Mashambulizi zaidi ya ndege zisizo na rubani dhidi ya Urusi huko Crimea - ripoti

Vyombo vya habari vya Urusi vilisema uvamizi dhidi ya bandari moja magharibi mwa Crimea ulizuiwa siku ya Ijumaa.

Moja kwa moja

  1. Al-Shabab: Vikosi vya Somalia vyadai kumaliza uvamizi wa hoteli uliodumu kwa saa 30

    TH

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Vikosi vya Somalia vinadai kuwashinda wanamgambo wa al shabaab waliovamia hoteli moja katika mji mkuu Mogadishu baada ya kuzingirwa kwa hoteli hiyo na mauaji kutekelezwa .

    Takriban watu 12 waliuawa katika mkasa huo mbaya wa saa 30, ingawa vyombo vya habari vya ndani vinaripoti kwamba idadi ya waliokufa inaweza kuwa kubwa zaidi.

    Washambuliaji walitumia vilipuzi kuingia kwenye Hoteli ya Hayat ya Mogadishu siku ya Ijumaa kabla ya kudhibiti kwa nguvu na kuwachukua mateka wageni usiku kucha.

    Kundi la wapiganaji wa Kiislamu la al-Shabab limekiri kutekeleza shambulio hilo.

    "Vikosi vya usalama vimemaliza uvamizi huo na sasa na watu wenye silaha wamekufa, hatujapata kusikia milio ya risasi kutoka kwa jengo hilo katika saa moja iliyopita," afisa ambaye hakutajwa jina aliambia shirika la habari la AFP.

    Hoteli hiyo imeharibiwa kwa kiasi kikubwa kufuatia mashambulizi makali ya vikosi vya usalama usiku wa kuamkia leo na Jumamosi, huku video zikionyesha moshi ukifuka kwenye paa la jengo hilo.

    BBC haijaweza kuthibitisha kwa njia huru ikiwa shambulio hilo limeisha.

    Afisa wa polisi aliliambia shirika la habari la Reuters kwamba magari mawili yaliyokuwa yametegwa mabomu yalitumiwa kufikia hoteli hiyo Ijumaa jioni - yakilenga kizuizi chake cha mbele na lango.

    Baada ya shambulio la awali, tovuti yenye uhusiano na al-Shabab ilisema kundi la wanamgambo walikuwa "wakifyatua risasi kiholela " baada ya "kuingia kwa lazima" katika hoteli hiyo - inayoelezwa kuwa eneo maarufu kwa wafanyakazi wa serikali ya shirikisho kukutana.

    Unaweza pia kusoma

  2. Ajali juu ya ajali: 16 wafa wakati wakishuhudia na kusaidia majeruhi wa ajali iliyotokea awali

    Turkey

    Chanzo cha picha, Reuters

    Basi moja limewagonga watu kadhaa waliokuwa kwenye eneo la ajali ya awali katika moja ya barabara za nchini Uturuki na kusababisha vifo vya watu 16 na wengine 21 kujeruhiwa.

    Ajali hizo mbili zimetokea karibu na mji wa kusini wa Gaziantep leo asubuhi. Waliofariki ni pamoja na wazima moto, waokoaji na timu ya wanahabari waliokuwa wametumwa kwenda kwenye eneo ambalo ajali ya awali ilitokea ambapo gari lilikuwa limeacha njia.

    Wakati kundi la watu likiwa kwenye eneo la ajali ya kwanza kusaidia majeruhi na waandishi kuripoti tukio, ghafla basi hilo lilienda kuwavaa likateleza na kupinduka umbali wa mita 200 (yadi 220).

    Majeruhi wamekimbizwa hospitali za karibu. Gavana wa mkoa wa Gaziantep alisema kwenye twitter kwamba "wazima moto watatu, wafanyikazi wawili wa dharura na waandishi wa habari wawili" walikuwa miongoni mwa waliokufa kwenye barabara kati ya Gaziantep na Nizip.

    Muungano wa wanahabari wa Uturuki ulithibitisha vifo vya wanachama wake wawili. Picha kwenye mitandao ya kijamii zilionyesha watu kadhaa wakiwa wamelala barabarani. Picha kwenye shirika la habari la DHA la Uturuki zilionyesha sehemu ya nyuma ya ambulensi ikiwa imetolewa nje na vifusi vya chuma vilivyotapakaa kuizunguka.

    Waziri wa sheria Bekir Bozdag ametangaza uchunguzi kuhusu ajali hiyo, BBC Uturuki iliripoti. Baadhi ya wanasiasa wa Uturuki walituma salamu zao za rambirambi mtandaoni.

