Raia wa Marekani agundulika na Ebola baada ya kurejea kutoka DRC
Raia mmoja wa Marekani anayefanya kazi katika shirika la misaada ya kibinadamu nchini Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) amegundulika kuwa na ugonjwa wa Ebola, kwa mujibu wa uthibitisho uliotolewa Ijumaa na Vituo vya Marekani vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (CDC).
Kisa hicho kimezua tena taharuki na kuongeza umakini kuhusu mapambano ya Congo dhidi ya moja ya magonjwa hatari zaidi ya virusi duniani.
Kwa mujibu wa taarifa za CBS News na Associated Press, huyu ni raia wa pili wa Marekani kuhusishwa na mlipuko wa sasa wa Ebola, baada ya kisa cha awali kuripotiwa mwezi Mei.
CDC imesema inashirikiana na mwajiri wa mgonjwa huyo, mashirika ya Marekani pamoja na mamlaka za afya nchini Congo, ili kuzuia kuenea zaidi kwa maambukizi na kufuatilia watu waliokuwa na mawasiliano ya karibu na mgonjwa huyo.
Kwa sasa, jina, jinsia na eneo halisi analopatikana mfanyakazi huyo wa shirika la kutoa misaada havijafichuliwa. Hakuna taarifa zaidi zilizotolewa kuhusu hali ya mgonjwa huyo.
Kisa hicho cha maambukizi kinatokea wakati DRC ikiendelea kukabiliana na mlipuko wa Ebola unaoendelea katika majimbo ya mashariki ya Ituri, Kivu Kaskazini, na Kivu Kusini.
Jitihada za DRC za kudhibiti Ebola zinaendelea kukabiliwa na changamoto huku uratibu wa kitaifa ukiimarishwa katika maeneo ya Ituri, North Kivu na South Kivu.
Mamlaka zimethibitisha jumla ya maambukizi 1,830, ambapo wagonjwa 780 wanaendelea kupatiwa matibabu, 284 wamepona, na 648 wamefariki dunia.
Maafisa wanasema ufuatiliaji wa watu waliokutana na wagonjwa umefikia asilimia 78.1, kiwango muhimu katika kufuatilia waliotangamana na mgonjwa kupitia utambuzi na ufuatiliaji wa haraka watu wote walio katika athari ya kuathiriwa na virusi vya Ebola.
Miongoni mwa wahudumu wa mstari wa mbele wanaoshiriki katika kukabiliana na mlipuko huo, wahudumu 112 wa afya wameambukizwa virusi vya Ebola, na 35 wamepoteza maisha, jambo linaloonyesha hatari kubwa wanazokabiliana nazo timu za matibabu.
Aidha, Mkuu wa Africa CDC, Jean Kaseya, alisema kuwa maambukizi ya hivi karibuni yanaonyesha gharama kubwa ya kuchelewa kuchukua hatua dhidi ya ugonjwa huo.
Alieleza kuwa Africa CDC imetuma timu za wataalamu kutoka nyanja mbalimbali katika maeneo yaliyoathirika zaidi mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC), ambako maambukizi mengi ya Ebola yameendelea kuripotiwa.
Soma Zaidi: