Museveni aomboleza kwa kusaini kitabu ubalozi wa Tanzania nchini Uganda

Chanzo cha picha, MUSEVENI/TWITTER
Rais Yoweri Museveni akiwa na mkewe mama Janet Museveni wameongoza raia wa Uganda katika maombolezo ya aliyekuwa rais wa Tanzania Hayati Dk.John Pombe Magufuli kwa kusaini kitabu cha maombolezo kwenye ubalozi wa Tanzania uliopo mtaa wa Kagera mjini Kampala.
Uganda na Tanzania wamekuwa na ushirikiano mkubwa na ushirikiano wao umeongezeka zaidi tangu alipoingia madarakani Rais Yoweri Museveni mwaka 1986, ndiyo sababu Rais Museveni alitangaza bendera kupeperushwa nusu mlingoti hadi siku ya mazishi siku ya Ijumaa nyumbani kwao wilayani Chato mkoa wa Geita.
Rais Museveni katika hotuba yake fupi amefahamisha kwamba siku ya leo Hayati Magufuli na yeye Rais Museveni pamoja na kampuni ya Total walipanga kusaini rasmi mkataba wa kuanza ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Hoima Uganda hadi bandari ya Tanga.
Pia amekumbusha katika barua aliyomuandikia hayati Magufuli alimfahamisha kwamba sherehe ya leo ingekuwa sherehe ya mara mbili ya sherehe ya siku jeshi la Tanzania JWTZ lilipoingia wilayani Mbarara nchini Uganda magharibi kuondoa utawala wa Idd Amin.
Katika ubalozi wa Tanzania raia wa Tanzania wakiongozwa na Balozi wa Tanzania Dk.Mlima walifanya ibada ya kumuombea Hayati Dk.John Pombe Magufuli.






