  3. Aliyepotea miaka 38 iliyopita, apatikana kwenye barafu

    Chandrashekhar Harbola

    Chanzo cha picha, @THEARVINDPANDEY

    "Mama, baba atakuja lini nyumbani?" Mabinti wawili wa Shanti Devi walimuuliza swali hili kila siku kwa miaka mingi. Kila mara alikuwa akiwaambia kwamba baba yao hayupo kazini na angerudi nyumbani hivi karibuni.

    Miaka ilipita, lakini mazungumzo yao yalibaki vilevile. Baba yao, Chandrashekhar Harbola - askari wa jeshi la India - alipotea mwaka 1984 wakati wa operesheni ya doria katika eneo la barafu la Siachen.

    Kikosi kilichokuwa na skari 20 kilinaswa katika maporomoko ya theluji katika kile kinachojulikana kama uwanja wa mapambano au vita uliojuu zaidi duniani (milimani), kwenye mpaka wa India na Pakistan.

    HARBOLA

    Chanzo cha picha, BBC/ASIF ALI

    Miili 15 ilipatikana huku askari wengine watano hawakujuliana walipo wala miili yao kuonekana, akiwemo Chandrashekhar Harbola.

    Alipotangazwa kutoweka, binti yake mkubwa Kavita alikuwa na umri wa miaka minane, huku Babita akiwa na miaka minne.

    Karibu miongo minne baadaye, hatimaye walipata habari kuhusu baba yao, lakini si aina waliyokuwa wakitarajia. Kwamba amefariki. Na muda wote huo mama yao, hakutaka kuolewa kwa kuwa aliamini mumewe yuko hai mahali, labda ametekwa au kuwekwa kizuizini na wapakistan, waliokuwa wakipambana nao vitani.

    Harbola

    Chanzo cha picha, BBC/ASIF ALI

    Mwili ulipatikanaje miaka 38 baadaye?

    Kikosi cha jeshi kilikuwa katika doria ya kawaida wiki iliyopita na kuona eneo maalumu linalotumiwa na wanajeshi kujificha ama kuikinga na risasi ama bomu. Walipokaribia wakakuta mwili. Wakaona na namba ya kitambulisho cha jeshi na kikosi cha Harbola, iliyochorwa kwenye kipande cha chuma.

    Harbola

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Siachen ni moja ya maeneo ya mapambano yaliyo juu zaidi dunaini (milimani).

    Walifikisha taarifa hizo makao makuu na baada ya ukaguzi wa kina wa kumbukumbu zao, walibaini kuwa mwili huo ulikuwa wa askari aliyepotea, Chandrashekhar Harbola.

    "Tulipata taarifa hizi usiku wa Agosti 13', alisema mpwa wake na Harbola, Harish Chandra Harbola. Ulipatikana mwili mwingine katika eneo hilo, lakini haujatambulika ni wa nani mpaka sasa.

    Matukio ya kuvunja moyo

    Kavita, ambaye sasa ana umri wa miaka 46, na Babita, ambaye sasa ana umri wa miaka 42, walikuwa wakisubiri wpamoja na mama yao wakati lori lililobeba mwili wa Harbola lilipofika.

    Harbola

    Chanzo cha picha, BBC/ASIF ALI

    Umati mkubwa wa ndugu, majirani na wananchi walikuwa wamekusanyika kumpa heshima zake. Tukio hilo lilikuwa likiambatana na nyimbo mbalimbali za huzuni ukiwemo unaosema Chandrashekhar Harbola hawezi kufa.

    Kila mtu aliyekuwepo machozi yalimtoka. Na wengi wao hawakuamini kwamba mwili wake ulikuwa umepatikana. Sio kila siku ambapo mwili hupatikana baada ya miaka 38 na kuletwa nyumbani kwa heshima kamili ya kijeshi. Kwa familia yake, suala hili limefungwa. Lakini uchungu wa kukatishwa tamaa kwa matumaini utakaa kwa muda mrefu.

  4. Rais mteule wa Kenya William Ruto akutana na ujumbe WFP

    th

    Chanzo cha picha, William Samoei Ruto/Facebook

    Rais mteule wa Kenya William Ruto ameendelea kukutana na jumbe mbali mbali zinazomzuru katika makao rasmi ya naibu rais Karen,jijini Nairobi .

    Kando na mikutano ya jumbe za viongozi wa kisiasa wengine kutoka vyamaambavyo havikumuunga mkono katika uchaguzi uliopita ,Ruto amekuwa akikutana na jumbe za wawakilishi wa mashirika ya kimataifa .

