Piripkura: Kabila la kiasili linalokabiliwa na 'tisho la kuangamia' msitu wa Amazon

Chanzo cha picha, Bruno Jorge
"Nina wasiwasi nao. Watauawa na tutaangamia."
Wakati Rita Piripkura alipokuwa akisimulia hali zao sauti yake iliashiria mtu aliyepoteza matumaini.
Mwanamke huyo mzee alikuwa akimwangazia kaka yake Baita na mpwa wake Tamandua katika mahojiano yaliyorekodiwa yaliyotolewa Septemba.
Watatu hawa ndio wanachama wa mwisho wanaojulikana wa watu waliotengwa wa Piripkura, kabila la kiasili katikati mwa Brazili ambalo wataalam wanasema linakabiliwa na "tisho la kuangamia" kwa sababu ya ukataji miti ovyo na ufugaji kwenye hifadhi yao.

Chanzo cha picha, Bruno Jorge
Ijapokuwa Rita anawasiliana mara kwa mara na watu wa nje, Baita na Tamandua hutumia siku zao kuzurura msitu wa Amazon wakiwa wamejitenga. Anaogopa kwamba hata kazi hiyo isiyokuwa na hatia inaweza kuwa hatari kwao.
Kushindwa vita
Hifadhi ya Piripkura iliyopo katika jimbo la Mato Grosso, ambalo ni muhimu sana kwa biashara ya kilimo ya Brazil, linapoteza asili yake kwa wakataji miti na wakulima ambao wanavamia eneo lao, licha ya kulindwa na sheria.
Wakati Piripkura wanateseka mikononi mwa watu wa nje wanaotishia kuangamiza kizazi chao, kasi ya uharibifu imeongezeka katika siku za hivi karibuni: Ripoti iliyochapishwa mwanzoni mw mwezi Novemba ambayo ilitoa ushahidi wa picha unaoonesha uharibifu wa makazi ya asilia katika msitu Amazon, matandao wa mashirika yasiyokuwa ya kiserikali unadai kuwa eneo la karibu kilo mita 24 mraba la msitu limeharibiwa katika hifadi ya Piripkura kati ya Augostu 2020 na Julai 2021 pekee.
Hiyo ni sawa na zaidi ya viwanja 3,000 vya soka vilivyowekwa pamoja.
Licha ya hifadhi nyingine za kiasili kote Brazil pia kukabiliwa na changamoto kutoka wa wakataji miti, wakulima na wachimba migodi, watu wa Piripkura wanakabiliwa na hali mbaya sana.

Chanzo cha picha, Survival International
"Wako kwenye ukingo wa kutoweka na wanaweza kuuawa katika muda wa siku chache," Sarah Shenker, mwanaharakati katika shirika lisilo la kiserikali lisilo la kiserikali la Survival International lenye makao yake mjini London, linaambia BBC.
"Wavamizi wanawakaribia Baita na Tamandua kila wakati."
Kuna ushahidi mzuri kwamba watu wa nje wanavamia hifadhi hiyo kwa haraka, kulingana na Leonardo Lenin, mratibu wa zamani wa Funai, wakala wa serikali ya Brazil wa masuala ya kiasili, ambaye amefanya kazi sana na makabila huko Mato Grosso.

Chanzo cha picha, Rogerio de Assis - ISA
Sasa katibu mkuu wa shirika lisilo la kiserikali la Observatory of Indigenous Human Rights (OPI), moja ya mashirika yaliyoandika ripoti ya Piripkura, yanasema kuwa ukataji miti umeonekana katika umbali wa kilomita 5 kutoka maeneo ambayo Baita na Tamandua walionekana au kuachwa hapo awali au kuacha nyayo zao.
Huo unaweza kuonekana kama umbali salama, lakini katika muktadha wa kiwango cha hifadhi - kilomita za mraba 2,430 - kwa kweli ni karibu sana.

"Wako katika hatari kubwa, hakuna shaka juu ya hilo," Lenin anasema.
"Pia tumesikia ripoti kwamba wakaguzi kutoka Funai na wakala wa ulinzi wa mazingira wa Brazil wametishiwa na wavamizi."
Hali mbaya ya makabila yaliyotengwa
Piripkura ni mfano wa yale ambayo wataalam wa kiasili wanayaita makabila yasiyoguswa au yaliyotengwa - watu wote au vikundi vidogo ambavyo havijapata mawasiliano ya mara kwa mara na majirani zao au mtu mwingine yeyote katika ulimwengu wa nje.

Chanzo cha picha, Ricardo Stuckert
Inakadiriwa kwamba kuna zaidi ya watu 100 kati ya vikundi hivyo duniani kote, na zaidi ya nusu katika eneo la Amazoni.
Kutengwa huko mara nyingi ni matokeo ya migongano na wavamizi, na Piripkura wamekuwa na sehemu yao ya shida.
Idadi kubwa ya jamaa zao waliuawa katika miaka ya 1970, wakichinjwa na wavamizi au kupata magonjwa ya kawaida kama vile homa, ambayo yalisababisha kifo kwa mifumo ya kinga ambayo haijawahi kukutana na virusi kama hivyo.
Rita anakumbuka kunusurika katika mauaji hayo ambapo tisa kati ya jamaa zake walikufa.
"Wao (wavamizi) waliwaua na tukalazimika kukimbia," alisema.
Pamoja na kupunguza idadi yao kwa kiasi kikubwa, Lenin anaeleza kuwa mapigano hayo yanaonekana kuwa na athari kubwa katika njia ya maisha ya Piripkura.

Chanzo cha picha, Ricardo Stuckert
"Lugha yao ina maneno ya kuelezea mazoea ya kilimo, ambayo yanaonyesha walikuwa na aina fulani ya jamii ya kilimo hapo awali."
"Lakini tangu miaka ya 1970 wamekuwa wawindaji wa kuhamahama."
"Ni mkakati wao wa kuishi kuwa katika harakati kila wakati."
Piripkura ilipowasiliana kwa mara ya kwanza na Funai mwaka 1984, wafanyakazi waliripoti kwamba kulikuwa na watu 15-20 pekee ambao walikuwa wanaishi katika hifadhi nzima.
Lakini ni Baita na Tamandua pekee ndio wameonekana tangu miaka ya 1990.
Fabricio Amorim, mtaalam wa watu wa kiasili ambao hawajawasiliana ambaye pia amefanya kazi na Piripkura, anasema kuwa Baita na Tamandua walikuwa wametaja kuwepo kwa "jamaa" ambao bado wanazurura msituni katika mawasiliano ya awali.
"Tatizo ni kwamba hawajawataja jamaa hao kwa miaka mingi. Haimaanishi moja kwa moja kwamba wamekufa, lakini pia sio ishara nzuri," Amorim anakiri.
"Ukweli kwamba hatuwezi kusema kwa uhakika kwamba hakuna Piripkura zaidi karibu inafanya kuwa muhimu zaidi kuhifadhi ardhi yao," anaongeza.













