Imran Khan akosolewa baada ya kumuita Osama Bin Laden mfiadini

Chanzo cha picha, AFP
Waziri Mkuu wa Pakistani Imran Khan amekiona cha moto kutoka upande wa upinzani bungeni baada kuarifu bunge kwamba Marekani ilimuua Osama Bin Laden.
Bin Laden, mtekelezaji wa mashambulio ya 9/11, was aliuawa 2011 pale vikosi maalum vya Marekani vilipovamia eneo alilokuwa amejificha katika mji wa Pakistani wa Abbottabad.
Pakistan haikuarifiwa mapema kuhusu maamuzi hayo ya Marekani.
"Sitasahau vile sisi raia wa Pakistan tulipoabishwa pale Marekani ilipoingia mji wa Abbottabad na kumuua Osama Bin Laden," Khan amesema.
Khan alitumia neno "shaheed" - neno la kiungwana linalomaanisha kuuawa kwa Muislamu aliyekufa kwa ajili ya dini.
Kiongozi wa upinzani na aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje Khawaja Asif alimkosoa Bwana Khan, na kumuita Bin Laden "gaidi".
"Aliharibu taifa langu, na [Khan] anamuita shahidi," Bwana Asif amesema hivyo bungeni.
Bilawal Bhutto Zardari, ambaye chama chake cha Pakistan Peoples kilikuwa uongozini wakati Bin Laden anauawa, alimshtumu waziri mkuu kwa kusifia vurugu, ghasia na wenye msimamo mkali.
Meena Gabeena, mwanaharakati wa ngazi ya juu Pakistani, ameandika kwenye Twitter: "Waislamu kote duniani wanapitia kipindi kigumu kwasababu ya kunyanyapaliwa kwasababu ya ugaidi ambao umekuwa ukitokea hivi karibuni, na Waziri wetu Mkuu anafanya hali hiyo hata kuwa mbaya zaidi kwa kumuita [Osama Bin Laden] Shahidi wa Uislamu!"
Hotuba ya Bwana Khan inawadia wakati ofisi ya wizara ya mambo ya nje ya Waziri Mkuu Pakistan kukatalia mbali ripoti ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani inayoshtumu Pakistan kwa kuendelea kuwa eneo salama kwa makundi ya kigaidi ya eneo.
"Wakati ambapo ripoti hiyo inatambua kuwa kwa kiasi kikubwa kundi la al-Qaeda limesambaratishwa eneo hilo, haikutaja jukumu la msingi la Pakistan katika kuangamiza kundi hilo, na hivyo basi kupunguza makali ya kwamba kuna wakati kundi hilo, lilikuwa tishio duniani," Wizara ya mambo ya nje imesema.

Chanzo cha picha, AFP
Bwana Khan, ambaye alikuwa mchezaji wa Kriketi, awali aliwahi kukosolewa kwa kuonesha kupendelea Taliban na wapinzani wakambandika jina la "Taliban Khan".
Baada ya matamshi yake tatanishi juu ya Bin Laden Alhamisi, Afrasiab Khatak, aliyekuwa seneta na kiongozi wa Tume Huru ya Haki za Binadamu Pakistan amesema katika mtandao wa Twitter: kwamba Waziri Mkuu aliingia madarakani kutekeleza "ajenda za Taliban ".
Katima mahojiano ya televisheni miaka minne iliyopita, bwana Khan alikataa kumuita Bin Laden kuwa ni gaidi wakati wa mahojiano.

Utafiti: M Ilyas Khan, BBC News, Islamabad
Imran Khan amemuita Osama Bin Laden mfiadini sio kwasababu ya wanaendana kiitikadi na aliyetekeleza mauaji ya 9/11 lakini kwasababu za kisiasa.
Dunia imekuwa na siasa za muda mrefu katika suala la mauaji ya 9/11, lakini wanamgambo wa kisiasa bado wanachukuliwa na wachambuzi kama silaha kuu ya jeshi la Pakistan lenye nguvu kuendeleza malengo yake nchini India na Afghanistan.
Bin Laden na viongozi wengine waandamizi wa al-Qaeda na Taliban wa wakati huo bado wanaheshimiwa na wanamgambo, na pia wana jukumu muhimu katika kusajili vijana.
Hatua yoyote ya kushusha hadhi ya Bin Laden huenda ikawa na athari kubwa kwake.
Bwana Khan anachukuliwa na wakosoaji wake kama aliyekaribu sana na jeshi mjumbe aliyepewa madaraka katika uchaguzi wa 2018, ambao unasemekana ulikumbwa na udanganyifu kutoka upande wa jeshi.
Maneno yake Alhamisi sio ajali. Wengi waliona kwamba katika hotuba yake kwanza kabisa alitumia neno kuuawa kwa Bin Laden, kisha akanyamaza na kurekebisha kwa kusema kuwa amekufa kama shahidi (mfiadini).