    Wa hivi punde kukutana naye ni Mkurugenzi mkuu wa shirika la chakula Duniani WFP David Beasley.Kupitia chapisho lakekwenye mitandao ya kijamii ,Ruto alisema walijadili hali ya kiangazi kaskazini mwa Kenya na upembe wa Afrika .

    Alisema mpango wa serikali ijayo utakuwa kuwapa msaada wakulima kupitia ruzuku ili waweze pia kupata mikopo .

    Unaweza pia kusoma

  5. Makombora ya Urusi yadunguliwa mashariki mwa Ukraine - ripoti

    TH

    Chanzo cha picha, Reuters

    Makombora manne ya Urusi yamedunguliwa mashariki mwa Ukraine, linasema shirika la habari la Ukraine UNIAN.

    Kulingana na ripoti hizo, ambazo zimeonekana lakini hazijathibitishwa na BBC, vikosi vya ulinzi wa anga vya Ukraine vilinasa makombora manne ya Kalibr ya Urusi katika eneo la mashariki la Dnipropetrovsk.

    "Mwanzo mzuri wa Jumamosi [20 Agosti] kutoka kwa jeshi letu," mkuu wa utawala wa kijeshi wa kikanda, Valentyn Reznichenko, alinukuliwa akisema.

    "Ulinzi wetu wa anga ulidungua eneo la Dnipropetrovsk makombora yote manne ya Kalibr ambayo Warusi walilenga eneo hilo. Utukufu kwa jeshi letu!"

    Kamanda mkuu wa Kikosi cha Wanajeshi cha Ukraine, Valeriy Zaluzhnyy, aliripotiwa kusema kuwa makombora manne ya S-300 yalitumiwa kuangusha makombora ya Kalibr, karibu na jiji la Dnipro.

    Unaweza pia kusoma

  6. Mwanasheria mkuu wa zamani wa Mexico akamatwa akihusishwa na tukio la kutoweka kwa wanafunzi 43

    Mexico

    Mwanasheria mkuu wa zamani wa Mexico amekamatwa akihusishwa na kutoweka kwa wanafunzi 43 mwaka wa 2014.

    Jesús Murillo Karam, ambaye aliongoza uchunguzi wa ukatili huo, ameshtakiwa kwa kutoweka kwa wanafunzi hao, mateso na kuzuia haki kutendeka.

    Wanafunzi hao walitoweka walipokuwa wakisafiri kwa basi kupitia mji wa Iguala wakielekea kwenye maandamano katika Jiji la Mexico.

    Zaidi ya vipande vya mifupa vichache vilivyopatikana kutoka kwa watatu kati yao 43, hakuna kilichoonekana wala kujulikana juu ya hatima yao.

    Inaelezwa Polisi walifyatulia risasi mabasi yaliyokuwa yamewabeba wanafunzi jioni ya tarehe 26 Septemba 2014 - lakini kilichotokea baadaye kimeibua mjadala.

    Kutoweka kwao kwa kushangaza kulileta mshtuko kote ulimwenguni na kusababisha maandamano makubwa nchini Mexico dhidi ya vitendo vya kutokujali na kushiriki katika uhalifu.

    Siku ya Alhamisi, tume iliyoundwa na Rais wa sasa Andrés Manuel López Obrador ilishutumu wanajeshi kwa kuhusika na mauaji hayo - sio moja kwa moja bali angalau kwa uzembe.

    Mapema mwaka huu Rais López Obrador alifichua kuwa wanajeshi wa wanamaji walikuwa wakichunguzwa kwa madai ya kuvuruga ushahidi, ikiwa ni pamoja na katika eneo la kutupa taka ambapo mabaki ya binadamu yalipatikana.

    Siku ya Ijumaa, alitoa wito kwa askari au maafisa wowote waliohusika katika kutoweka kwa wanafunzi hao kufikishwa mbele ya haki.

  7. Mashambulizi zaidi ya ndege zisizo na rubani dhidi ya Urusi huko Crimea - ripoti

    th

    Chanzo cha picha, Reuters

    Mashambulizi zaidi ya ndege zisizo na rubani dhidi ya malengo ya Urusi yameripotiwa huko Crimea na maeneo mengine yanayokaliwa na Ukraine.

