Simulizi ya Brigade ya Wanawake Weusi ambayo haipewi heshima yake katika historia

Iliyochapishwa

Na Oprah Flash na Amy Johnston

BBC News, West Midlands

Black women

Chanzo cha picha, US NATIONAL ARCHIVES

Simulizi ya kundi la wanawake weusi waliotoka Marekani hadi Uingereza wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia ili kutatua mzozo wa posta imekuwa ikifichwa kwa miongo kadhaa, lakini hatimaye wanapata kutambuliwa wanavyostahili. BBC imezungumza na baadhi ya jamaa wa wanachama wa Brigedi hiyo, ambayo ilijulikana kwa jina la "6888".

Mnamo 1945, huku vita vikiendelea katika sehemu kubwa ya dunia, wanawake 855 waliitikia wito wa Jeshi la Marekani la kusaidia kutatua tatizo la barua na vifurushi vilivyokuwa vimerundikana nchini Uingereza kwa miaka miwili.

Kikosi hicho kilisafiri kwa meli kutoka Marekani hadi Uingereza, na kukaa katika mji wa Birmingham.

Meja Charity Adams, wakati huo akiwa na umri wa miaka 26, alikuwa mwanamke wa kwanza mweusi kuongoza kikosi cha Jeshi la Marekani nje ya nchi, na yeye na kitengo chake walisaidia kutatua tatizo kubwa.

Kikosi cha wanawake hao kilipewa muda wa miezi sita, lakini kilifanikiwa kumaliza kazi hiyo katika nusu ya kipindi hicho, kwani kiliunda timu zilizofanya kazi kwa zamu kwa saa 24, na kuchukua nafasi ya kupanga na kuainisha kwa herufi vifurushi milioni 17.

Kwa kufanya hivyo, wanawake hawa waliweza kuongeza ari ya askari waliokuwa mstari wa mbele ambao walikuwa wamepoteza mawasiliano na wapendwa wao nyumbani.

"Ni nadra kusikia chochote kuhusu wanawake weusi waliokuwa wakihudumu katika jeshi wakati wa Vita vya Pili vya Dunia kana kwamba waliondolewa kwenye historia," asema Kanali Edna Cummings, afisa mstaafu ambaye alihudumu katika Jeshi la Marekani kwa miaka 25.

Black women

Chanzo cha picha, US Army

Hauhitaji Whatsapp
BBC Swahili sasa kwenye WhatsApp

Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.

Bonyeza hapa kujiunga

Mwisho wa Whatsapp

Kikosi hicho cha wanawake kilikuwa na makao yake katika Shule ya King Edward, Edgbaston, Birmingham, na baadaye kuhamia Rouen na Paris nchini Ufaransa. Walikabiliwa na changamoto nyingi, zikiwemo vifaa vya kizamani, tofauti za kitamaduni na ubaguzi dhidi ya wanawake.

Wanawake hawa walifanya kazi katika majengo finyu, yenye mwanga hafifu yasiyo na joto, na rundo la vifurushi vilivyofika kwenye dari. Wengi wao walisema walikuwa wamezungukwa na panya na panya wakijaribu kupata chakula kilichoharibika ndani ya vifurushi.

Licha ya hayo, wanawake walivuka vikwazo vyote na kupata sifa dhabiti kwa ufanisi wao na kujitolea kufanya kazi.

Kitengo hicho—kilichokuwa pia na baadhi ya wanawake wa Amerika ya Kusini—kiliporudi Marekani mwaka wa 1946, hakukuwa na sherehe au kutambuliwa kwa washiriki wake kwa mafanikio yao.

Lakini baada ya karibu miaka 80, kikosi hicho hatimaye kilipata heshima iliyostahili.

Simulizi yao ni mada ya filamu ya Tyler Perry, ambayo inatazamiwa kutolewa kwenye Netflix.

Wakiiigizwa na Oprah Winfrey na Kerry Washington, wazo la filamu hiyo lilizaliwa wakati Berry alipoona nakala ya jarida la Vita vya pili vya duni kuhusu brigedia hiyo, iliyoandikwa na mwanahistoria Kevin M. Heimel mnamo mwaka 2019.

