Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Urusi na Ukraine: Wanajeshi wa Urusi wauteka mji wa Svitlodarsk huko Donetsk

Vikosi vya Urusi vimeudhibiti mji wa Svitlodarsk katika wilaya ya Bakhmut katika eneo la Donetsk nchini Ukraine, kulingana na maafisa wa Ukraine na Jamhuri ya Watu wa Donetsk - eneo linaloshikiliwa na waasi mashariki mwa Ukraine, linaloundwa na watu wanaotaka kujitenga.

Moja kwa moja

  1. Dkt.Tedros achaguliwa tena kuwa mkuu wa WHO

    Tedros Adhanom Ghebreyesus wa Ethiopia amechaguliwa tena kuwa mkuu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) kwa muhula wa pili wa miaka mitano.

    Matokeo ya kura ya siri yalikuwa ni utaratibu kwa vile alikuwa mgombea pekee.

    Akifungua Mkutano wa 75 wa Afya Ulimwenguni huko Geneva, Dk Tedros, ambaye ameongoza mwitikio wa ulimwengu dhidi ya janga la Covid, alisema virusi vya corona vimeubadili ulimwengu, na kuwaacha wengi bado wanateseka.

    Akiyazuia machozi alipokuwa akizungumza, pia alitoa wito wa kukomeshwa kwa vita, ambayo alisema "inatikisa na kuvunja misingi ambayo jamii ziliisimamia".

    Alikumbuka uzoefu wake wa kwanza kama mtoto wa vita nchini Ethiopia, ambayo inakabiliwa tena na migogoro ya wenyewe kwa wenyewe katika eneo lake la kaskazini la Tigray, ambako ni asili yake.

    Mkuu huyo mwenye umri wa miaka 57 amekuwa katika mzozo na serikali ya Ethiopia baada ya kumshutumu kwa kuunga mkono vikosi vya Tigray - tuhuma ambayo ameikanusha hapo awali.

    Alikuwa Waziri wa Afya wa Ethiopia - ambapo alipokea sifa kwa juhudi zake za kudhibiti magonjwa kama vile malaria na VVU/UKIMWI - na waziri wa mambo ya nje kabla ya kuchaguliwa kwa mara ya kwanza kuongoza WHO mwaka 2017.

    • Umakini kwa Ukraine unaonesha upendeleo kwa watu weupe dhidi ya weusi, Mkuu wa WHO asema
    • Wanawake waliolipa gharama ya vita vya wenyewe kwa wenyewe vya Ethiopia
  2. Ukraine yatumiwa makombora ya kuzuia mashambulizi

    Ukraine inatumiwa silaha za hali ya juu zaidi ambazo zitaongeza safu yake ya mashambulizi kwa mara ya kwanza tangu vita hivyo kuanza, baada ya Denmark kuahidi makombora ya kukinga meli ya Harpoon yaliyotengenezwa na Marekani.

    Silaha hizo zinaweza kutumika kusukuma jeshi la wanamaji la Urusi mbali na bandari za Bahari Nyeusi, kuruhusu mauzo ya nafaka na bidhaa za kilimo kuanza tena.

    Ukraine imekuwa ikiomba silaha za hali ya juu zaidi kama vile za ulinzi wa anga, makombora ya kukinga meli na roketi za masafa marefu, lakini hadi sasa misaada mingi imekuwa katika mifumo ya masafa mafupi kama vile silaha za kivita za mizinga.

    Waziri wa Ulinzi wa Marekani Lloyd Austin alisema "anaishukuru sana" Denmark kwa kusambaza silaha "kuisaidia Ukraine kulinda pwani yake".

    Nchi nyingine kadhaa zilikuwa tayari kutuma silaha aina ya Harpoon nchini Ukraine, maafisa wa Marekani na vyanzo vya bunge vimesema, na kuongeza kuwa hakuna taifa lililotaka kuwa taifa la kwanza au la pekee kutuma Harpoons, wakihofia kulipizwa kisasi na Urusi ikiwa meli itazama.

    • Olena Zelenska: Mke wa Rais wa Ukraine aeleza alichofanya mumewe asubuhi ya kwanza Urusi ilipoivamia Ukraine
    • Vita vya Ukraine: Nini kinaweza kuleta usawa katika vita hivi?
  3. Habari za hivi punde, Wanajeshi wa Urusi wauteka mji wa Svitlodarsk huko Donetsk

    Vikosi vya Urusi vimeudhibiti mji wa Svitlodarsk katika wilaya ya Bakhmut katika eneo la Donetsk nchini Ukraine, kulingana na maafisa wa Ukraine na Jamhuri ya Watu wa Donetsk - eneo linaloshikiliwa na waasi mashariki mwa Ukraine, linaloundwa na watu wanaotaka kujitenga.

    Jeshi la Urusi liliingia mjini humo mapema leo asubuhi, mkuu wa utawala wa kijeshi wa Svetlodar wa Ukraine, Sergei Goshko, alikiambia kituo cha redio cha Ukraine.

    "Kwa sasa wanapeperusha bendera yao juu ya jengo la utawala," Goshko alisema, akimaanisha bendera ya Urusi.

    Kabla ya vita kuanza, Svitlodarsk ilikuwa na idadi ya watu 11,000.

  4. Kenya na Zimbabwe zapigwa 'kufuli' kushiriki AFCON 2023

    Zimbabwe na Kenya hazitashiriki Kombe la Mataifa ya Afrika 2023, Shirikisho la Soka la Afrika (CAF) limetangaza.

    Mataifa yote mawili hayatashiriki mechi za kufuzu michuano hiyo mwezi ujao kwa sababu ya marufuku yao ya kutoshiriki soka la kimataifa, iliyotolewa na Fifa kwa sababu ya serikali kuingilia shughuli za uendeshaji wa soka katika nchi hizo.

    "CAF iliziweka [Kenya na Zimbabwe] katika droo rasmi mapema Aprili 2022 kwa sharti kwamba adhabu hiyo ( ya FIFA)iondolewe wiki mbili kabla ya mechi yao ya kwanza," ilisema taarifa ya Caf.

    FIFA haijaziondolea marufuku nchi hizo.

    Harambee Stars, ambayo mechi yao ya hivi majuzi zaidi ya Kombe la Mataifa ya Afrika ilikuwa mwaka wa 2019, ilikuwa icheze na Cameroon Juni 4 huku Zimbabwe, ambao wamekuwepo kwenye fainali tatu zilizopita, wakipangiwa kuwa mwenyeji wa Liberia siku tano baadaye.

    Ina maana kuwa Kundi C ambalo Kenya ilikuwa imepangwa, sasa itaziacha Cameroon, Namibia na Burundi huku Kundi K la Zimbabwe likiwa limebaki na mataifa ya Morocco, Afrika Kusini na Liberia pekee. Timu mbili za juu zitasonga mbele.

    Marufuku hiyo iliyowekwa na Fifa mwezi Februari ilikuja baada ya serikali za nchi zote mbili kuingilia kati kufuta mashirikisho yao.

    Kenya ilishiriki mmara sita michuano ya AFCON wakati Zimbabwe ameshiriki fainali hizo mara tano.

  5. Kurt Zouma: Beki wa West Ham akiri kosa la kumpiga paka wake

    Beki wa West Ham United Kurt Zouma amekiri kosa la kumpiga teke na kumpiga paka wake kwenye video ambayo pia ilimuonesha akisema "Naapa nitamuua".

    Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 27 alikiri makosa mawili chini ya Sheria ya Ustawi wa Wanyama katika katika Mahakama ya Thames.

    Kaka yake Zouma Yoan, anayechezea Dagenham na Redbridge, alikiri kosa moja baada ya uchunguzi wa RSPCA. Yoan, 24, alirekodi tukio hilo, ambalo lilichapishwa kwenye mitandao ya kijamii.

    Kesi imeahirishwa hadi Juni 1. Anwani za ndugu hao zilizuiwa kufuatia agizo la mahakama.