    "Moshi unapaa juu ya makao makuu ya meli ya Bahari Nyeusi ya Shirikisho la Urusi huko Sevastopol," shirika la utangazaji la Suspilne la Kiukreni liliripoti asubuhi ya leo, likinukuu vyombo vya habari vya ndani na kuchapisha video kutoka eneo la tukio.

    BBC bado haijaweza kuthibitisha mashambulizi hayo.

    Vyombo vya habari vya Urusi vilisema uvamizi dhidi ya bandari moja magharibi mwa Crimea ulizuiwa siku ya Ijumaa.

    Video zilizorekodiwa huko Crimea zilionyesha ulinzi wa anga ya Urusi ukikamata shabaha angani juu ya Sevastopol, Yevpatoriya na Zaozerne. Mamlaka zinazoikalia kwa mabavu Urusi zilisema hizi ni ndege zisizo na rubani za Ukraine, lakini hili halijathibitishwa kwa njia huru na BBC.

    Kumekuwa na msururu wa mashambulizi dhidi ya maeneo ya jeshi la Urusi na vifaa vyake huko Crimea wiki iliyopita, ambayo Ukraine haijadai kuhusika nayo.

    Peninsula hiyo ilichukuliwa na Urusi mnamo 2014.

    Maafisa wa nchi za Magharibi wamesema mashambulizi hayo dhidi ya Crimea yana madhara makubwa ya kisaikolojia na kiutendaji kwa vikosi vya Moscow.

    Milipuko katika kambi ya anga ya Saki tarehe 9 Agosti na mashambulizi mengine yameziweka zaidi ya nusu ya ndege za meli za bahari ya Black Sea kufanya kazi, walisema.

    Unaweza pia kusoma

  8. Vanessa asema alishangazwa na kuvujishwa kwa picha za eneo la mkasa alikofariki mume wake Kobe Bryant

    Kobe wife

    Mjane wa Kobe Bryant amethibitisha kuwa alipatwa na hofu baada ya kujua kwamba picha za ajali ya helikopta iliyoua mumewe na bintiye zilipigwa na kusambazwa.

    Vanessa Bryant anaishtaki kaunti ya Los Angeles baada ya watu wa kwanza kujibu kudaiwa kusambaza picha za ajali hiyo. "Nilitarajia wangekuwa na huruma zaidi," aliwaambia majaji katika ushahidi wake wa kesi ya faragha.

    Bi Bryant, 40, anatafuta mamilioni ambayo haijabainishwa kwa ajili ya matatizo yake ya kihisia.

    Mumewe, nguli wa mpira wa vikapu Kobe Bryant, 41, binti Gianna, 13, na marafiki sita wa familia walikufa wakati helikopta yao ilipoanguka katika Thousand Oaks, California mnamo Januari 2020.

    Ripoti ya Los Angeles Times inayodai wafanyikazi wa kaunti walipiga picha kwenye eneo la ajali na kuzishiriki na wengine imewakasirisha familia za waathiriwa.

    Novemba mwaka jana, kaunti ilikubali kulipa $2.5m (£2.1m) kutokana na dhiki ya kihisia iliyosababishwa na familia mbili zilizopoteza jamaa zao kwenye ajali hiyo - lakini Bi Bryant alikataa fidia hiyo.

  9. Mzozo wa Ukraine: Urusi kuwaruhusu wakaguzi wa UN kukagua kinu cha nyuklia cha Zaporizhzhia - Putin

    Ukraine

    Rais wa Urusi Vladimir Putin amesema maafisa wa Umoja wa Mataifa watapewa kibali cha kuzuru na kukagua kinu na kambi ya nyuklia ya Zaporizhzhia.

    Ikulu ya Kremlin ilitoa tangazo hilo baada ya mazungumzo kwa njia ya simu kati ya Bw Putin na Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron.

    Hatua hiyo inakuja huku madai ya mapigano karibu na mtambo huo yakiendelea, na kusababisha raia wanne kujeruhiwa na makombora ya Urusi.

    Mbali na hilo, Marekani iliahidi siku ya Ijumaa kutuma silaha na risasi zaidi kusaidia katika juhudi za vita vya Ukraine.

    Kufuatia mazu ngumzo ya viongozi hao wa Ufaransa na Urusi, Kremlin ilisema, Bw Putin amekubali kuwapa wachunguzi wa Umoja wa Mataifa "msaada unaohitajika" ili kufikia eneo la nyuklia la Zaporizhzhia.

    Kinu hicho kimekuwa chini ya umiliki wa Warusi tangu mapema Machi lakini mafundi wa Kiukreni bado wanakiendesha chini ya maelekezo ya Urusi.

    Unaweza pia kusoma