Filamu hii, pamoja na juhudi kubwa za Kanali Cummings kuangazia mafanikio ya wanawake hawa, ilitumika kama kichocheo cha kutambuliwa kwa ulimwengu wa 6888.

Ukumbusho uliowekwa wakfu kwa washiriki wa kike wa kikosi hicho uliwekwa Kansas mwaka wa 2018. Miaka mitatu baadaye, Rais Joe Biden alitia saini Medali ya Dhahabu ya Congress ya 2021 ya Sheria ya [Battalion] 6888, ambayo iliwatunuku wanawake hawa heshima ya juu zaidi ya kiraia nchini Marekani Machi mwaka jana.

Pia kuna mipango ya kutengeneza muziki kulingana na simulizi yao.

Lakini wanawake hawa walioheshimiwa ni akina nani? Waanzilishi hawa wanyenyekevu walikuwa akina mama na nyanya wapendwa, na nguzo za jumuiya zao.

Black women

Chanzo cha picha, SANDRA FRAZIER DEAN

Maelezo ya picha, Sajenti Virginia M. Flexible

Miongoni mwa wanawake waliohudumu katika kikosi hicho ni, Sajenti Virginia M. Flexible.

Katika kipindi ambacho wanawake waliondoka Marekani, mivutano ya rangi ilikuwa juu, jamii iligawanyika juu ya suala la ubaguzi wa rangi, na haki za binadamu za watu weusi zilitawaliwa na sheria za Jim Crow ambazo ziliendelea kutumika hadi miaka ya 1960.

Sheria zilipitishwa katika majimbo ya kusini mwa Amerika baada ya kukomeshwa kwa utumwa. Sheria hizi ziliwanyima watu weusi haki sawa na wazungu, na hawakuruhusiwa kutumia vifaa vya umma vya "wazungu pekee" kama vile shule na mbuga.

"Alikuwa akisimulia jinsi watu walivyomchukulia kama mwanamke mwenye asili ya Kiafrika," anasema Danielle Brown, 47, akikumbuka mazungumzo aliyokuwa nayo na nyanya yake.

"Ingawa kulikuwa na ubaguzi wa rangi nchini Uingereza, alisema watu hapa walimtendea vizuri zaidi kuliko nyumbani [Marekani], na alizungumza juu yake kwa kirefu.

"Alisema alijiona mtu hapa."

"Kuwa sehemu ya jeshi kulileta utulivu na nidhamu katika maisha yetu," anasema Sandra Fraser-Dean, 67, mamake, picha ya Sajenti Lynn, ikionekana imebandikwa kifuani mwake kwa fahari. "Ilimpa kusudi na kusudi, na alituhimiza kila wakati kufanya vizuri zaidi na kusafiri."

“Hilo lilikuwa mojawapo ya mambo yaliyomfanya apende [kutumikia jeshini], kupata fursa ya kutembelea maeneo mengine.”

Urithi wa Indiana Hunt-Martin aliwaacha akiishi katika watoto wake pia.

Alizaliwa mnamo 1922, Indiana alikuwa msafishaji kabla ya kujitolea kujiunga na Kikosi hicho cha wanawake.

"Inasikitisha sana kwamba wanawake hawa... waliweza kukabiliana na vizuizi, sio tu kwa sababu walikuwa wanawake katika jeshi, lakini pia kwa sababu walikuwa Wamarekani wenye asili ya Kiafrika, na bado hakuna aliyetuambia simulizi yao," anasema binti yake. Janice Martin.

US NATIONAL ARCHIVES

Chanzo cha picha, US NATIONAL ARCHIVES

Maelezo ya picha, Wanawake wa Kikosi cha 6888 wamesimama mbele ya sanamu ya Shakespeare huko Stratford-on-Avon.
EDNA CUMMINGS

Chanzo cha picha, EDNA CUMMINGS

Maelezo ya picha, Katika ziara iliyolenga kufuata nyayo za bibi zao, baadhi ya ndugu wa kike wa wanawake wa kikosi hicho walipiga picha inayofanana na ile waliyopiga bibi zao.

