Rais Samia: Ziara zangu za kigeni zinazaa matunda
Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ametetea ziara zake nje ya taifa hilo tangu alipochukua madaraka mwezi Machi akisema kwamba ziara hizo zimekuwa zikiwafaidi Watanzania.
Kulingana na gazeti la The Citizen Online, Rais Samia ametaja ziara yake nchini Kenya mnamo mwezi Mei akisema kwamba imeimarisha biashara kati ya nchi hizo mbili.
Rais Samia alisema hayo nchini Tanzania wakati akihutubia mkusanyiko wa watu mjini Arusha ikiwa miongoni mwa ziara zake za kikazi katika eneo hilo.
Kwa mujibu wa gazeti la The Citizen Tanzania, Samia ambaye alichukua mamlaka kutoka kwa mtangulizi wake John Pombe Magufuli mnamo tarehe 19 Machi mwaka huu kufuatia kifo cha Magufuli tarehe 17 mwezi Machi , alisafiri nchini Uganda mwezi Aprili ambapo alikutana na mwenzake wa taifa hilo Yoweri Mjuseveni pamoja na washikadau wengine katika mradi wa bomba la Mafuta.
Mwezi Mei , alifanya ziara ya siku mbili nchini Kenya ambapo yeye na mwenzake wa Kenya rais Uhuru Kenyatta walizungumzia kuimarisha biashara kati ya mataifa hayo mawili.
Mwezi huohuo, alifanya ziara ya siku moja nchini Uganda ili kuhudhuria sherehe ya kuapishwa kwa rais Museveni kufuatia ushindi wake katika uchaguzi mkuu wa Uganda wa 2021.
Mnamo mwezi Juni Rais Samia alielekea katika mji mkuu wa Msumbiji , Maputo kwa mkutano wa viongozi wa SADC ambapo walizungumzia kuhusu masuala ya ushirikiano na maendeleo.
Mwezi Julai alielekea Burundi kuimarisha biashara kati ya mataifa hayo mawili. Mwezi Agosti alisafiri nchini Rwanda.
Mwezi huohuo pia alielekea nchini Malawi ambapo alishiriki mkutano wa 41 wa SADC.
Baadaye akaelekea Zambia kuhudhuria kuapishwa kwa rais Hakainde Hichilema baada ya kiongozi huyo kuibuka mshindi wa uchaguzimkuu.
Mwezi Septemba , rais Samia alihudhuria mkutano wa 76 wa baraza la Umoja wa mataifa {Unga} mjini New York.
‘’Naambiwa kwamba kiwango cha biashara katika mpaka wa Namangaimeongezeka mara sita’’, alisema.
Kulingana na EAC , bishara ambazo tanzania inauza Kenya zimefikia $167m katika kipindi cha miezi sita kufikia mwezi Juni mwaka huu.