Ripoti: Kanisa la Uingereza 'limeshindwa kuwalinda watoto' dhidi ya unyanyasaji wa kijinsia

Iliyochapishwa

Kanisa la Uingereza limeshindwa kuwalinda watoto kutokana na vitendo vya unyanyasaji kingono dhidi ya watoto, na kutengeneza utamaduni wa ''kuwawezesha watekelezaji wa vitendo hivyo kujificha'' Ripoti imehitimisha.

Ripoti ya taasisi huru iliyokuwa ikifanyia uchunguzi matukio ya unyanyasaji wa kingono dhidi ya watoto (IICSA) imesema kuwa kitendo cha kanisa kushindwa kuchukua hatua kuwanusuru waathirika na manusura wa vitendo hivyo kumewasababishia matatizo zaidi ya kiasikolojia.

Iliongeza kuwa watuhumiwa mara nyingi walipewa msaada zaidi kuliko waathirika.

Kanisa la Uingereza linatarajiwa kuchapisha majibu baadae.

Ripoti hiyo, ambayo ni ya hivi karibuni katika mfululizo wa machapisho kutoka IICSA, inasema viongozi 390 wa dini na viongozi wengine wa kanisa walihukumiwa kwa unyanyasaji kati ya miaka ya 1940 na 2018.

Mwaka 2018 kulikuwa na wasiwasi wa kulinda kesi 2,504 zilizoripotiwaa kwa majimbo (dayosisi) kuhusu watoto au watu wazima walio katika mazingira magumu, na madai 449 ya unyanyasaji wa kijinsia wa watoto hivi karibuni.

Uchunguzi huo ulisema kwamba Kanisa la Uingereza lilikuwa "linapingana moja kwa moja na dhamira yake ya msingi ya maadili katika kuwatunza na kutoa upendo kwa wasio na hatia na wanyonge".

Mwenyekiti wake, Prof Alexis Jay, alisema: "Kwa miongo mingi, Kanisa la Uingereza lilishindwa kulinda watoto na vijana dhidi ya wanyanyasaji wa kijinsia, badala yake kuwezesha utamaduni ambapo wahusika wanaweza kujificha na wahanga kukabiliwa na vizuizi vya kutoa taarifa ambavyo wengi wasingeweza kushinda.

"Ndani ya Kanisa huko Wales, hakukuwa na maafisa wa kutosha wa kutosha kutekeleza idadi ya kazi zinazohitajika kufanywa. Utunzaji wa kumbukumbu uligundulika kuwa haupo na hautumiki sana kujaribu kuelewa masuala ya zamani ya ulinzi."

Aliongeza ni "muhimu" Kanisa kuboresha jinsi inavyoshughulikia madai ya unyanyasaji wa kijinsia wa watoto, na inapaswa kutoa "msaada mzuri" kwa waathiriwa.

Ripoti hiyo, ambayo inayoegemea mkutano wa wazi wa uchunguzi uliofanyika mnamo Julai 2019, ilitoa mapendekezo kadhaa, pamoja na:

  • Kanisa la Uingereza linapaswa kuimarisha namna linavyoshughulikia madai -kwa mfano kwa kuweka sheria ya kuwafukuza viongozi wa kidini wanaokutwa na hatia ya kujihusisha na vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia.
  • Uwajibikaji wa kutoa ulinzi unapaswa kuondolewa kwenye mikono ya maaskofu wa dayosisi na kuwapa jukumu hilo maafisa walioajiriwa na uongozi wa Kanisa.
  • Kanisa la Uingereza na Kanisa la Wales wanapaswa kubadilishana taarifa kuhusu viongozi wanaohama kati ya taasisi hizo mbili.
  • Kanisa linapaswa kuanzisha sera za ufadhili na msaada kwa manusura wa vitendo vya unyanyasaji wa watoto ambao wanaowadhulumu wana mahusiano ya karibu na Kanisa

Profesa Jay amesema ana matumaini ripoti hiyo na mapendekezo yatasaidia kuhakikisha kuwa ''hali hii haijitokezi tena''.