    Mahakama ilielezwa kuhusu picha za video za kutatanisha za tukio hilo, ambazo zilinakiliwa nyumbani kwa mchezaji huyo wa West Ham na kuchapishwa kwenye Snapchat na emoji za 'kucheka' na kaka yake tarehe 6 Februari.

    Zouma alionekana akimzungusha paka huyo, kabla ya kumrushia jozi ya viatu na kumpiga kichwani.

  6. Kiongozi wa upinzani nchini Urusi aliyefungwa jela amuita Putin 'mwendawazimu'

    Kiongozi wa upinzani wa Urusi aliyefungwa jela Alexei Navalny amemlaani Rais Vladimir Putin katika kikao cha moja kwa moja cha mahakama, akimtaja kuwa "mwendawazimu" aliyeanzisha "vita vya kijinga" nchini Ukraine.

    "Hii ni vita ya kijinga ambayo Putin wenu alianzisha," Navalny aliiambia mahakama ya rufaa huko Moscow kupitia kiungo cha video kutoka kwa kituo cha kutoa adhabu.

    "Vita hivi vilianzishwa kwa kutumia uwongo. Mwendawazimu mmoja ameingiza kucha zake Ukraine na sijui anataka kufanya nini nazo - mwizi huyu kichaa," Navalny alisema kuhusu Putin.

    Hapo awali Navalny alihukumiwa na mahakama miaka tisa katika koloni kali ya utawala kwa udanganyifu na kudharau mahakama.

    Ikulu ya Kremlin imetupilia mbali shutuma za Navalny kuhusu Putin, ambaye inasema ameshinda chaguzi nyingi za haki nchini Urusi tangu mwaka 2000 na anasalia kuwa mwanasiasa maarufu zaidi nchini humo.

  7. Noussair Mazaroui: Bayern Munich wamsajili beki wa Morocco kutoka Ajax

    Mlinzi wa timu ya taifa ya Morocco, Noussair Mazraoui amejiunga na mabingwa wa Ujerumani Bayern Munich kutoka Ajax ya Uholanzi kwa uhamisho huru.

    Mkataba huo ulikuwa umeripotiwa sana katika miezi ya hivi karibuni huku kandarasi ya mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 24 na Ajax ikitarajiwa kukamilika mwezi Juni.

    Ametia saini mkataba wa miaka minne na Bayern hadi 30 Juni 2026, na ataungana na wachezaji wenzake wapya kwa ajili ya mazoezi ya kujiandaa na msimu mpya Julai.

    "Nilikuwa na hisia nzuri tangu mazungumzo ya kwanza na nina furaha kuhamia moja ya klabu kubwa barani Ulaya," Mazraoui aliiambia tovuti ya Bayern Munich.

    "Bayern ndio wametoka kuwa mabingwa wa Ujerumani kwa mara ya 10 mfululizo na pia watakuwa miongoni mwa washindani wa kushinda Ligi ya Mabingwa tena mwaka ujao. Nilichagua klabu hii kwa sababu ninaweza kushinda mataji makubwa zaidi hapa."

    Mtendaji mkuu wa Bayern Munich Oliver Khan pia anatumai raia huyo wa Morocco anaweza kuisaidia klabu hiyo ya Bundesliga kuongeza fedha zaidi. "Noussair ndiye kizuizi kinachofuata tunapoendelea kuimarisha timu yetu ," mlinda mlango huyo wa zamani wa Ujerumani aliiambia tovuti ya klabu.

  8. Ukraine inasema kwamba 'wezi wa Urusi' wanaiba nafaka yao na kuiuza ughaibuni

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Ukraine, Dmytro Kuleba, anadai kwamba "wezi wa Urusi" wanaiba nafaka ya Ukraine ili kuziuza nje ya nchi, akisema nafaka inapakiwa kwenye meli, ambazo zitapitia Bosphorus – mkondo mwembamba ambao unagawanya pande za Ulaya na bara Asia – ili kuuzwa nje ..

