Vietnam yawakamata watu 65 kwa kusafirisha dawa za kulevya kwenye mirija ya dawa ya meno

Chanzo cha picha, Getty Images
Polisi wamewakamata watu 65 kwa kusafirisha kilo 50 za dawa za kulevya - zingine zikiwa zimefichwa kwenye mirija ya dawa za meno - hadi Vietnam.
Tukio hili Iinafuatia kukamatwa mwezi uliopita kwa wafanyakazi wanne wa shirika la ndege la Vietnam waliokutwa na mirija kwenye mifuko ya kubebea baada ya safari ya ndege kutoka Paris kuelekea Ho Chi Minh City.
Walisema waliajiriwa kusafirisha kilo 60 za dawa ya meno lakini hawakujua ni ecstasy, ketamine na cocaine.
Vietnam ni kitovu kikuu cha biashara ya dawa za kulevya licha ya kuwa na sheria kali zaidi za dawa za kulevya ulimwenguni.
Takriban nusu ya mirija 327 ya dawa za meno ambayo wahudumu wa ndege walikuwa wakisafirisha ilikuwa na dawa za kulevya.
Wachunguzi walisema wanawake hao hawakujua yaliyomo - kwa sasa wako nje kwa dhamana.
Polisi walisema wiki hii kwamba washukiwa hao 65 walikamatwa baada ya kugundua shehena nyingine sita za mihadarati zikisafirishwa kwenda Vietnam kupitia njia hiyo hiyo.
Inadaiwa walielekezwa na kisa hicho cha magendo ambacho kilikodi wahudumu wa ndege hiyo.
Washukiwa hao 65 wanachunguzwa kwa makosa mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kununua, kuuza, kusafirisha na kuhifadhi mihadarati, vyombo vya habari nchini viliripoti.
Polisi wanashuku kundi moja mara nyingi hutumia raia wa Vietnam wanaosoma na wanaoishi Ufaransa kuleta dawa za kulevya nchini humo.
Wale waliopatikana na hatia nchini Vietnam kwa kumiliki au kusafirisha zaidi ya gramu 600 za heroini au zaidi ya kilo 2.5 za methamphetamine wanakabiliwa na hukumu ya kifo.
Uzalishaji au uuzaji wa dawa za kulevya zaidi ya kiasi fulani pia huadhibiwa kwa kifo.
















