Tokyo 2020: Mtu wa pili wa timu ya Olimpiki ya Uganda athibitishwa kuwa na corona Japani
Raia wa pili wa timu ya Uganda amethibitishwa kuwa na virusi vya corona nchini Japani, siku tatu baada ya raia mwingine wa nchi hiyo hiyo kuthibitishwa kuwa na virusi hivyo baada ya kuwasili tu nchini humo kwa ajili ya michezo ya Olimpiki itakayofanyika mwezi ujao.
Michezo ya Olimpiki iliahirishwa kwa mara ya kwanza katika historia mwaka jana kwsababu ya janga hilo lakini imepangiwa kuanza Julai 2 licha ya kuibuka kwa wimbi jingine la virusi hivyo nchini Japani.
Uganda, ambayo imekuwa ikishuhudia kuongezeka kwa maambukizi siku za hivi karibuni, imetuma kikosi cha watu 9 katika mashindano hayo ambao wote wamepata chanjo.
"Mtu wa pili wa timu yetu Uganda amethibitishwa kuwa na virusi vya corona," Kamati ya Olimpiki ya Uganda imesema kupitia taarifa iliyotoa.
"Mwanariadha huyo haoneshi dalili za moja kwa moja na anafuatiliwa kwa karibu na mamlaka ya afya katika mji wa Izumisano. Wengine katika timu wako sawa na wanaendelea kuzoea hali ilivyo katika mji wa Izumisano."
Wajumbe wote wa Uganda waliokwenda kwenye mashindano hayo ikiwa ni pamoja na wanamasumbwi, mwogeleaji na mnyanyuaji uzani walithibitishwa kutokuwa na virusi hivyo kabla ya kuondoka nchini Uganda wiki jana.
Hata hivyo, Patrick Lihanda alithibitishwa kuwa na virusi vya corona baada tu ya kuwasili uwanja wa ndege wa kimataifa wa Tokyo huko Narita Jumamosi, na aliwekwa karantini katika kituo kilichotengwa na serikali, maafisa wa Japani walinikuliwa na vyombo vya habari.
Kuendelea kuthibitishwa kwa maambukizi ya virusi vya corona kutazua maswali zaidi kuhusu ikiwa michezo hiyo ya Olimpiki inastahili kuendelea huko Japani ambako wenyeji wengi wanapinga wazo hilo.
Hata hivyo, mafisa husika wamekataa kuahirisha tena michezo hiyo ambayo inatarajiwa kuanza Julai 23 hadi Agosti 8, wakisema kwamba watakuwa salama wa salmin.
Uganda imekuwa na ongezeko la maambukizi ya virusi vya corona tangu mwanzoni mwa mwezi Juni, huku idadi ya watu wanaothibitishwa kuwa na virusi hivyo ikiongezeka kutoka chini ya 100 hadi zaidi ya 1,700.
Wajumbe kutoka Afrika ndio waliokuwa kundi la pili la wanariadha wa kigeni kuwasili kwa ajili ya mazoezi kabla ya kuanza kwa mashindano hayo.