    "Ninatoa wito kwa majimbo yote kuwa macho na kukataa mapendekezo yoyote kama hayo. Msinunue vilivyoibiwa. Msiwe washiriki wa uhalifu wa Urusi," Kuleba alisema kwenye Twitter.

    BBC haijathibitisha madai hayo. Urusi mnamo Jumanne ilipuuza picha za "bandia" zinazoonyesha meli zikiwa zimejaa nafaka huko Crimea.

    Wakati huohuo Rais wa Tume ya Umoja wa Ulaya, Ursula von der Leyen, aliishutumu Urusi kwa kutumia chakula kama silaha katika vita vya Ukraine, akiongeza kuwa ilikuwa ikitwaa nafaka na kuzijaza katika meli kwenye maeneo inayoyadhibiti.

    Alisema madhara tayari yanaonekana katika kuongezeka kwa bei ya chakula, mbolea na nishati duniani - na kusababisha mateso zaidi kwa wale wanaohitaji zaidi.

  9. Mwanamke mjamzito na watoto wake wanne wauawa katika shambulio Nigeria

    Polisi nchini Nigeria wanasema wanawasaka watu wenye silaha walioua takriban watu 12, akiwemo mwanamke mjamzito na watoto wake wanne, katika jimbo la kusini-mashariki la Anambra.

    Polisi wamelaumu ghasia zinazoongezeka katika eneo hilo kwa watu wanaotaka kujitenga kwa Biafra.

    Kiongozi wa jamii aliiambia BBC kwamba mwanamke huyo mjamzito na watoto wake walikuwa wakirejea nyumbani kwa pikipiki wakati watu wenye silaha walipowavizia katika eneo la Orumba.

    Watu wengine kadhaa pia waliuawa kwa kupigwa risasi katika matukio tofauti Jumapili jioni.

    Polisi wanasema wanachunguza. Mauaji hayo yamezua hasira kwenye mitandao ya kijamii.

    Zilitokea siku moja baada ya miili iliyoharibika ya mwanasiasa wa eneo hilo na msaidizi wake kugunduliwa wiki moja baada ya kutekwa nyara.

    Ghasia zinazozidi kuwa mbaya kusini-mashariki mwa Nigeria zinalaumiwa kwa kundi lililopigwa marufuku la kujitenga - the Indigenous People of Biafra - ambalo linafanya kampeni kwa ajili ya jimbo lililojitenga katika eneo hilo.

    Kundi hilo limekanusha kuhusika na baadhi ya mashambulizi hayo. Vikosi vya usalama pia vinakabiliana na makundi mbalimbali yenye silaha yanayotekeleza mauaji na utekaji nyara katika maeneo mengine ya Nigeria.

    Kaskazini-mashariki mwa nchi hiyo, zaidi ya watu 30 waliripotiwa kuuawa au kutekwa nyara katika shambulio lililotokea katika jimbo la Borno Jumapili iliyopita.

    Wanamgambo wa Boko Haram na kundi lenye uhusiano na IS wanafanya kazi katika eneo hilo. Ukosefu wa usalama ulioenea ni wasiwasi mkubwa kabla ya uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Februari mwaka ujao.

    • Mwaka mmoja baada ya kifo cha Abubakar Shekau: Mashambulizi 12 mabaya zaidi ya Boko Haram nchini Nigeria ambayo hayatasahaulika.
    • Efuoma Amos: 'Kila nikimwangalia mke wangu nabubujikwa na machozi'
  10. Marekani yaonya Makampuni dhidi ya kufanya biashara Sudan

    Marekani imetoa onyo kwa makampuni ya Marekani na watu binafsi kufanya biashara na makampuni ya Sudan yanayomilikiwa na serikali na kudhibitiwa kijeshi.

    Ilisema kuna hatari ya kuharibu sifa zao kwa kufanya biashara na makampuni haya huku kukiwa na kuzorota kwa hali ya haki za binadamu nchini Sudan.

    Wizara ya Mambo ya Nje ilisema kwamba ingawa baadhi ya hatari hizo zilikuwepo kabla ya mapinduzi ya Oktoba mwaka jana, jeshi kuchukua mamlaka na hatua walizochukua zilifanya hali kuwa mbaya zaidi.

