Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Wanaojiita watoza ushuru wa Naijeria: mtindo wao kama mafia
Wanaojiita watoza ushuru wa Naijeria: wanaofanana kama mafia
Akiwa ameajiriwa kama mtu anayejiita mtoza ushuru na familia kadhaa zenye ushawishi mkubwa, Kapteni Nwokuha anaonyesha sura ya kutisha anapotembea na fimbo yake mfano wa mbao kutekeleza mamlaka yake katika barabara ya makutano yenye shughuli nyingi katika mji wa kusini wa Nigeria wa Port Harcourt.
Kazi ya kijana huyo mwenye umri wa miaka 34 ni kukusanya "kodi" kwa kile anachokiita "jamii" kutoka kwa teksi na mabasi ya abiria 18 ambayo hufanya kazi katika sehemu hiyo ya jiji.
Kazi ya Bw Nwokuha ina mizizi yake katika utamaduni wa zamani, wakati wafanyabiashara walikuwa wakilipa ada ya mara moja, au zawadi ya kinywaji, kama heshima kwa wenyeji wao kwa habari njema.
Lakini sasa imegeuka kuwa kile wakosoaji wanasema ni ulaghai.
Baadhi ya familia, zinazodai kuchukua hatua kwa niaba ya jamii za wenyeji, hudai ada kutoka kwa wafanyabiashara, wawe madereva wa teksi au wafanyabiashara wa soko, wanaofanya kazi katika kile wanachoona kama haki yao.
Bw Nwokuha anasema anakusanya naira 5-7,000 (£5-7; $6.50-9) kwa siku - kiasi cha kuridhisha nchini Nigeria.
Akiwa ameoa na ana watoto wawili, anahifadhi baadhi ya pesa huku nyingine zikipewa familia tano zenye nguvu katika jamii - ambapo hupotea katika msururu wa mifuko ya watu binafsi.
Wanaoitwa watoza ushuru au mawakala wa watu wengine, pia hutumiwa na majimbo ya Nigeria na serikali za mitaa kukusanya baadhi ya kodi.
"Maajenti hawa hutumia akaunti za kibinafsi na kufanya makato kabla ya kupeleka kwa serikali," anasema Michael Ango, afisa wa zamani wa ushuru wa serikali ambaye sasa yuko na kampuni ya kibinafsi ya Andersen Tax.
"[Mbinu zao] zinajenga hisia kwamba serikali inatumia nguvu na misuli badala ya uhalali."
Ikiongozwa na Rais mpya Bola Tinubu, serikali ya Nigeria imeapa kukabiliana na kile inachokiita "watozaji ushuru, wakorofi na watoza ushuru wanaojilazimisha".
Kuhusu Bw Nwokuha, anaamini kuwa ana jukumu muhimu, akifanyakazi kama afisa wa trafiki ambaye anasuluhisha mizozo katika biashara ya teksi iliyokithiri.
"Ikiwa kuna vita kati ya madereva ninasuluhisha," anasema Bw Nwokuha, ambaye hushika doria kwenye makutano ya Rumuola ya bandari ya Harcourt siku za wiki kuanzia alfajiri hadi jioni akiwa amevalia fulana yake yenye mng’ao.
Kabla ya dereva kuanza safari, mtu aliyeandikwa ambaye hadi fulana yake inamaandishi kuashiria kuwa ni yeye, anapokea 20% ya nauli za abiria.
"Teksi haziruhusiwi kufanya kazi hapa," asema Bw Nwokuha, akionyesha alama ya "hakuna maegesho" iliyopakwa rangi za polisi.
"Lakini wakiamua, basi wanapaswa kulipa kwa jamii," anaiambia BBC.
Katika tukio nadra ambapo dereva anakataa kulipa, wanaweza kuvunjiwa kioo cha pembeni au taa ya nyuma - au nambari zao za usajili wa gari kuondolewa.
Wakithubutu kupigana, wanaweza kukumbana na fimbo ya mbao ya Bw Nwokuha ikipasua fuvu lao.
Bw Nwokuha anafanya kile ambacho kinafaa kuwa kazi ya wafanyikazi wa baraza la mtaa.
Nigeria ina mabaraza 780 lakini mengi yao hayafanyi kazi.
