Chhattisgarh, Jumapili.

    Baada ya wapiga mbizi wa eneo hilo kushindwa kuipata, alilipia garama ya kueltwa kwa pampu ya dizeli , Bw Vishwas alisema katika taarifa ya video iliyonukuliwa katika vyombo vya habari vya India.

    Alisema alikuwa na ruhusa ya mdomo kutoka kwa afisa kumwaga "baadhi ya maji ya bwawa hilo kwenye mfereji wa karibu", akiongeza kuwa afisa huyo alisema "kwa kwani kufanya hivyo kungenufaisha wakulima ambao watakuwa na maji zaidi".

    Pampu hiyo ilidumu kwa siku kadhaa, ikimwaga takriban lita milioni mbili (galoni 440,000) za maji – ambayo yaliripotiwa kuwa ya kutosha kumwagilia kilomita za mraba 6 (hekari 600) za mashamba.

  10. Vita vya Ukraine: Idara ya ujasusi ya Ukraine yaonya juu ya uwezekano wa uchokozi kuhusu kinu cha nyuklia cha Zaporozhye

    Kurugenzi Kuu ya Ujasusi ya Wizara ya Ulinzi ya Ukraine (GUR) Ijumaa jioni ilisema kwamba jeshi la Urusi linadaiwa kuandaa ''uchokozi mkubwa'' kwa kuiga ajali ya kinu cha nyuklia cha Zaporozhye ili kuzuia shambulio linalotarajiwa kutoka kwa jeshi la Ukraine.

    Kinu hicho cha nyuklia, kilicho katika sehemu iliyotwaliwa na Urusi katika eneo la Zaporozhye, ndicho kinu kikubwa zaidi cha nyuklia barani Ulaya, na eneo hilo limekuwa likipigwa makombora mara kwa mara, ambapo wahusika wanalaumiana, linasema shirika la habari la Reuters.

    Kulingana na ujasusi wa Ukraine, shambulio linaweza kupigwa moja kwa moja kwenye eneo la kinu cha nyuklia.

    "Madhumuni ya hatua hii ni kuichochea jumuiya ya kimataifa kufanya uchunguzi wa kina, ambapo uhasama wote utasitishwa," GUR ilisema katika taarifa yake kwa vyombo vya habari. Kwa hivyo, kulingana na ujasusi wa Ukraine, Urusi inatarajia "kupata muda wa kukaribishwa" ili kuutumia kupanga tena vikosi vyake kwa ajili ya mashambulio.

    Taarifa ya kurugenzi hiyo hatahivyo haitoi ushahidi wowote kuhusiana na madai hayo, linasema Shirika la habari la Reuters. Wakati huo huo, GUR pia inadai kwamba Urusi ilivuruga awamu ya mzunguko wa wakaguzi wa silaha wa Kimataifa la udhibiti wa silaha za maangamizi- IAEA ambao wako kwenye kituo hicho, iliyopangwa kufanyika Ijumaa. IAEA haiajasema iwapo kulikuwa na ukiukaji wa makubaliano.

    Wiki iliyopita mashuhuda waliripoti kwamba jeshi la Urusi lilikuwa likiimarisha vikosi vyake katika maeneo ya ulinzi yaliyopo karibu na kinu cha nyuklia cha Zaporozhye ikitarajia mashambulizi ya jeshi la Ukraine yanayotarajiwa, limeripoti shirika la habari la Reuters.

    Mashambulio ya Ukraine: Mengi zaidi

    • YA MSINGI:Mzozo wa Ukraine: Kwanini Urusi inaivamia Ukraine na Putin anataka nini?
    • UFAFANUZI:Mzozo wa Ukraine: Swift ni nini na kwa nini kuipiga marufuku Urusi ni muhimu sana?
    • UCHAMBUZI:Mzozo wa Ukraine: Putin humsikiliza nani?
    • KWENYE RAMANI:Uvamizi wa Ukraine: Shambulio la Urusi kwenye ramani
    • ZELENSKY:Volodymyr Zelensky: Mfahamu rais wa Ukraine aliyeacha umaarufu wake wa TV na kuingia kwenye siasa
    • PUTIN:Vladimir Putin: Rais wa Urusi aliyeagiza shambulio Ukraine
  11. Oleksiy Danilov: Mashambulizi ya Ukraine yako 'tayari kuanza'

    Ukraine iko tayari kuanzisha mashambulizi yake ya muda mrefu ya kukabiliana na majeshi ya Urusi, mmoja wa maafisa wakuu wa usalama nchini humo ameiambia BBC.

    Oleksiy Danilov hatataja tarehe lakini alisema shambulio la kutwaa tena eneo kutoka kwa vikosi vya uvamizi vya Rais Vladimir Putin linaweza kuanza "kesho, kesho kutwa au baada ya wiki moja".

    Alionya kwamba serikali ya Ukraine "haina haki ya kufanya makosa" juu ya uamuzi huo kwa sababu hii ilikuwa "fursa ya kihistoria" ambayo "hatuwezi kupoteza".

    Kama katibu wa Baraza la Usalama la Kitaifa na Ulinzi la Ukraine, Bw Danilov ndiye kiini cha baraza la mawaziri la vita la Rais Volodymyr Zelensky.

    Mahojiano ya nadra na BBC yalikatizwa na ujumbe wa simu kutoka kwa Rais Zelensky ukimuita kwenye mkutano kujadili hatua hiyo.

    Wakati wa mahojiano, alithibitisha pia kwamba baadhi ya askari mamluki wa kundi la Wagner walikua wakiondoka katika mji wa Bakhut , ambako kumekuwa na vita vya umwagaji damu zaidi hadi sasa - lakini aliongeza kuwa "wanajipanga tena katika maeneo mengine matatu.

    Mashambulio ya Ukraine: Mengi zaidi

    • YA MSINGI:Mzozo wa Ukraine: Kwanini Urusi inaivamia Ukraine na Putin anataka nini?
    • UFAFANUZI:Mzozo wa Ukraine: Swift ni nini na kwa nini kuipiga marufuku Urusi ni muhimu sana?
    • UCHAMBUZI:Mzozo wa Ukraine: Putin humsikiliza nani?
    • KWENYE RAMANI:Uvamizi wa Ukraine: Shambulio la Urusi kwenye ramani
    • ZELENSKY:Volodymyr Zelensky: Mfahamu rais wa Ukraine aliyeacha umaarufu wake wa TV na kuingia kwenye siasa
    • PUTIN:Vladimir Putin: Rais wa Urusi aliyeagiza shambulio Ukraine
  12. Hujambo na karibu kwa matangazo yetu ya moja kwa moja ya leo tarehe 27.05.2023