    "Hatari hizi zimekuja kutokana na hatua za hivi karibuni zilizofanywa na Baraza Kuu la Sudan na vikosi vya usalama chini ya amri ya jeshi, ikiwa ni pamoja na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu dhidi ya waandamanaji," Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje Ned Price alisema katika taarifa.

    Bw Price alisema serikali ya Marekani imebaki na nia ya kuunga mkono azma ya watu wa Sudan ya serikali ya mpito ya kiraia inayoongozwa na raia kuelekea serikali itakayochaguliwa.

    • Mambo matano usiyoyajua kuhusu Sudan Kusini
    • Waandamanaji walioapa kupigania uhuru wao Sudan
    • Sudan: Je mapinduzi ya kijeshi yanaongezeka Afrika?
  11. Urusi inalenga kukuza zaidi uhusiano wake na China- Lavrov

    Waziri wa mambo ya nje wa Urusi amesema kuwa Moscow itaangalia pendekezo la kutoka nchi za Magharibi ili kuanzisha tena uhusiano, lakini kwa sasa itazingatia zaidi kuendeleza uhusiano wake na China.

    Sergei Lavrov alishutumu nchi za Magharibi kwa kuunga mkono "Russophobia" tangu Moscow ilipoanzisha "operesheni yake maalum ya kijeshi" nchini Ukraine, ambavyo ni namna Kremlin inavyofafanua uvamizi wake.

    "Ikiwa [Magharibi] wanataka kutoa kitu katika suala la kuanzisha tena uhusiano, basi tutazingatia kwa umakini ikiwa tutaihitaji au la," Lavrov alisema katika hafla, kwa mujibu wa maelezo yaliyo kwenye tovuti ya wizara ya mambo ya nje jana usiku.

    Urusi "lazima iache kutegemea kwa njia yoyote ile vifaa" vinavyotoka Magharibi, aliongeza. Lengo la Moscow sasa ni kuendeleza uhusiano na China, alisema.

    Urusi ingependa kutegemea "sisi wenyewe tu na kwa nchi ambazo zimejidhihirisha kuwa zinaaminika na 'hazichezi muziki wa waimbaji wengine'", alisema.

    "Ikiwa nchi za Magharibi zitabadilisha mawazo yao na kupendekeza aina fulani ya ushirikiano, basi tunaweza kuamua."

    • Urusi na Ukraine: Uhusiano wa kiuchumi kati ya Urusi na China una jukumu gani katika vita ?
    • Je Taiwan inaweza kujitetea katika vita dhidi ya China?
    • Kwa nini China pia inaiona NATO kuwa tishio na inahofia kwamba itafikia mipaka yake?
  12. 'Mauzo ya Chelsea 'bado yana vikwazo vikubwa kuvishinda'

    Serikali ya Uingereza iko tayari kuidhinisha mauzo ya Chelsea ya £4.25bn ndani ya saa 24 zijazo, BBC Sport imebaini.

    Hata hivyo, mpango huo "bado una vikwazo vikubwa vya kuvishinda" kwa mujibu wa chanzo cha ndani cha Whitehall.

    Inafahamika kwamba, kwa sababu mmiliki Roman Abramovich ana pasipoti ya Ureno, uuzwaji huo unahitaji kupewa leseni na mamlaka katika nchi hiyo pia.

    Mawaziri sasa wanasemekana kuwa katika "majadiliano makali" na wenzao katika Tume ya Ulaya ili kuwahakikishia wanaohitaji kuidhinisha mpango huo.

    Chelsea wamekubaliana kuhusu mkataba unaofadhiliwa na mashirika ya kibinafsi unaoongozwa na mwekezaji wa Marekani Todd Boehly, mmiliki mwenza wa timu ya besiboli ya LA Dodgers.

    Klabu hiyo iliuzwa kabla ya mmiliki Abramovich kuwekewa vikwazo kwa madai ya kuwa na uhusiano na rais wa Urusi Vladimir Putin kufuatia uvamizi wa Ukraine.

    Kisha serikali ilitoa leseni maalum kwa Chelsea kuendelea kufanya kazi, ambayo itaisha tarehe 31 Mei.

    Wiki iliyopita BBC iligundua kuwa serikali ilikuwa na wasiwasi kwamba mpango huo unaweza kuwa katika hatari ya "kusambaratika" kutokana na kukosekana kwa maelewano na klabu kuhusu mapato ya mauzo yoyote.

    "Kila mtu anataka kufanikisha mpango huo, lakini kutokana na hali ngumu ya mkataba na muundo wa umiliki wa Chelsea, hakuna kitu rahisi," kilisema chanzo cha Whitehall.

    "Muda unaenda kwa kasi, mpango huu lazima ukamilike mwishoni mwa Jumanne, vinginevyo klabu itakuwa hatarini."

    • Roman Abramovich awekewa vikwazo na Uingereza
    • Roman Abramovich anasema ana mpango wa kuiuza klabu hiyo
    • Mzozo wa Ukraine: Ni vikwazo gani vilivyowekwa dhidi ya Urusi?
  13. Tajiri wa Misri afungwa jela kwa kuwanyanyasa kingono yatima kwenye kituo chake.

    Mahakama nchini Misri imemhukumu tajiri mmoja na mfanyabiashara mkubwa aliyekuwa na uhusiano wa karibu na serikali kifungo cha miaka mitatu jela kwa kuhusika katika biashara haramu ya kusafirisha binadamu na shambulio la aibu kwa wasichana wenye umri mdogo katika kituo cha watoto yatima alichoanzisha.

    Mohamed El-Amin - ambaye alikuwa anamiliki vyombo vingi vya habari vyenye ushawishi mkubwa, alikamatwa mapema mwaka huu baada ya madai ya unyanyasaji wa kingono katika kituo hicho cha watoto yatima kuwekwa hadharani na shirika la misaada ya kibinadamu liitwalo Missing Children.

    Mwendesha mashtaka wa serikali alisema kuwa alitumia mamlaka yake na mazingira magumu ya wasichana hao.

    Mamlaka ilifunga kituo hicho cha watoto yatima mwishoni mwa mwaka jana baada ya madai dhidi ya el-Amin kuibuka. Alikamatwa Januari na tangu wakati huo amekuwa gerezani.

    El-Amin anaweza kukata rufaa dhidi ya hukumu hiyo.

    • Wanawake wananyanyaswa zaidi Misri
    • Ni uhalifu kuwanyanyasa wanawake Misri
  14. Rwanda yasema mashambulio ya DR Congo yamewajeruhi raia wake

    Jeshi la Rwanda linasema watu kadhaa wamejeruhiwa katika mashambulio kati yao na wenzao wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

    Rwanda inasema ilikuwa imeomba timu ya kikanda ya waangalizi wa kijeshi, Utaratibu wa Uthibitishaji wa Pamoja wa upanuzi, ili kufanya uchunguzi wa haraka.

    Taharuki kati ya nchi hizo mbili imeongezeka tangu mwezi Machi, wakati waasi wa kundi la M23 rebel waliposhambulia ngome za jeshi la Congo.

    Rwanda inakanusha madai kwamba inaunga mkono waasi hao.

    Kundi hilo liliteka eneo la mashariki mwa DR Congo wakati wa uasi mwaka 2012 na 2013, kabla ya wapiganaji wake kufukuzwa na vikosi vya Congo na Umoja wa Mataifa.

    Familia nyingi zimeacha makazi yao katika jimbo la Kivu Kaskazini-DRC nchini DR Congo, kuelekea mji wa mpakani wa Uganda wa Bunagana.

    Mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi nchini Uganda, Joel Boutroue, aliambia BBC kwamba maelfu ya wakimbizi waliwasili Uganda siku ya Jumatatu.

