Mwanamke aliyezikwa na vifusi aokolewa akiwa hai baada ya saa 36

Chanzo cha picha, Reuters
Kwa mujibu wa Idara ya Zimamoto ya Bogotá, timu za uokoaji zimemtoa mwanamke akiwa hai baada ya kunaswa chini ya vifusi kwa saa 36 katika mji wa Pereira.
Waziri wa Mambo ya Ndani wa Colombia, Rodrigo Lara, amesema katika ujumbe kwenye mtandao wa X kwamba Daniela Largo Sanchez, mwenye umri wa miaka 32, alipatikana chini ya vifusi vya hoteli.
Mwanamke huyo alihamishiwa mara moja katika kituo cha afya cha eneo hilo, ambako anaendelea kupatiwa matibabu.
Kwa mujibu wa Rais Abelardo de la Espriella, waokoaji mjini Pereira bado wanaendelea kuwatafuta zaidi ya watu 40 ambao hawajulikani walipo.
Idadi ya waliofariki katika tetemeko la ardhi lililoikumba Colombia imefikia watu 181, huku vifo vingi vikiripotiwa katika miji ya Cali na Pereira.
Tetemeko hilo lenye ukubwa wa 7.4 lilitokea saa 1:34 asubuhi kwa saa za nchini humo Jumatatu, na mitikisiko yake ilihisiwa katika maeneo makubwa ya magharibi mwa Colombia, huku mitetemeko midogo ikiendelea hadi Jumanne.
Ingawa idadi rasmi ya vifo ni 181, mamlaka za eneo hilo zinasema huenda idadi hiyo ikaongezeka na kuvuka watu 240 kadiri shughuli za uokoaji zinavyoendelea.
Rais wa Colombia Abelardo de la Espriella ametangaza hali ya dharura nchini humo.
Akitoa taarifa kuhusu hali ilivyo mjini Pereira, mojawapo ya maeneo yaliyoathirika zaidi, rais amesema watu wapatao 2,600 wamejeruhiwa na takriban watu 200 bado hawajulikani walipo.
Aidha, amesema zaidi ya nyumba 1,100 zimeharibiwa kabisa, huku zaidi ya nyumba 8,000 zikiharibiwa kwa viwango tofauti.
Soma Zaidi Hapa:
























