Marekani yatoa tahadhari ya kiwango cha juu kufuatia kuapishwa kwa rais Joe Biden

Chanzo cha picha, EPA
Maafisa wakuu wa usalama nchini Marekani wameonya kuhusu tisho la tukio la kigaidi nchini humo kutoka kwa watu wasiopenda matokeo ya uchaguzi uliopita.
Idara ya usalama wa ndani nchini humo imesema kwamba uvamizi wa tarehe sita Januari wa majengo ya bunge uliotekelezwa na wafuasi wa Donald Trump huenda umewapatia msukumo watu wenye itikadi kali.
Katika taarifa yake kwa umma , imeonya kuhusu tisho kutoka kwa watu binafsi waliokasirishwa na jinsi serikali inavyotekeleza mamlaka yake.
Lakini pia iliongezea kwamba hakuna habari za moja kwa moja kuhusu njama fulani.
Uvamizi wa jengo la bunge nchini Marekani ulijiri wakati ambapo wabunge wa bunge la uwakilishi walikuwa wanakongamana kuthibitisha ushindi wa rais Joe Biden .
Aliyekuwa rais Donald Trump awali alikuwa amehutubia maelefu ya wafuasi wake nje ya Ikuu ya Whitehouse na kurejelea madai yasio ya kweli kwamba uchaguzi huo ulikuwa umeibwa.
Aliwaambia: Iwapo hamtapigana hamutakuwa na taifa tena.
Kundi moja baadaye likaelekea katika jengo la Bunge la Capitol , na kuwashinda nguvu maafisa wa usalama na kuingia ndani . Watu watano akiwemo afisa mmoja wa polisi alifariki katika ghasia hizo.
Rais Trump kwa sasa ameshtakiwa na bunge la uwakilishi kwa kuchochea ghasia na kesi yake katika bunge la seneti inatarajiwa kuanza mwezi ujao.
Taarifa hiyo ya tahadhari iliotolewa siku ya Jumatano ilisema kwamba idara hiyo inaamini kwamba tishio litaendelea kuwepo katika wiki zinazojiri baada ya rais kuapishwa.
''Habari zinasema kwamba watu wenye itikadi kali na wanaopinga utekelezwaji wa mamlaka ya serikali na kuapishwa kwa rais pamoja na malalamishi mengine yanayosababishwa na madai ya uwongo, yanaweza kuendelea kuchochea vurugu'', "ilisema.
Tahadhari hiyo iliongezea kwamba raia wa Marekani walio na itikadi kali huenda wakachochewa na kupewa msukumo na uvamizi wa jengo la bunge ili kuwalenga wabunge na vifaa vya serikali.
Ni tahadhari ya kwanza kwa umma kutolewa na idara hiyo katika kipindi cha mwaka mmoja.
Uvamizi wa jengo la bunge uliwashangaza wengi nchini humo na mamlaka ilichukua hatua za haraka kuwatambua na kuwakamata wahusika.
Waendesha mashtaka wanasema kwamba kufikia sasa wamewatambua washukiwa 400 na kuwakamata 135 kuhusiana na ghasia hizo.