  15. Waafrika Kusini wananunua bia zaidi kuliko vinywaji laini

    Bia nchini Afrika Kusini zinatajwa kuuzwa kwa wingi kuliko vinywaji baridi visivyo na vileo hii ni kwa mujibu wa wachambuzi wa data za watumiaji katika kampuni ya NielsenIQ SA.

    "Tumefuatilia mauzo katika maduka zaidi ya 150,000... iwe ni maduka rasmi, migahawa, vioski," msemaji aliambia shirika la habari la eNCA.

    Ripoti ya Kampuni hiyo inasema mauzo ya bia nchini Afrika Kusini yamepanda kwa 8% katika kipindi cha miezi 12 iliyopita.

    Alipoulizwa kuelezea ongezeko hilo, Jon-Jon Emary wa NielsenIQ SA alisema "ukuaji mkubwa" umekuja "kufuatia marufuku mfululizo tulizoona wakati na baada ya sheria ya kutotoka nje tuliyokuwa nayo 2020".

    • Afrika Kusini imeondoa marufuku ya uuzwaji wa pombe
    • Rais Ramaphosa asema mlipuko wa virusi utakuwa mbaya zaidi
  16. Mwanadiplomasia wa Urusi ajiuzulu kutokana na vita nchini Ukraine

    Mwanadiplomasia wa Urusi ameacha kazi kupinga vita vya "umwagaji damu, visivyo na msingi" "vilivyoanzishwa na Putin dhidi ya Ukraine".

    Boris Bondarev, ambaye LinkedIn inasema alifanya kazi katika ubalozi wa Urusi katika Umoja wa Mataifa huko Geneva, aliiambia BBC kuwa alijua uamuzi wake huenda ukamaanisha kwamba Kremlin sasa inamwona kama msaliti.

    Lakini alisimama na kauli yake iliyoeleza vita hivyo kuwa ni "uhalifu dhidi ya watu wa Ukraine" na "watu wa Urusi".

    Moscow bado haijatoa tamko lolote.

    Urusi imekabiliana na wale wanaokosoa au kujiepusha na masimulizi rasmi kuhusu vita hivyo, ambayo inayataja tu kama "operesheni maalum ya kijeshi".

    Katika barua hiyo iliyotumwa kwenye mitandao ya kijamii na kushirikishwa na wanadiplomasia wenzake, Bw Bondarev alieleza kuwa amechagua kukatisha maisha yake ya utumishi kwa miaka 20 kwa sababu hangeweza "kushiriki tena katika aibu hii ya umwagaji damu, ya kipumbavu na isiyo na maana".

    "Wale ambao walianzisha vita hivi wanataka kitu kimoja tu - kusalia madarakani milele," aliandika.

    • YA MSINGI:Mzozo wa Ukraine: Kwanini Urusi inaivamia Ukraine na Putin anataka nini?
    • UFAFANUZI:Mzozo wa Ukraine: Swift ni nini na kwa nini kuipiga marufuku Urusi ni muhimu sana?
    • UCHAMBUZI:Mzozo wa Ukraine: Putin humsikiliza nani?
    • KWENYE RAMANI:Uvamizi wa Ukraine: Shambulio la Urusi kwenye ramani
    • ZELENSKY:Volodymyr Zelensky: Mfahamu rais wa Ukraine aliyeacha umaarufu wake wa TV na kuingia kwenye siasa
    • PUTIN:Vladimir Putin: Rais wa Urusi aliyeagiza shambulio Ukraine
  17. Samia Suluhu Hassan atajwa kwenye orodha ya watu wenye ushawishi mkubwa duniani

    Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ametajwa katika orodha ya viongozi 100 wenye ushawishi mkubwa duniani., kwa mujibu wa jarida la TIME 100.

    Kwa mujibu wa TIME 100 Rais Samia ametajwa katika orodha hii kutokana na uongozi wake wa kusisimua tangu alipoingia madarakani Machi 2021 na kuleta mabadiliko makubwa kwa nchi ya Tanzania ikiwemo kufungua mlango wa mazungumzo kati ya wapinzani wa kisiasa, hatua zimechukuliwa ili kujenga upya imani katika mfumo wa kidemokrasia, juhudi za kuongeza uhuru wa vyombo vya habari na amekuwa mfano wa kuigwa na wanawake na wasichana wengi.