Ombwe hilo linajazwa na wanaume kama Bw Nwokuha - au pengine mtu yeyote ambaye anaweza kuweka kizuizi barabarani na kutekeleza mamlaka yao.
Hizi huwa zinajumuisha kizuizi cha mbao kati ya mapipa mawili yenye kutu, na miiba iliyotengenezwa nyumbani kwa madereva wanaotaka kuwa werevu kwa kujaribu kuziepuka.
Zinapatikana zaidi katika maeneo tajiri ya kusini mwa Nigeria, ikiwa ni pamoja na barabara kuu ambapo ukusanyaji wa ushuru hufanywa kwa niaba ya baadhi ya serikali za majimbo.
Dereva mmoja wa lori anaiambia BBC kuwa analipa kiasi cha naira 80,000 (£80; $100) anaposafiri kwenye vizuizi vingi akiwa njiani kutoka jiji kubwa la Nigeria, Lagos, hadi Imo mashariki: umbali wa 540km (maili 335) .
"Kati ya Edo na bandari ya Harcourt [peke yake] kuna vizuizi 15 kama hivyo," anaongeza.
Akitoa maoni kama hayo, mwendeshaji wa vifaa vya nyakati ya baridi anasema: "Kuna kodi nyingi za usafirishaji, kuna moja inaitwa mapato, kuna ushuru wa redio, kuna ushuru wa kupakia, mwingine wa maegesho, mmoja wa kupakua."
Na hiyo haijumuishi hongo anazolazimika kulipa maafisa wa polisi anapozunguka nchi nzima.
Clement Akanibo, wa Taasisi ya Chartered Taxation ya Nigeria, anaielezea kama "sawa na kukusanya ushuru kwa mtutu wa bunduki".
"Inafanya kuwa vigumu kufanya biashara na huongeza gharama ya mwisho kwa asilimia 15," anasema.
Haijulikani ni jinsi gani Bw Tinubu anapanga kukomesha hili, lakini atahitaji kuungwa mkono na serikali za majimbo na serikali za mitaa kwani kodi hizi ziko chini ya mamlaka yao - sio ya serikali ya shirikisho.
Kitovu cha haya yote, kuna mfumo wenye nguvu wa ufadhili ambao unahusisha sehemu ya pesa zikiingia kwenye mifuko ya wanasiasa, familia zenye nguvu, na jeshi la watu wasio na ajira kama Bw Nwokuha.
Serikali ya Bw Tinubu inasema inataka kurekebisha mfumo mzima wa ushuru ili kuongeza mapato yake ili iweze kuongeza kiasi inachotumia katika huduma kama vile afya na elimu, na pia kulipa madeni yake yaliyoonegezeka.
Imejiwekea lengo la kuongeza uwiano wa kodi kwa Pato la Taifa hadi 18% ndani ya miaka mitatu ijayo.
Takwimu rasmi za Nigeria zinaonyesha uwiano ulikuwa karibu 11% mwaka wa 2021, chini ya kile Benki ya Dunia iliripoti kwa Kenya (13%) na Afrika Kusini (26%).
Kwa sasa, serikali ya Bw Tinubu inaangazia ushuru unaowajibika - ikiwa ni pamoja na Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT).
Serikali kuu haitumii wanaoitwa watoza ushuru, wakitarajia wafanyabiashara kufanya malipo ya moja kwa moja.
Katika kile kinachoonekana kuwa jaribio la kukomesha ukwepaji kodi, inataka kuweka malipo ya VAT kwenye dijitali, kuanzia na muungano wa wafanyabiashara wa sokoni wenye thamani ya milioni 40.
Hili halitakuwa rahisi kwani wengi wao hawahifadhi rekodi za kifedha na hawajawahi kulipa VAT, kwa hivyo wanaweza kupinga hatua hiyo huku kukiwa na ugumu wa kiuchumi uliopo.
Lakini kama mpango huo utafanya kazi, serikali ya Bw Tinubu inaweza kutumaini kushawishi serikali za majimbo na serikali za mitaa kuacha mfumo wao wa kizamani - jambo ambalo Wanigeria wengi wangelifurahia kwani lingewakomboa kutoka kwenye makucha ya watoza ushuru wanaotisha kama Bw Nwokuha.