Kudharau urithi wao ( alama na mema waliyofanya) inaonekana kuwa ni sifa ya kawaida miongoni mwa wanachama wa kike wa kikosi hicho. Roger Matthews, 65, anasema mama yake, Vashti Murphy, hakuzungumzia kuhusu muda wake jeshini pia.

Lakini aliandika kuhusu kipindi hicho.

Katika nukuu zillizochapishwa na gazeti la jumuiya ya Waamerika wakati huo, Murphy alisimulia uzoefu wa kulala katika sehemu zenye "msongamano" na hamu yake kubwa ya kuoga:

"Nina furaha sana kwa sababu kwa mara ya kwanza baada ya miezi minne naweza kuoga…kwa maji ya moto.

"Maji ni magumu, lakini baada ya kuvaa kofia kwa muda mrefu, ni jambo kubwa."

Lakini inaonekana kwamba mara tu aliporudi nyumbani, aliacha kuzungumzia uzoefu wake wakati wa vita.

Ushauri wa mama

Bila Murphy kujua, tukio hili liliwahimiza wanawe kujitahidi kuzingatia ubora na kushinda vizuizi ndani ya jeshi.

Matthews alipigana katika Vita vya Vietnam na alihudumu kama Luteni wa pili kwa miaka 24.

Wakati huo mnamo 1974, ushauri wa mama yake kwake ulikuwa: "Ikiwa unapaswa kujiunga na jeshi, jiunge nalo kama afisa."

"Maneno yake bado yanasikika masikioni mwangu," Matthews anasema.

Babu yake, John H. Murphy, alikuwa mwanzilishi mwenza wa Gazeti la Afro, mojawapo ya magazeti kongwe zaidi ya Amerika yanayomilikiwa na familia ambayo bado yanachapishwa hadi leo - miaka 130 baada ya kuchapishwa kwa mara ya kwanza.

Vashti Murphy alikuwa mpiga picha, kisha mtafiti na mtunzi wa kumbukumbu wa gazeti hilo - huku akiwalea watoto wake watano.

Black women

Chanzo cha picha, USA Army

Mwanahistoria wa West Midland Gary Stewart, 51, ambaye pia ni mwanachama wa Recognize Black Heritage and Culture, alisaidia kuandaa mojawapo ya vituo kwenye ziara ya 6888 ya ndugu na jamaa za Wanawake kwenda Birmingham.

"Kwetu hapa Birmingham, simulizi hii ni muhimu sana," anasema Stewart. "Inatuwezesha kuonyesha kwamba urithi wa watu weusi katika jiji unarudi nyuma hadi mwaka 1945 au nyuma zaidi."

Simulizi ya wanawake 855 ambao walisaidia kuinua ari ya askari sio tu kwamba ilitengeneza maisha ya watoto wao na wajukuu, lakini pia ilikuwa ya umuhimu mkubwa kwa Waingereza weusi wanaoishi katika jiji hilo.

Olivia Brecon-Smith, 33, mwalimu wa hesabu katika Shule ya King Edward, alisema: “Athari ambayo kikosi cha jeshi la wanawake wote kimekuwa nayo shuleni ina maana kubwa kwangu. Ni msukumo kwangu kama mwanamke mweusi.

Nikiwa katika familia ya kizazi cha Windrush (kizazi cha wahamiaji waliokuja Uingereza kutoka visiwa vya Karibea kwenye Empire Windrush mnamo 1948), naweza kusema kwamba uzao wa kizazi hicho wanawakilisha jamii kubwa huko Birmingham, lakini haipati kutangazwa inavyostahili, na ujuzi wa watu ambayo 6888 ilitumikia hapa ni muhimu sana kwa historia ya Birmingham.

"Wanafunzi watajiamini zaidi na wataweza kuwa na matarajio makubwa wakati wanajua kuwa sio muda mrefu uliopita kitengo kizima kilikuwa kikileta mabadiliko, kubadilisha ulimwengu na kubadilisha mitazamo, na wao pia wanaweza kuwa sehemu ya kizazi kijacho ambacho kitafanya kitu kama hicho. .”