    Mnamo Septemba 2021, miezi michache ya urais wake, Suluhu Hassan alitoa hotuba ya kihistoria kama kiongozi mwanamke wa tano pekee wa Kiafrika aliyewahi kuhutubia mkutano mkuu wa Baraza la Umoja wa Mataifa.

    "Kama Rais wa kwanza mwanamke katika historia ya nchi yangu," alisema, "mzigo wa matarajio ya kuleta usawa wa kijinsia ni mzito zaidi kwenye mabega yangu."

    Rais Samia ameungana na marais kutoka nchi nyingine katika orodha hiyo wakiwemo Volodymir Zelenskyy wa Ukraine, Xi Jinping wa China, Vladimir Putini wa Urusi na Joe Biden wa Marekani

    • Tanzania kuhudhuria Kikao cha Umoja wa Mataifa kuna tafsiri gani?
    • Jinsi Tanzania ilivyorudi katika ulimwengu wa diplomasia
    • Ni upi mustakabali wa ‘wanasiasa pendwa’ wa awamu ya tano Tanzania?
    • Rais wa Tanzania Samia Suluhu akutana na Tundu Lissu Brussels
  18. Ukraine kupokea makombora mapya na vinu vya kufyatulia silaha

    Nchi kadhaa za Magharibi kutoa silaha mpya kwa Ukraine, ikiwemo, helikopta za mashambulizi, vifaru na mifumo ya makombora

    Itapokea makombora ya kujikinga kwenye meli ya Kimarekani kutoka Denmark, na silaha nyingine kutoka nchi nyingine 20.

    Hayo yamesemwa na Waziri wa Ulinzi wa Marekani Lloyd Austin kufuatia mkutano wa Kikundi cha Ushauri kuhusu Usaidizi kwa Ukraine.

    "Ninaishukuru sana Denmark kwa kutangaza kwamba itaipatia Ukraine vifaa vya kufyatua vinu na makombora ili kusaidia kulinda pwani," alisema.

    Makombora ya kupambana na meli ya Marekani yana umbali wa kilomita 124-220. Kulingana na marekebisho, wanaweza kuzinduliwa kutoka kwa meli, manowari, ndege, mitambo ya pwani. Kasi ya kukimbia ya kombora hufikia 240 m / s.

    Je, nchi nyingine zitatoa msaada gani?

    "Pia ninashukuru kwa msaada muhimu wa Jamhuri ya Czech, ambayo hivi karibuni imetoa helikopta za mashambulizi, vifaru na mifumo ya makombora," Waziri wa Ulinzi wa Marekani alisema.

    "Nchi kadhaa zimetangaza kwamba zitasaidia kwa mifumo muhimu ya mizinga na makombora," aliongeza.

    Hasa, Italia, Ugiriki, Norway na Poland itasaidia na silaha.

    “Pia niipongeze Uingereza kwa uongozi na usaidizi wake katika kuratibu usaidizi wa usalama na kwa kiasi kikubwa cha vifaa vya ulinzi vinavyoendelea kumiminika nchini Ukraine,” alisema Lloyd Austin.

    Kulingana na yeye, jumla ya nchi zaidi ya 20 zimetangaza vifurushi vipya vya usaidizi wa kiulinzi, ambavyo vitajumuisha mizinga, makombora, mifumo ya ulinzi ya pwani, mizinga, magari ya kivita, na baadhi ya nchi zimeahidi kusaidia kutoa mafunzo kwa wanajeshi wa Ukraine.

    Waziri wa Ulinzi wa Marekani ameahidi kuwa wanachama wa muungano huo wataongeza uratibu wa kuimarisha na kukifanya Kikosi cha Wanajeshi cha Ukraine kuwa cha kisasa.

    "Kila mtu hapa anaelewa umuhimu wa vita hivi, wanaenda mbali zaidi ya Uropa," Lloyd Austin alisema.