Trump asema makubaliano na Iran bado yanawezekana

Chanzo cha picha, Getty Images
Rais wa Marekani Donald Trump amesema bado anaamini kuna uwezekano wa kufikiwa makubaliano kati ya Marekani na Iran, licha ya kuendelea kwa mashambulizi ya kijeshi na kurejeshwa kwa kizuizi cha majini dhidi ya Tehran.
"Ndiyo, naamini makubaliano bado yanawezekana," alisema Trump alipoulizwa ikiwa bado anaona nafasi ya mazungumzo.
Hata hivyo, Trump alisema Marekani itaendelea kuishambulia Iran huku ikiongeza shinikizo kwa kurejesha kizuizi cha majini kinacholenga biashara ya Iran.
"Tunawashambulia kwa nguvu kubwa na tutaendelea kufanya hivyo. Tunaharibu uwezo wao wote wa kushambulia," alisema.
Rais huyo alisema kizuizi hicho kinaihusu Iran pekee, akisisitiza kuwa meli zinazofanya biashara na Iran hazitaruhusiwa kupita, huku meli nyingine zikiendelea kutumia njia za baharini.
"Yeyote anayefanya biashara na Iran hataweza kupita, lakini wengine wataweza," alisema.
Trump aliongeza kuwa anaamini kizuizi hicho kinaweza kuwa na athari kubwa hata kuliko mashambulizi ya kijeshi, lakini akasema hatua hizo mbili zikichanganywa ndizo zitakazoongeza shinikizo dhidi ya Iran.


























